Thursday, August 18, 2022

TUMETIMIZA MIAKA 18 BILA PATRICK BALISIDYA

Patrick Balisidya, nyuma yake Salim Willis

Mwaka 1974 mwezi wa sita, ulikuwa mwezi wa furaha kwangu na wenzangu wa Operesheni Ukombozi pale Ruvu JKT.

Tulikuwa tumemaliza miezi sita ya kutumikia Jeshi la Kujenga Taifa ‘kwa mujibu wa sheria’. Mafunzo ya miezi sita yaliyoanzia kambi ya Mafuleta kule Handeni na kukakamilika katika kambi kubwa ya Ruvu, mkoa wa Pwani. Miezi sita iliyojaa visa na vituko  vingi vya ujana, marafiki wapya, na shughuli nyingi za kujenga ukakamavu,  kama vile mchakamchaka kila asubuhi, paredi, route march na mazoezi mbalimbali ya kivita na  kazi mbalimbali zikiwemo kilimo cha mpunga, ufugaji wa kuku na ng’ombe, hakika hakukuweko muda uliokosa shughuli. Hatimae siku ya mwisho ilifika tukafanya paredi kubwa ya kumaliza mafunzo, chini ya Mkuu wa Kambi Marehemu Meja Jenerali Rashid Makame. 

Baada ya paredi ya 'Pass Out', kulikuwa na shamra shamra nyingi za kumaliza mafunzo  zilizoishia na dansi lililoporomoshwa na bendi ya Afro 70.
Pamoja na kuwa nilikuwa nafahamu habari za bendi hii na pia nilishaanza kununua santuri zao toka mwaka 1973, siku hiyo ilikuwa siku ya kwanza kuiona bendi hiyo ikiwa jukwaani. Ilikuwa furaha juu ya furaha. Furaha ya kumaliza muda wa kulitumikia Jeshi la Kujenga Taifa juu yake furaha ya kuiona Afro70, bendi tuliyozowea kuiita Afrosa, kutokana na jina la mtindo wa muziki wake.
Dansi lilianza kama saa tatu usiku hivi baada ya chakula cha jioni, Afro 70 hawakutuangusha, na nyimbo zao zilizokuwa maarufu ziliporomoshwa usiku kucha, Dirishani, Weekend, Dada Rida, Pesa, Tausi na nyingine nyingi, pia bendi ilipiga nyimbo za wanamuziki waliopendwa miaka hiyo akina Clarence Carter, Otis Redding, James Brown, Aretha Franklin, ilikuwa raha kubwa. Sharti la muziki wa siku hii ya mwisho ilikuwa ni bendi kupiga muziki mpaka jua litakapochomoza kwani mabasi yalikuja mapema ili kuondoka na askari tuliokuwa tumemaliza muda kurudi makwetu. Alfajiri tulitoka kwenye muziki na masunduku yetu na kuingia kwenye mabasi kurudi makwetu.
Nimekumbuka sana siku hii kwa kuwa mwezi huu tunatimiza  miaka kumi na nane toka tulipo mzika Patrick Balisisdya, mtunzi, muimbaji, mpiga gitaa na kiongozi wa bendi ya Afro 70 pale makaburi ya Buguruni Malapa.

Patrick Pama Balisidya alizaliwa Mvumi Dodoma tarehe 18 April 1946. Mama yake alikuwa anapiga kinanda kanisani  hakika Patrick angeweza kujisifu kuwa muziki uko katika damu yake. Alianza kushiriki katika mambo ya muziki mapema na hata kuwa kiongozi wa Bendi ya shuleni kwake pale Dodoma secondary School. Alipomaliza shule ya sekondari akajiunga na Chuo cha Ufundi Dar es salaam, maarufu wakati huo kwa jina la Dar Technical, baada ya kumaliza mafunzo Dar Tech, alifanya kazi hiyo kwa muda na 1967 akawa tayari anapiga muziki Dar Es Salaam Jazz B.
Bendi hii ilikuwa inafanya kazi nzuri sana hivyo kuanza kuwa tishio kwa bendi kongwe Dar es Salaam Jazz Band yenyewe ( Majini wa bahari), na hivyo uongozi wa Dar Jazz ukaamua kuivunja bendi hiyo ndogo kabla haijaipoteza kabisa bendi kaka. Patrick hakufurahishwa na hatua hiyo, kufikia mwaka 1970 Patrick alikuwa ameanzisha kikosi chake mwenyewe kilichoitwa Afro70, kikiwa na mtindo wake Afrosa.
Mkongwe Shebby Mbotoni aliwahi nihadithia jinsi walivyokuja na wazo la kuanzisha bendi ya Afro 70, bendi iliyokuja kumtambulisha Patrick ulimwenguni. Shebby alisema siku moja alikuwa kwao akipiga gitaa, ndipo Patrick alipomkuta wakati akiwa anamtafuta rafiki yake aliyekuwa amepanga nyumba hiyo aliyokuwa akiishi Shebby. Basi alijitambulisha na wakaanza urafiki na ndipo likaja wazo la kuanzisha bendi,  na hatimae ikazaliwa Afro 70,
 Patrick alikuwa  mbunifu katika muziki wake, na kwa muda mrefu alikwepa sana kuingia katika wimbi la kufuata mapigo ya Kikongo kitu ambacho hata wakati huo bendi nyingi zilikifanya, hata bendi aliyokuwa akipigia, Dar es Salaam Jazz Band ilikuwa katika mkumbo huo wa kuiga bendi za Kikongo. Msimamo wa Patrick uliyumba baada ya kukutana na Franco wakati bendi ya TP OK Jazz ilipofanya ziara yake ya kwanza  nchini mwaka 1973, Patricka akaanza kuiga staili ya upigaji gitaa wa Franco. Wimbo wake wa Umoja wa kinamama, ulikuwa wazi umeiga sehemu kubwa wimbo wa Georgette wa TP OK Jazz.  

Afro70 ilipata bahati kuwakilisha wanamuziki wa Tanzania katika maonyesho ya mtu mweusi Lagos, Nigeria. (FESTAC festival 1977). Bahati hii ilikuja baada ya Afro 70 kushinda mashindano ya bendi yaliyoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, kwa ajili ya kupata muwakilishi wa kwenda kwenye Tamasha hilo.  Baada ya mashindano, bendi ilipata fursa ya kuzunguka sehemu mbalimbali nchini kuonyesha kilichowafanya washinde na pia kupata mazoezi zaidi kabla ya safari ya kwenda Lagos. Lakini  bahati mbaya wakati wa kurudi Dar gari lao lilipata ajali na vyombo vya bendi vyote viliharibika. Wakati huohuo  Wizara ya Utamaduni ilikuwa imenunua vyombo vipya kwa ajili ya kuanzisha bendi yake, vyombo hivyo ilikabidhiwa Afro 70 kuvitumia FESTAC. Baada ya kurudi kutoka Nigeria Afro 70 waliamuliwa kurudisha vyombo vile serikalini, na  pia baada ya kurudi Festac bendi ilianza kusambaratika haikufanya onyesho tena kama Afro 70. Afro 70 ikafa rasmi.
Vyombo vile viliporudishwa serikalini vilitumika kuanzisha bendi ya Wizara ya Utamaduni iliyoitwa Asilia Jazz Band. Mwaka 1979, Balisidya alikwenda Sweden na kushirikiana na kikundi cha Archimedes akatoa album nzuri sana iliyoitwa Bado Kidogo. Patrick pia alipitia Orchestre Safari Sound, (Masantula) na kupiga piano katika ule wimbo maarufu, ‘Unambie siri’, alipitia pia bendi iliyoitwa Rainbow Connection, nakumbuka kukutana nae nilipotaka kujiunga na bendi hiyo wakati ikipiga pale New Africa Hotel, lakini Patrick akanishauri nisijiunge kwani alisema kuwa hakuwa anaona maendeleo yoyote katika bendi ile. Utabiri ambao ulikuja kuwa kweli bendi ilikuja kusambaratika.
Kwa kweli nyimbo za Patrick zilizokuwa juu katika chati ni nyingi,  Harusi, Dirishani, Weekend, Tausi, Pesa, Nakupenda kama Lulu, Ni mashaka na mahangaiko, Afrika, na nyinginezo nyingi. Patrick alifariki tarehe 7, Agosti 2004 na kuzikwa 12 Agosti katika makaburi ya Buguruni Malapa.

MUNGU AMLAZE PEMA PATRICK BALISDYA

 

KIKI, PROMO, PROPAGANDA, WATOTO WA BABA MMOJA

 


Kiki ni neno ambalo limekuwa maarufu zama hizi za Bongofleva. Kiki ni neno lilitokana na neno la Kiingereza, ‘kick’ yaani teke. Hivyo kiki maana yake katika ulimwengu wa wasanii ni kutafuta tukio ambalo litashtua jamii na kupaisha sifa yao au ya kazi yao. Ni kama vile ambavyo ukimpiga teke chura ndio unamsaidia kuruka. Hivyo wasanii wa zama hizi hutafuta kiki za aina mbalimbali ili kupaisha sifa za kazi zao, wengine hujitangaza kuwa wamefariki, wengine utakasikia wamefumaniwa, au wengine wameachana au wengine kutangaza wamerudiana au wameoana, au mara nyingine kueneza taarifa kuwa wimbo wao umeibiwa studio, na imefikia hata wazazi wa wasanii wengine kuingia kikamilifu katika shughuli za kiki kwa kutoa matamshi tata kuhusu kazi za watoto wao ili tu watu waelekeze masikio na macho yao kwenye kazi mpya. Pamoja na neno kiki kuwa jipya lakini hakika kutafuta kiki hakukuanza na Bongofleva. Makampuni yenye kutaka kutangaza bidhaa mpya sokoni, yamekuwa yakifanya matukio mengi makubwa kutafuta kiki. Makampuni hupitisha magari yenye maspika makubwa mitaani na kutangaza bidhaa zao, au hufanya matamasha makubwa, au huanzisha hata misemo tata ili tu kupata kiki ya bidhaa zao. Lakini hapa haiitwi kiki inaitwa promosheni. Wanasiasa nao hakika ni mabingwa wa kiki,wakati wa kutafuta kura, kila aina ya vituko hufanyika. Tumeshaona wanasiasa wanapiga magoti kuomba kura, wengine hata kugaragara chini wakiomba kura, hao wanaoamua kucheza ngoma za kiasili au dansi jukwaani ni kawaida sana.  Na wakifungua mdomo kueleza sifa walizonazo na watakachokifanya vyote ni kujinadi ili kuonekana bora, ila huku haiitwi kiki inaitwa siasa, au wengine huiita propaganda. Zama hizi hata viongozi wa dini nao wamo katika kutafuta kiki, utasikia wakishusha sifa za uwezo wao kama katika vyombo mbalimbali vya matangazo, wengine wamefikia mpaka kuingilia matatizo ya wasanii maarufu ili nao wajulikane kuwa wapo. Kutokana na malezi duni ya baadhi ya wasanii, kiki hizi zimekuwa zikichukua sura mpya siku hadi siku. Kwa sasa zimefikia hata kuongea, kutangaza au kuonyesha vitu vya faragha hadharani, ikiwa kama njia ya kutafuta kiki, na hapo ndipo ugomvi na watu wenye busara zao unapoanza.

Kama nilivyosema mwanzo neno kiki ni geni lakini shughuli zake si ngeni kabisa. Bendi za zamani zilikuwa na njia kuu moja tu ya kupata pesa nayo ilikuwa kwa  kiingilio mlangoni, gate collection, na hakika kulilazimika kuweko na mbinu za kujitangaza, au kutafuta kiki. Kulikuwa na njia kuu tatu za kutangaza onyesho,  kwanza ni kupitia redioni na pili kupitia magazeti, na tatu kwa kubandika matangazo kwenye kuta na nguzo za umeme. Magazeti yaliyokuwa yakishughulika na muziki yalikuwa ni magazeti ya serikali, magazeti ya Chama Cha Mapinduzi na magazeti ya chama cha wafanyakazi, NUTA na baadae JUWATA.  Vyombo hivi havikuwa na maadili ya kuruhusu ‘kiki’ za maisha binafsi ya wanamuziki, matangazo yalilazimika kuwa yanayohusu muziki tu.  Hivyo ubunifu ulikuweko, bendi zilijinadi kwa staili zake zenye mvuto ili kutafuta kiki. Kulikuweko staili kama  Katakata mwendo wa jongoo vumbi nyuma, Bomoa tutajenga kesho, Super mnyanyuo, Sikinde ngoma ya ukae, Mahepe ngoma ya wajanja, Dunda dunda, Bayankata, Kokakoka balaa  na majina mengine mengi. Matangazo kwenye magazeti yaliwekwa picha za wanamuziki au kuchorwa picha za kujinadi kwa njia moja au nyingine. Maswala ya kuachana, kupendana, kuhongana, kufumaniana hayakuhusika kabisa katika kutangaza kazi ya muziki. Nikifikiria sana nadhani vitu ambavyo wasanii wa sasa hufanya katika kutafuta kiki, vingefanywa na wasanii wa miaka ile na kutangazwa kama ilivyo sasa ingekuwa ndio mwisho wa msanii huyo, jamii ingemtema.

Nadhani moja ya sababu ya kuweko kwa kiki za ajabu katika zama hizi, ni kujaribu kujazia mapungufu yaliyomo kwenye sanaa husika. Msanii anakuwa anajua hata yeye kuwa kazi yake ni duni,  hivyo anazua kitu kisichohusika kabisa na kazi yake ya sanaa ili kuweza kuwafanya wateja japo wasikilize kazi yake kwa muda.

Taratibu za kurekodi siku hizi nazo zinafanya msanii asiwe na uhakika wa mpokeo ya wimbo wake hivyo kulazimisha vituko ili kujulikana kama ana kazi mpya. Msanii wa kizazi cha sasa anaweza kutunga wimbo asubuhi akaingia studio na kukamilisha wimbo na jioni wimbo uko tayari youtube na umeanza kurushwa kwenye vyombo ya utangazaji mbalimbali,

Hali haikuwa hivyo zamani, ukiwa na wazo la wimbo unalipeleka kwenye bendi yako yenye watu zaidi ya saba, wao wanakusikiliza na kuamua kama uchukuliwe na bendi au la, wakikubali ndipo mnaanza kuujenga wimbo, magitaa, ngoma. vyombo vya upulizaji, kila mtu anatoa wazo lake. Wimbo ulichukua japo siku mbili kukamilika, ingawa kuna nyimbo zilichukua hata zaidi ya wiki kuwa tayari. Bendi ikiridhika , wimbo ulianza kupigwa kwenye maonyesho, na hapa ndipo wapenzi wa bendi walikuwa wakiingia na kutoa maoni yao, mkikubaliana ndipo unaenda kurekodiwa. Mara nyingi bendi zilikuwa zinajua kabla hata ya kwenda kurekodi wimbo gani utakuwa maarufu kutokana na maoni ya wapenzi. Kwa taratibu hizo kiki za kujidhalilisha zilikuwa hazina nafasi, kazi ilikuwa inajiuza yenyewe.

Wednesday, August 17, 2022

SHAW HASSAN SHAW, MPIGA KINANDA ALIYEWAHI KUPANDA JUKWAANI AKAKUTA AMESAHAU KUPIGA NYIMBO ZOTE

Shaw Hassan Shaw
Kwa wapenzi wa nyimbo za Vijana Jazz Band hakika watakuwa wanakumbuka vile vipande vya kinanda vilivyokuwa vikianzisha zile nyimbo mbili alizokuwa akiimba Kida Waziri, Penzi Haligawanyiki na Shingo feni. Mpigaji wake alikuwa Shaw Hassan Shaw Rwamboh. Mwanamuziki huyu alizaliwa tarehe 25 September 1959, Dar Es Salaam. Alianza kujifunza kupiga gitaa na wenzie kando ya Ziwa Tanganyika huko Kigoma, wakitumia magitaa ya tajiri mmoja aliyekuwa na meli ya uvuvi. Alipokuja Dar es Salaam akakutana na mwanamuziki Zahir Ally Zorro, Zahir ndiye aliyeboresha upigaji wake wa gitaa kiasi cha kukubaliwa na Patrick Balisidya kupiga gitaa la rythm katika bendi yake ya pili PAMA Band, chini ya Afro70.

Shaw Hassan Shaw wa kwanza kulia aliyenyoosha mkono. Mwendeshaji wa blog hii John Kitime wa kwanza aliyesimama kushoto. Hapa wakiwa Stadium Morogoro wakingojea onyesho la kumkaribisha Nelson Mandela.

Ni chini ya malezi ya Patrick alipojifunza kupiga Keybords (Kinanda). Baada ya hapo aliacha muziki na kujiunga na Dar Technical College. Lakini 1980 alijiunga na Vijana Jazz kama mpiga Keyboards, alishirikiana na wanamuziki wengi lakini wengi kwa mapenzi ya Mungu,  wametangulia mbele ya haki. Baadhi ya waliobaki kati ya aliyokuwa nao wakati huo ni John Kitime, Kida Waziri, Saad Ally Mnara, Hamisi Milambo, Huluka Uvuruge, Hassan Dalali, Hamza Kalala na Rashid Pembe. Mwaka 1990 alijiunga na Orchestra Safari Sound, chini ya Maalim Muhidin Gurumo (MJOMBA) na Marehemu Abel Baltazar, hapa alikutana na akina Benno Villa Anthony na Mhina Panduka (Toto Tundu) .Aliacha bendi baada ya miezi sita tu, mwenyewe anasema, ‘….kutokana na muhusika kutozingatia mkataba wangu…’. Alihamia Zanzibar na kujiunga na bendi iliyokuwa ikipiga Mawimbini Hotel, hakukaa sana kwani Washirika Tanzania Stars walimwita. Hapa akakutana na mwalimu wake wa gitaa Zahir Ally, Ally Choki, Musemba wa Minyugu,Tofi Mvambe, Abdul Salvador na wengine, ilitokea kutoelewana baina ya wanamuziki na yeye kama kiongozi wa bendi ilibidi aachie ngazi kuepusha bendi kuzidi kujichanganya. Baada ya hapo Kanku Kelly ambaye ni mume wa dada wa mke wake alimuita ajiunge na Kilimanjaro Connection Band. Anasema Kanku alimvumilia sana kwa kuwa alikuwa hajawahi kufanya kazi ya kukopi nyimbo za wanamuziki wengine wakubwa duniani, hatimae akaweza kujiendeleza na kuweza kumudu kupiga vitu vikubwa, bendi hii ya Kanku  ilikua inazunguka kwa kupiga muziki hotel mbalimbali katika nchi za Malaysia, Singapore, Indonesia, Thailand na Japan jambo ambalo lilifanya aone kila kitu ni kigeni kila alipokwenda. Katika bendi hiyo alishirikiana na akina Kanku Kelly, Mafumu Bilal, Maneno Uvuruge, Burhan Adinan, Shomari Fabrice, Bob Sija, Fally Mbutu, Raysure boy, Delphin Mununga na Kinguti System. Baadaye Shaw, Kinguti na Burhan Muba waliamua kuanzisha kundi dogo wakitumia sequencer keyboards na kumuaga Kanku Kelly. Group hili lilijiita Jambo Survivors Band, bendi ambayo itakumbukwa  kwa ule wimbo Maprosoo ulioimbwa na MlasiFeruzi ambao uliokuwa katika album ya MAPROSOO.
Mlasi feruzi
Baada ya hapo bendi ikaanza kuzunguka nchi mbalimbali ikipiga katika mahotelini. Kupitia muziki Shawa amekwisha fika Oman , Fujairah, U.A.E, Singapore, Malaysia na Thailand. Shaw anasema wanamuziki ambao hatawasahau kwa kuwa wamemfikisha alipo ni Zahir Ally Zorro, Marehem Patrick Balisdya, Waziri Ally, Kinguti System, Burhan Muba na Kanku Kelly. Kituko ambacho hawezi kusahau ni nchini Malasyia wakati akiwa na Kanku Kelly na ikiwa ni mara ya kwanza kwake kupiga muziki akiwa amezungukwa na watu weupe watupu. Anasema nyimbo zote zilipotea kichwani akawa hakumbuki hata nyimbo moja aliyokuwa kafanyia mazoezi

MJUE JEAN 'JOHNNY' BOKELO ISENGE

 

 


 Jean ‘Johnny’ Bokelo Isenge alizaliwa mwaka 1939 nchini Kongo, nje kidogo ya jiji la Kinshasa. Familia yake ilikuwa ni ya wanamuziki. Johnny alikuwa mdogo wa Paul Ebengo’Dewayon’ Isenge mwanamuziki mwingine aliyekuwa mkubwa sana nchini Kongo toka mwanzoni mwa miaka ya 50. Huyu Dewayon alikuwa na bendi inaitwa Watam, hapa ndipo Johnny alipoanzia muziki akipiga na mtoto mwingine aliyekuja kutikisa ulimwengu wa muziki Franco Luambo Luanzo, wakati huo Franco akiwa na miaka 12 tu. Johnny Bokelo aliendelea kupiga katika bendi alizoanzisha kaka yake kama vile Conga Jazz na Orchèstre Cobantu, lakini mwaka 1958 Johhn akaanzisha bendi yake, Orchestre Conga Succès, akiwa na mdogo wake Mpia Mongongo maarufu kwa jina la Porthos Bokelo, ambaye alikuwa mpiga gitaa la rhythm mahiri sana. Kaka yao Dewayon, akaja kujiunga na kundi hilo1960 lakini miaka miwili baadae1962 Johnny na kaka yake wakatengana. Bokelo alifanikiwa kulijenga kundi lake kuwa na nguvu na likawa kwa namna fulani linafanana sana na OK Jazz. Hata tungo nyingine zilikuwa ni za kujibu tungo za OK Jazz au kuzungumzia mada ambayo imeanzishwa na OK Jazz. Hii haikuwa kwa ugomvi bali kutokana na ukaribu uliokuwa kati ya Franco na Johnny. Kuna wakati Bokelo alianzisha mtindo wa kutunga nyimbo alizozipa jina la Mwambe, kukawa na Mwambe no 1 na 2 mpaka 5 ambapo alikuwa akiongea na kushangaa jamii inaelekea wapi. Upigaji wa Bokelo Dewayon na Franco ulishabihiana, pengine ni kutokana na wote kuanzia Watam. Mwaka 1968 Johnny Bokelo akabadili jina la kundi lake la Conga succès” na kulita “Conga 68” akaanzisha label yake akaanza kutoa santuri, hii ilimuongezea kipato japo wanamuziki wake walitishia kuachana nae kwani walisema hawakuwa wanapata fedha zozote kutokana na mradi huo. Santuri nyingi wakati huu alikuwa akiziachia kwanza kutoka Ufaransa ili kupata mapato zaidi. Kati ya 1972 mpaka 1974 Bokelo Isengo alikuwa anatumia muda mwingi zaidi akiwa studio, kwenye mwaka 1970, viwanda vya kutengeneza santuri vya Kinshasa vikawa vimechoka hivyo bokelo akaanza kupeleka master zake Kenya ili kutengeneza santuri. Mwaka 1980 Bokelo aliachana sana na shughuli za muziki.

Bokelo alifariki 15 January 1995 baada ya kuugua kwa muda mrefu

 

 



Friday, August 12, 2022

HAKIKA DANSI LIMEBADILIKA SANA

 


Kweli dansi limebadilika sana.

Kumbukumbu zangu huwa zinanirudisha Iringa nilipokuwa na umri wa miaka minne hivi. Nadhani ndipo nilipoanza kutambua kuwa wazazi wangu walikuwa wanajitayarisha kwenda dansini, nakumbuka wakituaga na kutumbuambia ‘Haya laleni sisi tunaenda dansini’. Moja ya dansi nakumbuka lilikuwa limepigwa na Cuban Marimba wakiongozwa na Salum Abdallah, nakumbuka kwa sababu kesho yake Mwalimu Nyerere alikuja kuhutubia kwenye uwanja ambapo upo sasa ni uwanja wa Samora. Wakati huo ulikuwa ni uwanja wa mpira wa shule ya Middle School na baba yangu alikuwa Headmaster wa shule ile, na nyumba yetu ilikuwa pembeni tu ya uwanja huo wa mpira.
Siku alipokuja kuhutubia Mwalimu Nyerere, wimbo uliokuwa ukisikika kwenye spika ukirudia rudia, ulikuwa wimbo wa Cuban Marimba na baadhi ya  maneno yake yalikuwa ‘ Tutie jembe mpini, twendeni tukalime’. Mama akatuambia na wadogo zangu kuwa wimbo huo walikuwa wameucheza jana yake dansini. Kwa kweli toka nikiwa mtoto, dansi kwangu ni neno la furaha  kwenye maisha yangu. Nikiwa mdogo  wazazi wangu walikuwa wakituonyesha namna ya kucheza aina mbalimbali za dansi, zikiwemo tap dancing, aina ya dansi ambayo viatu lazima uvigonge sakafuni wakati wa kucheza kufuatia mapigo ya muziki, wazazi walitufundisha kucheza  chacha, waltz na aina nyingine za dansi ambazo sijapata hata  kujua majina yake.
Nyakati hizo na miaka mingi baadae, mtu akiaga anakwenda dansini, jambo la muhimu atakalolifanya huko ni kucheza nyimbo nyingi kadri atavyoweza. Kesho yake mazungumzo kuhusu dansini ni kuulizana nyimbo ngapi zilichezesha. Mpenzi wa muziki kurudi nyumbani akiwa kachoka kwa kucheza ilikuwa ndio dalili ya kufurahia kwa usiku ule.

Miaka mingi baadae hatimae nikaja kuwa mwanamuziki wa muziki wa bendi,  aina ya muziki ambao miaka ya 80 ulianza kuitwa muziki wa dansi, ulipewa jina hili kuutofautisha na aina nyingine za muziki kama vile taarab,  kwaya, muziki wa asili na aina nyingine za muziki. Muziki huu wa dansi ulikuwa ni ule uliopigwa kwa vifaa vya kisasa na kutegemea kuwa lazima utachezwa, tena kwa mtindo maalumu.  
Katika miaka ya hamsini na mwanzoni mwa miaka ya sitini, bendi zilikuwa zikitangaza aina muziki itakaoupiga, kwa mfano kiongozi wa bendi aliweza kutoa maelezo yafuatayo kabla ya kupiga wimbo. ‘ Muziki ufuatao unaitwa Dada Adija, umepigwa katika mtindo wa Cha Cha’. Basi muziki ukianza wapenzi wa muziki huingia uwanjani na kuonyesha umahiri wao wa kucheza ChaCha. Na hivyo hivyo kama wimbo ni Twist, Bolelo, Charanga na kadhalika. 

Utunzi wa zamani

Utunzi wa nyimbo mpya za bendi ulikamilishwa kwa muungano wa mawazo kutoka kwa wanamuziki mbalimbali katika bendi. Mtunzi wa awali aliweza kuleta  mashahiri, mara nyingine yakiambatana na melodia na kuwaimbia wenzie ambao kama wangeukubali, walianza kutunga vipande mbalimbali vya wimbo kupitia  vyombo mbalimbali wanavyovipiga. Tungo nyingi za awali zilianza kwa rumba, na ilipofika katikati mwendo ulibadilika na kuingia katika kile tulichokuwa tukikiita ‘chemka’.
 Chemka mara nyingi ilianza kwa kuimba na kisha kuingia kipande cha gitaa la solo. Hapa ndipo wapiga solo walikuwa wakipimwa kwa umahiri wao wa kutunga na kupiga vipande vya solo ambavyo vingeweza kuwateka akili wasikilizaji na kuwafanya wacheze dansi.
Katika bendi nilizopitia kama vile TANCUT Almasi na Vijana Jazz Band, baada ya bendi kukamilisha wimbo, ulianza kupigwa katika maonyesho mbalimbali, lakini jambo la muhimu ambalo wanamuziki wote tulikuwa tunaliangalia lilikuwa Je, watu wanaucheza wimbo mpya? Ikionekana wimbo  umekosa hamasa ya kuwasimamisha  wachezaji, wimbo huo ulirudishwa mazoezini na kubadilisha vitu tulivyohisi vinafanya watu wasipende kucheza wimbo ule. Na mara nyingine wimbo huo ulitupwa pembeni moja kwa moja kama haukuchezesha, mamia ya nyimbo  katika bendi mbalimbali ziliishia kupigwa kwenye kumbi mara moja tu na hazikurudiwa tena, kwa kuwa tu watu hawakuchangan mkia kuzicheza.
Siku hizi mambo yako tofauti kabisa, unaweza kuingia kwenye onyesho la muziki wa Taarab, muziki ambao kwa asili ulikuwa ukisifika kwa kuwa muziki wa kusikiliza tu, ukakuta wapenzi wakitiririka jasho kwa kucheza nyimbo mbalimbali za Taarab, halafu ukaingia katika onyesho la ‘muziki wa dansi’, ukakuta waimbaji wakitoka mishipa ya shingo lakini hakuna anaeshughulika kucheza dansi hilo. Kama ingekuwa  zamani, hiyo ni dalili ya moja kwa moja kuwa muziki huo hauwafurahishi wapenzi. Lakini hizi ni zama nyingine.

Katika zama hizi, bendi huwa na wacheza show wake au hata waimbaji nao wakatengeneza show, kisha wakawa wanapiga muziki na kucheza wao wenyewe. Sijui nilinganisha na kujitekenya halafu kucheka mwenyewe?
Teknolojia imeleta aina nyingine ya kuonyesha upenzi na unazi wa muziki. Wapenzi wa muziki siku hizi huonyesha upenzi wao wa muziki kwa kuchukua simu na kurekodi video za  bendi zikiimba na kucheza, wao wenyewe wakiwa wamekaa kwenye viti wakiendelea kunywa vinywaji vyao, kisha vipande hivi vya video husambazwa kwenye makundi ya Whatsapp, vikiambatana na sifa kuhusu ubora wa bendi hizi. Ndio namna ya ‘ku appreciate’ muziki zama hizi.
Lakini pia kuna madansi ambayo utakuta wapenzi wamechangamka wanacheza sana, lakini ukiangalia kila mtu anacheza akili inavyomtuma, hakuna tena mpangilio wa kucheza staili maalumu ya muziki. Ile staili ya wapenzi kukumbatiana kwa hisia wakati wa kucheza rumba imepotea, si ajabu kabisa kumkuta mtu na mpenzi wake wanacheza wimbo wa taratibu, lakini kila mtu na staili yake na juu ya hayo kila mmoja anatuma meseji kwenye simu yake.
Hakika dansi limebadilika sana

 

Wednesday, August 10, 2022

WANAMUZIKI WA SASA WANAKUBALI KUKOSOLEWA?

 

Top Ten Show 1989

Jana nilikuwa naangalia maktaba yangu ya kanda za video za zamani, nikaiona kanda moja iliyonirudisha miaka mingi sana nyuma. Ilikuwa ni kanda ya video ya onyesho moja la bendi ya Tancut Almasi Orchestra lililofanyika katika ukumbi wa klabu ya bendi hiyo eneo la Sabasaba pale Iringa.
Mwaka 1989 yalianza kufanyika mashindano ya bendi yaliyoitwa Top Ten Show, mashindano haya yalifikia kilele mwaka 1990. Yalikuwa ni mashindano makubwa sana ya muziki wa dansi na mpaka leo hayajawahi kufanyika mashindano ya bendi yenye ukubwa ule. Mashindano haya yaliyotayarishwa kwa ushirikiano wa CHAMUDATA, Radio Tanzania na Umoja wa Vijana wa CCM, yalianza tarehe 29 Julai 1989 na kufikia kilele tarehe 25 November 1989. Bendi zilizoshiriki zilikuwa 50 kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Arusha , Kilimanjaro, Tanga, Iringa,  Mbeya,  Morogoro, Rukwa , Kigoma na Pwani. Hii ilikuwa maendeleo kwani Top Ten Show ya mwaka 1988 ilikuwa na bendi 27 tu. Wafanyakazi wa Radio Tanzania Dar es Salaam  walizunguka katika mikoa mbalimbali na bendi za huko zilifanya maonyesho ambayo yaliyorushwa ‘live’  redioni na hivyo kuwapa wasikilizaji nchi nzima nafasi ya kusikiliza na kufuatilia mashindano hayo katika hatua zote.  Mwaka huo nilishiriki mashindano haya wakati nikiwa mmoja wa wanamuziki wa bendi ya TANCUT Almasi Orchestra iliyokuwa na masikani yake mjini Iringa.  Masharti ya mashindano tulipewa mapema sana. Kila bendi ilitakiwa ijitayarishe kwa nyimbo tatu, mmoja uwe unaitwa Nakulilia Afrika, wimbo wa pili ulikuwa lazima utokane na wimbo wa tuni ya asili ya kabila mojawapo la Tanzania na wimbo wa tatu uwe wimbo wowote ambao bendi ilipendelea kuupiga. Tulianza kufanya mazoezi makali  ya nyimbo hizo. Marehemu Kasaloo Kyanga na pacha wake Kyanga Songa wakaja na tungo yao ya wimbo Afrika Nakulilia, na mimi nikatoa mchango wa wimbo wa asili ya Kihehe ulioitwa Lung’ulye, kwa pamoja tukaamua kuwa wimbo wetu wa tatu uwe Ngoma za Afrika uliokuwa utunzi wa Kalala Mbwebwe.
Baada ya mazoezi makali tuliamua kufanya onyesho lisilo la kiingilio na kuwakaribisha wapenzi wa muziki wa dansi pale Iringa kuja kutoa maoni yao kuhusu matayarisho yetu hayo.  Mkuu wa Mkoa wa Iringa wakati huo, Mama Mary Chipungahelo alikuwa mgeni rasmi  wa onyesho hilo. Kilichofanyika pale siku ile, kilikuwa si kitu ambacho naona kitawezekana kwa urahisi katika zama hizi. Baada ya kupiga nyimbo zile wapenzi walikaribishwa jukwaani  kuongea ukweli kuhusu nyimbo zile, tuliomba waliotaka kutoa sifa wakae nazo, tulichokuwa nania nacho ni mapungufu katika matayarisho hayo. Hakika kulikuweko maneno makali ambayo sidhani wasanii wengi siku hizi wangekubali kukosolewa vile. Kulikuwa na kukosoa kuanzia mavazi, uchezaji na hata tungo zenyewe. Tungo ya Afrika Nakulilia iliyotungwa na akina Kasaloo ilikataliwa kwani ilionekana ilitokana na wimbo wa Pepe Kalle, hivyo muimbaji Kalala Mbwebwe na mpiga gitaa la solo Kawele Mutimwana wakaleta tungo nyingine ambayo ndio ilikuwa moja ya kete zetu katika mashindano yale.



Baada ya kuvuka kigingi cha wapenzi wetu wa Iringa, tulikuja Dar es Salaam na tulikuwa tumepangiwa katika kituo cha ukumbi wa Silent Inn uliokuwa eneo la Mpakani Dar es Salaam. Katika onyesho hilo, tulikuwa jukwaani pamoja na bendi iliyokuwa ikiitwa Orchestra Linga Linga Stars wakati huo muimbaji wake mahiri alikuwa Karama Regesu ambaye kwa sasa yupo Msondo Music Band. Tancut tukaibuka kuwa katika bendi kumi bora na kuja kushiriki fainali za onyesho lile zilizofanyika uwanja wa Taifa. 
Baadhi ya bendi zilifika kumi bora  zilikuwa, Tancut Almasi, Super Matimila, MK Group, Salna Brothers, Varda Arts, Bima Lee, Kilimanjaro Band na Vijana Jazz Band, hakika Uwanja wa Taifa palipendeza siku ile. Lakini kwangu mimi mambo yalikuwa na utata kidogo kwani siku ya fainali, nilikuwa nimeshamia Vijana Jazz Band, lakini kwa siku hiyo nilirudi bendi yangu ya zamani ya  Tancut Almasi  kwani wakati wa mashindano nilishiriki katika bendi hiyo. Uwanja wa Taifa ulijaa wanamuziki wengi sana, na kwa kuwa bendi zilikuwa na ustaarabu wa kuvaa sare, basi sare za aina mbalimbali zilitawala siku hiyo.

Ushindi wa TANCUT

 Hatimae matokeo yalitangazwa na kila wimbo ulikuwa na mshindi wa kwanza mpaka wa kumi, washindi watatu wa kwanza wakipata zawadi mbalimbali. Wimbo wangu wa asili ya Kihehe, ulishinda zawadi ya kwanza katika nyimbo za kiasili na washiriki wote tulipewa ‘radio cassette’ zilizotolewa na Ubalozi wa Uholanzi. Wimbo Afrika Nakulilia ulishika nafasi ya pili na wimbo uliokuwa chaguo la bendi ulikuwa Ngoma za Kwetu uliokuwa utunzi wa Kalala Mbwebwe ulichukua nafasi ya nne katika kundi lake, Kwa ujumla matokeo yalikuwa mazuri sana kwa bendi ya TANCUT Almasi.
Wanamuziki na viongozi wa TANCUT ALMASI Orchestra wakiwa na zawadi zao


 Art Critic

Katika nchi ambazo sanaa imekuwa, huwa kuna watu wanaoitwa ‘art critics’, hawa kwa kweli ni mabingwa katika fani za sanaa wanazo shughulikia na wao kazi yao moja kubwa ni kukosoa kazi mbalimbali za sanaa na hatimae hata kuzipa grade. Kwa mtizamo wa haraka haraka utaweza kudhani kuwa kukosoa kwao kunaweza kuharibu soko la sanaa husika, lakini kwa kuwa hawa watu huwa wakweli na wenye uzoefu, wasanii huwa wanafuatia sana watu hawa wanasemaje kuhusu kazi zao. Kupasishwa na watu hawa hupandisha thamani ya sanaa husika. Wakosoaji hawa pia huwafanya wasanii wawe makini katika kazi zao na hivyo ubora wa sanaa nzima unapanda.  Kitendo cha bendi ya TANCUT kuruhusu kukosolewa kabla ya kuingia katika mashindano ilikuwa sababu moja wapo ya bendi kupata ushindi mnono katika mashindano yale. Wasanii wa sasa hapa nchini wako tayari kukosolewa?

Friday, August 5, 2022

TUZIKUMBUKE BENDI ZETU ARUSHA NA MOSHI

 

The Ambassador Band ya AICC

Safari ya kuzikumbuka bendi zetu leo inatufikisha miji ya kaskazini mwa nchi yetu. Jiji la Moshi na jiji la Arusha. 
Tuanze na jiji la Moshi, hakika  ukisikiliza hadithi mtaani za siku hizi unaweza ukadhani Moshi si mji wa kuwepo katika historia ya muziki, lakini kinyume kabisa, huwezi kuongelea historia ya muziki Tanzania bila kutaja Moshi. Kwanza kuna mchango mkubwa wa wanamuziki waliotoka Moshi, na pili kati ya wawekezaji wakubwa katika muziki waliowahi kutokea Tanzania, waliotoka Moshi.
Taja bendi karibu zote zilizokuwa kubwa miaka ya sitini na sabini utaukuta mkono wa muwekezaji toka Moshi.
Wanamuziki wa Moshi walianza kuiweka Tanzania katika ramani ya muziki wa Afrika ya Mashariki kuanzia miaka ya 50. Mabingwa kama Frank Humplick na Dada zake, ambao walikuwa watoto wa  baba muhandisi kutoka Austria na mama Mchaga,  Dr Hosea Macha na mke wake, Dr Hosea alikuwa baba mzazi wa mwandishi na msanii maarufu Freddy Macha,  Kimambo Brothers na wengine wengi waliweza kurekodi nyimbo zao kwa mtindo ule wa kutumia gitaa kavu, yaani gitaa lisilotumia umeme. Frank Humplick alirekodi nyimbo nyingi na wasanii wa Kenya chini ya lebo ya Jambo, ukiwemo wimbo maarufu Mi Francois mi naimba,ambao alifanya ‘kolabo’ na mwanamuziki kutoka Kongo Edward Mazengo, mambo yote hayo kabla ya Uhuru.
Baadhi ya bendi nyingine  zilizokuweko Moshi ni Ringo Jazz, halafu kulikuweko na Black Beatles, hawa walikuwa wakivaa kama wale wanamuziki wa Beatles wa Uingereza, walikuwa na gari lao la Combi ambalo waliliandika maandishi makubwa Black Beatles.  Moshi pia ilikuweko bendi maarufu ya Zaire Success, hii ilikuwa bendi ya vijana wa Kikongo. Kulikuwa na hadithi zamani ikisema hawa walikuwa ni kundi lililovunjika kutoka kutoka kwa kundi la Orchestra Fauvette la akina King Kiki na Ndala Kasheba Supreme, hata lile kundi la bendi ya Wakongo la Mwanza lilioitwa Orchestra Super Veya nayo husemekana ilitokana na mpasuko wa Orchestre Fauvette.
Mara ya mwisho kuingia muziki wa Zaire Success ilikuwa mwaka 1974 walipopiga community center Same, siku ilipofunguliwa Benki ya kwanza mji huo. Mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Bwana Peter Kisumo. Mimi na rafiki zangu tulizuiliwa kuingia kwa kuwa kulikuwa na mgambo mlangoni kazi yake ilikuwa kuangalia waliovaa nguo zisizofaa,  tulikuwa tumevaa suruali zetu zilizokuwa pana chini, maarufu kwa jina la bugaluu. Ikalazimu kwenda kubadili ili kuweza kuingia dansi lile.  Nigusie hapa kuwa kuwa Same pia kulikuwa na bendi iliyoitwa TANU Youth League Jazz Band, kuna Askofu maarufu alikuwa mwanamuziki wa bendi hiyo miaka hiyo ya 70.

Chuo cha Polisi cha Moshi maarufu kwama Police Training School, PTS, kwa miaka mingi ilikuwa na bendi moja nzuri iliyokuwa ikitumbuiza mjini Moshi mara kwa mara. Moshi pia kulikuwa na bendi iliyokuwa inaitwa Bana Afrika Kituli, awali ilikuwa bendi kubwa ikaapoteza umaarufu mpaka ikawa inapiga kwenye vilabu vya mbege. Mmoja wa wanamuziki wa bendi hii niliwahi kumkuta Tanga akiwa amebadili taaluma na kuwa mganga wa kienyeji. Ni jambo la ajabu kidogo lakini kuna wanamuziki wengi sana ambao walikuja kuacha muziki na mkuwa waganga wa kienyeji.
Shule ya sekondari ya Old Moshi na hata Shule ya Ufundi ya Moshi ( Moshi Tech), zote zilikuwa na bendi ambazo zilikuwa zikipiga muziki kwa umahiri wa hali ya juu. Bendi ya shule ya Old Moshi walijiita Orchestra Mosesco. Baadhi ya wanamuziki wa bendi hii walikuwa Joseph Mkwawa, Pelegrin, Mwakibete, Tamba, Kufakunoga  na kadhalika.
Tuhamie Arusha, mji ambao katika miaka ya mwanzo ya sabini ulikuwa umechangamka sana kutokana na kuwa na wafanyakazi wengi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, halafu ukijumlisha na  biashara ya utalii, hakika mji ulikuwa na burudani nyingi. Hoteli za kitalii zilizokuwa chini ya Shirika la utalii Tanzania, karibu zote zilikuwa zikishindana kuwa na bendi bora hotelini, bendi kama The Revolutions, ambayo baade iliitwa Kilimanjaro Band, The Bar Keys ambayo ikaja kuitwa Tanzanites ni baadhi ya bendi ambazo zilitamba sana kwenye mahoteli ya Arusha. Bendi chache nyingine zilizokuwa zikipiga mahotelini ni Juju Masai ya akina Sabuni, hawa walikuwa ndugu waliokuwa mahiri sana katika muziki,  Crimson Rage, Ambassadors akina Andy Swebe na Likisi matola (wanaoonekana pichani), Tonics ya David Marama  na kadhalika.

Kwenye uwanja wa muziki wa Rumba kulikuwa na bendi kama Orchestra National, bendi ambayo ndio aliyoanzia muimbaji mahiri sana Hassan Bitchuka kabla ya kuonekana na NUTA Jazz Band. Kulikuwana Arusha Jazz Band, bendi iliyokuwa ya akina Wilson Peter na wenzie baada ya kuihama Jamhuri Jazz Band ya Tanga. Arusha Jazz Band ilihamia Mombasa na ndipo ikabadili jina na kujiita Simba wa Nyika, umaarufu wa bendi hiyo unafahamika kwa wapenzi wote wa muziki wa zamani. Arusha pia kulikuwa na bendi ya Chuo Cha Jeshi Monduli, bendi iliyoitwa Les Mwenge, bendi iliyokuja kupata umaarufu mkubwa kutokana na album ya wimbo Kila munu ave na kwao wa Halila Tongolanga.

Ukurugenzi wa Mkoa wa Arusha  ulianzisha bendi, nadhani ulikuwa ukurugenzi wa kwanza kufanya hivyo baadae mikoa mingine ikafuatisha. Bendi hiyo  iliundwa na  wanamuziki wa bendi ya Orchestra Lombelombe, bendi iliyokuwa ni matokeo ya mpasuko wa Morogoro Jazz band. Bendi hiyo mpya ikaitwa Kurugenzi Arusha. Kurugenzi Arusha ilitunga nyimbo kadhaa zilizotikisa anga ya muziki nchini, nyimbo  kama vile Wivu na Ujamaa mpaka leo bado zina wapenzi lukuki. Mwisho huwezi kuongelea bendi za Arusha bila kuitaja  Serengeti Band, bendi iliyoanzishwa na mmoja ya wanamuziki wa Orchestra Mkwawa iliyokuwa bendi ya shule ya Mkwawa, mwandishi mkongwe Danford Mpumilwa, hakika bendi hii nayo ilichangamsha jiji la Arusha.

Thursday, July 28, 2022

TUZIKUMBUKE BENDI ZETU 6 -MBEYA

 


Hebu tuendelee na safari ya kukumbuka bendi mbalimbali nchini, leo tuanzie mkoa wa Mbeya, tuanze na wilaya ya Mbeya, wilaya ambayo kabla ya mwaka 1927 ilikuwa ikijulikana kama wilaya ya Igali.
Mbeya ilikuja kuanza kupata umaarufu kutokana na kugundulika kwa dhahabu sehemu mbalimbali za kuzungukia mji huu kuanzia mwaka1906, hali iliyoendelea kwa karibu miaka ishirini baada ya hapo. Mji ukapata wageni kutoka kila kona ya Afrika Mashariki na Kati mpaka visiwa vya Ngazija, watu wakaja Mbeya na miji jirani kutafuta utajiri.

Popote penye vijana wengi, tena wakiwa wanatafuta pesa, hakukosekani burudani na hasa burudani ya muziki. Bahati mbaya si mengi yaliyohusu burudani za wakati huo yaliyowekwa kwenye kumbukumbu,lakini kati ya machache tuanze na historia ya mtu moja aliyekuwa maarufu sana aliyeitwa John Benedict Mugogo Mwakangale, mwenyewe alipendelea kuitwa JBM. John Mwakangale, JBM alikuwa mwanasiasa mashuhuri katika harakati za kupigania Uhuru na baadae katika siasa ya kutafuta umoja wa Afrika. Alifanya kazi kubwa ya kutambuliwa na hatimae alikuweko katika Baraza la Mawaziri la kwanza la Tanganyika huru chini ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, na akateuliwa kuwa Waziri wa kwanza wa Kazi, pia alikuwa Mbunge wa Nyanda za juu kusini kwa kipindi kirefu, kabla ya Uhuru na hata baada ya Uhuru. Pamoja na yote hayo JBM pia alikuwa mpenzi mkubwa wa muziki. Kati ya mwaka 1959 na mwaka 1960 alikwenda Zambia, wakati huo ikiitwa Northern Rhodesia, alikwenda kununua vyombo vya muziki kwa ajili ya bendi yake iliyoitwa Free Mwakangale Jazz. Alipokuwa huko akakutana na vijana kutoka jimbo la Luanshya waliokuwa  na kundi lao      wakipiga vizuri sana muziki, akaongea nao na hatimae wakakubaliana kuondoka kwao na kuingia Tanganyika kujiunga na Free Mwakangale Jazz, mmoja wa vijana hao alikuwa Michael Enoch. Michael Enoch baadae alikuja kuchukuliwa na Dar es Salaam Jazz Band na kuiendeleza kwa miaka mingi akiwa mpiga solo, kisha akahamia Dar es Salaam International akiwa mpiga saksafon  na hatimae Mlimani Park Orchestra alikoendeleza umahiri wake katika saksafon, na kupewa majina mengi ya sifa, King Enoch, na Teacher, Michael alikutwa na mauti  alipokuwa DDC Mlimani Park Orchestra.
Bendi ya Free Mwakangale Jazz makao yake makuu yalikuwa mji uliopewa jina la Neu Langenburg na Wajerumani lakini wote tunaufahamu siku hizi kama Tukuyu, , pamoja na Michael Enoch bendi hiyo ilikuwa na wanamuziki wengine wanaokumbukwa ni Ben Jack na Saiz Vera.
Kuna hadithi ya kuchekesha na kusikitisha kuhusu kisa kilichofanya Free Mwakangale Jazz ife na Michael Enoch atue Dar es Salaam Jazz Band.
Siku moja  bendi ya Free Mwakangale Jazz ilipata safari ya kwenda Mwanza na baada ya kufika huko ilifanya maonyesho kadhaa, siku moja vijana hawa walikodi gari ili kubeba vyombo vyao, pengine wakati huo kwa ugeni na pengine hata Kiswahili walikuwa hawajakifahamu sawasawa, dreva wa gari akawaomba wamsubiri akaweke mafuta, wakamruhusu, alipoondoka hakuonekana tena ukawa ndio mwisho wa Free Mwakangale Jazz. Wanamuziki wakajikuta wamekwama Mwanza, bahati nzuri baada ya muda mfupi walipata kazi ya kupiga muziki katika bendi moja pale Mwanza, wakiwa katika bendi hiyo, muwakilishi wa Dar es Salaam Jazz Band , marehemu Limi Ally,ambaye alikuwa katika harakati za kumtafuta mpiga gitaa la solo akamuona Michael Enoch, na ndipo wakakubaliana kurudi nae Dar es Salaam kujiunga na Dar es Salaam Jazz Band.

Bendi nyingine ya Mbeya ilikuwa TANU Youth League Jazz Band, bendi iliyokuwa maarufu miaka ya sitini na ilirekodi nyimbo kadhaa RTD, kati ya nyimbo zake zilizokuwa maarufu ni ule ulioitwa Nampenda Firida mwenye macho mazuri. Kulikuwa na bendi nyingine ambayo ilisemekana ilitokana na kufa kwa TANU Youth League Jazz Band ilikuwa ikiitwa  bendi ya Lemi au Remi.

Bendi nyingine iliyokuweko Mbeya ni hiyo iliyoko kwenye picha ambayo iliitwa Azimio Co Bantou Jazz Band. Ukiangalia vizuri picha hiyo, utaona ilipigwa katika kota zilizokuwa za wafanyakazi wa  serikali zilizokaribu na mitaa ya Ghana, pengine hapo ndipo yalikuwa masikani ya bendi hii.

Katika tasnia ya muziki wa bendi kuna utamaduni wa kuigana majina, kwa mfano baada ya kuundwa bendi ya Dar es Salaam International Orchestra, bendi nyingi ziliibuka na kujiita international, zikiwemo Dodoma International Orchestra, Tanga International Orchestra, Ruaha International Orchestra na kadhalika. Kule Sumbawanga ikaundwa bendi iliyoitwa Rukwa International Orchestra, bendi hii ilijitokea sana na kushiriki matukio ya kitaifa. Rukwa International Orchestra ilikuwa mojawapo ya bendi zilizojitokeza kushiriki Mashindano ya Bendi Bora (MASHIBOTA) yaliyofanyika katika ukumbi wa Diamond Jubilee Dar es Salaam miaka ya 90.

Thursday, July 21, 2022

KAMIKI WIMBO WA MIAKA YA SABINI UNAOKUMBUKWA NA WAZEE MPAKA LEO

Kamiki yeye motema aaa, Kamiki yeye motema oooo. Wapenzi wa muziki wa kavasha wa miaka ya 70 na 80, hawakosi kuanza kutabasamu, mistari hiyo niliyoanzia habari hii ilikuwa ni maneno ya mwanzo ya wimbo maarufu enzi hizo, wimbo ulioitwa Kamiki. Wimbo huu ulipigwa na bendi  iliyoitwa Orchestra Kiam kutoka Kongo. Bendi hii ilikuwa na nyimbo nyingi sana zilizopendwa sana karibu Afrika nzima. Wakati huo ulikuwa ndio wakati ambapo vijana waliojiona wa kisasa Afrika nzima walikuwa wakivaa suruali pana zilizoitwa Bugaluu na viatu vyenye soli ndefu ambavyo vilifahamika kama platform. Shati zilikuwa ni zenye kubana sana na siliitwa ‘slimfit’, huku kichwani kila kijana mjanja alikuwa nafuga nywele ndefu zilizokuwa zikichanwa kwa mtindo wa Afro. Vijana wa kiume walikuwa wakitumia sana chanuo za chuma ambazo zilipashwa moto kisha kunyoosha nywele ili ziwe ndefu. Lakini turudi kwa Orchestra Kiam, historia ya kundi hili ilianza baada ya Papa Noel, mwanamuziki mkongwe wa Kongo aliyepigia bendi nyingi maarufu za Kongo ikiwemo TP OK Jazz, kuwa na taratibu za kusaidia vijana waliotaka kujiendeleza kimuziki waliokuwa wakiishi jirani na kwake, hivyo basi  alitengeneza bendi iliyoitwa Orchestra Bamboula, bendi hii haikuwa na vyombo, vijana walifanya mazoezi kwa magitaa makavu nyumbani kwa mkongwe huyu na walipo bahatika kupata sehemu za kufanya  onyesho, Papa Noel alikuwa akikodi vyombo na bendi kuweza kupiga, lakini kwa mtindo huu mara nyingi hawakupata malipo mazuri, lakini nia yao ilikuwa kupiga muziki na si kusaka fedha.
Siku moja Papa Noel alisafiri na TP OK Jazz kwenda kufanya onyesho nchini Algeria aliporudi alikuta vijana wake wamesambaratika, basi akatafuta vijana wengine na kuunda kundi jipya lililofanya mazoezi miezi sita. Baada ya muda huo Papa Noel alienda kwenye studio ya mkongwe mwingine wa muziki  wa Kongo ,Verckys, na kulipia gharama za kurekodi, kundi la Bamboula  likaingia studio na kurekodi na chini ya fundi mitambo wa studio hiyo Kidiata M’Pole, bendi hiyo ikarekodi  nyimbo nne katika muda wa masaa machache, kama ilivyokuwa taratibu miaka hiyo.
Ilikuwa ni kawaida ya Verckys kusikiliza nyimbo  zilizorekodiwa katika studio yake, na aliposikia nyimbo hizo mpya akamtuma meneja wake kuwatafuta vijana waliopiga muziki  huo. Meneja wake aliyekuwa anamfahamu Frank Muzola Ngunga, akaanza msako. Muzola alipopatikana alisema wana nyimbo nyingine pia ambazo hawajazirekodi, wakaalikwa kuzirekodi zote, Muzola akasita kurekodi nyimbo hizo kwani alihisiki atakuwa anamsaliti Papa Noel, wenzie wakamshinikiza hatimae akakubali. Wakati huo Papa Noel alikuwa akitafuta fedha za kukamilisha malipo ya kuweza kutengeneza santuri ya nyimbo nne zilizorekodiwa na pia kumlipa fundi mitambo aliyezirekodi. Kesho yake Papa Noel alikwenda studio kukamilisha malipo alishangaa kukuta kundi lake likiwa studio linarekodi likiwa linasikilizwa na Verckys, ugomvi mkubwa ukaanza hapohapo, lakini hatimae Verckys alimzidi kete Papa Noel kwa kumtaka aonyeshe mkataba wake na wana muziki hao. Papa Noel aliondoka kwa hasira hakuna anaejua alizipeleka wapi nyimbo zile nne zilizorekodiwa kwani hata yeye alipoulizwa miaka mingi baadae alisema hakumbuki.
Verckys aliamua kuliita kundi lake jipya,  Orchestra Kiam, Kiam ikiwa kifupi cha Kiamwangana jina halisi la Verckys. Wanamuziki waanzilishi wa kundi hili walikuwa Frank Muzola Ngunga, Bakolo Keta, Jeannot Botuli Ilonge na Mboyo Bola Eddie waimbaji, wapiga gitaa la solo walikuwa  Guyno na Souza Vangu (Souza alijiunga miezi michache baadae), wapiga gitaa la  rhythm walikuwa  Lélé Nsundi na Djo Morena, kwenye gitaa la bezi alikuweko Vieux Kody na mpiga drums  Suké Ngonge. Wanamuziki hawa wakaingia mkataba na Verkcys akampa kila mmoja wao fungu la bonas ya kujiunga na bendi na kisha wakawa wanalipwa mshahara, shilingi alfu thelathini katikati ya mwezi na shilingi alfu sabini mwisho wa mwezi, na wengine pia wakanunuliwa samani kwa ajili ya vyumba vyao, hakika walijiona wamepata mfadhili wa kweli ukikumbuka kuwa kwa Papa Noel, walikuwa wakiishi kwa kubahatisha. Walikabidhiwa vyombo vipya wakawa wanafanya mazoezi siku tatu kwa wiki na siku za wikiendi wakawa wanapiga katika kumbi mbalimbali ambazo zilikuwa zimeingia mkataba na Verckys. Verckys aliendeleza utaratibu huu wa kuwa na bendi alizozilipa mshahara mdogo na kupata mapato makubwa kutokana na kuzikodisha kwenye kumbi na pia kuuza santuri za bendi zilizokuwa chini yake.
Mwaka 1974 Orchestra Kiam waliingia studio na kurekodi wimbo wa Nina, wimbo wao wa kwanza kupendwa sana, ulikuwa utunzi wa  Bakolo Keta, utunzi mwingine wa Bokolo ulioitwa  Baya-Baya ulisaidia sana umaarufu wa bendi hii. Umaarufu wa Kiam ukaanza kuwapa uchu matajiri wengine kuimiliki bendi hii. Mfanya biashara mmoja Mbuta Suka alianzisha label yake aliyoiita Mabele Productions, na  mwanzoni mwa mwaka 1975 aliwashawishi wanamuziki kadhaa wa Kiam kuja kurekodi kwa kutumia label yake  kwa kutumia utaratibu  ulioitwa zong zing, yaani kurekodi nje ya bendi. Kundi kubwa la Kiam lilishiriki kazi hii na kurekodi nyimbo nne. Mbuta Nsuka alianza kusambaza santuri za nyimbo hizo na kuzitambulisha kuwa zimepigwa na Orchestra Baya-Baya, Verckys alipozisikia nyimbo hizo alijua ni bendi yake akawasimamisha kazi wanamuziki wote walioshiriki. Mbuta Nsuka akatumia fursa hiyo kuwashawishi wanamuziki hao waachane na Verckys, na ndipo rasmi ikaundwa bendi ya Orchestra Baya- Baya.

Huku Orchestra Kiam kikawa kilio maana waliobaki walikuwa ni muimbaji Frank Muzola Ngunga, mpiga bezi  Vieux Kody na mpiga rhythm Djo Morena. Muzola Ngunga akapewa kazi ya kutafuta wanamuziki wengine kufufua bendi.  Baada ya kama mwezi kundi likafufuka na waimbaji Germain Kanza, Adoly Bamweniko na Otis Mbuta, kwenye magitaa akapatikana mpiga solo Adamo Lewis na  Djuké, kwenye gitaa la rhythm akaweko Antoine Denewadé. Baada ya mazoezi ya miezi michache Kiam wakarudi tena studio. Hapo ndipo vikatoka vibao maarufu kama Memi, Yanga Yanga na Kobondela .

Wakati huo Orchestra Baya-Baya walianza safari ya kuzunguka kupiga muziki miji mbalimbali, muda si mrefu bendi ikakwama  katika mji wa Bandaka kutokana  na kukosekana mapato.  Ukawa mwisho wa Orchestra Baya- Baya, Lélé Nsundi ,Bakolo Keta na Suké Ngonge wakarudi Orchestre Kiam. Huyu Lélé Nsundi alikuwa mpangaji mzuri sana wa muziki hivyo ilianza kazi  nzuri sana ya  nyimbo mpya ikianzia na wimbo maarufu wa Kamiki , wimbo huu ulitungwa na Muzola Ngunga kumsifia mwanamke aliye kuwa akiishi nae wakati huo. Wimbo huo ulipendwa Afrika nzima wakati huo na hata leo. Mpaka mwaka 1977 Kiam waliendelea kutoa vibao motomoto kama Ifantu, Bomoto, Ya Yona, Mbale, Bakule, Masumu na kadhalika. Mwezi Agosti mwaka 1978, Kiam walirekodi wimbo ulioitwa Exode  wakiwa na muimbaji mualikwa kutoka Gabon alieitwa Mack Joss. Mark akawazindua kuhusu hakimiliki na jinsi Verkcys alivyokuwa akiwadhulumu haki zao hizo, kwa kuwapa mshara tu bila kuwapa mirabaha iliyotokana na mauzo ya santuri walizotunga na kushiriki. Elimu hii ikawafanya  Bakolo Keta , Lélé Nsundi na Adoly Bamweniko, kuondoka Kiam mara moja. Lilikuwa pigo kubwa kwa Kiam kwani baada ya hapo hawakuweza kutoa tena nyimbo za kutikisa wapenzi wao.

Verckys alijitahidi sana kulitambulisha kundi la Kiam Afrika ya Mashariki na Afrika ya Magharibi, jambo ambalo lilifanya kundi hili kukumbukwa zaidi katika maeneo haya kuliko Kinshasa kwenyewe mpaka leo. Lakini hatimae mwaka 1983, Muzola Ngunga na Verckys waliamua kulivunja rasmi kundi la Orchestra Kiam.

 

Wednesday, July 20, 2022

TUZIKUMBUKE BENDI ZETU 5

Katika safari yetu ya kuzikumbuka bendi mbalimbali nchini, kuna kitu kinaonekana wazi kabisa, katika swala la muziki kwa ujumla tumerudi nyuma sana. Kulikuwa na bendi binafsi, bendi za serikali , bendi za chama tawala na karibu kila mji ulikuwa na zaidi ya bendi moja. Watu walikuwa wachache sana kuliko siku hizi lakini walikuwa na na nafasi za uchaguzi wa burudani kuliko siku hizi. Sababu ni nyingi lakini si nia ya makala hizi kuongelea hayo japo baada ya mzunguko wa nchi nzima pengine italazimika kujiuliza tumefikaje huku tuliko? Kabla ya kuendelea na safari kuna kitu kiko wazi kinajitokeza, wakati wa awamu tatu za mwanzo za uongozi wa nchi hii, wasanii wa kila mahala walithaminika, ndio maana unakuta kila mkoa kulikuweko na makundi ya muziki ambayo hatimae yaliweza kujitokeza na kufahamika nchi nzima. Siku hizi ni kawaida kabisa viongozi wa juu kuoneka wakisindikizwa na wasanii ‘wakubwa ‘ wa kutoka Dar es Salaam, utadhani huko wanakokwenda hakuna wasanii, au wanaenda nchi nyingine kutangaza sanaa ya nchi yao.
Safari yetu leo inatupeleka mikoa ya kusini, mikoa hii haikuwa nyuma kabisa katika mambo ya dansi, kulikuweko na bendi toka enzi ya mkoloni. Kati ya bendi ambazo nina kumbukumbu nazo, nianze na White Jazz Band iliyokuwa na masikani yake mjini Lindi,  bendi hii kama zilivyokuwa bendi nyingine ilipitisha wanamuziki wengi lakini kati ya wanamuziki waliokuja kung’aa nchini waliopitia bendi hii ni marehemu Mzee Kasim Mapili, yeye alinza kupiga muziki katika bendi hii mwaka 1958, kuna kila sababu kuamini kuwa ilikuweko kabla ya mwaka huo. Mwaka 1963 tayari kulikuwa na bendi iliyokuwa inaitwa Jamhuri Jazz Band mjini Lindi, bendi hii ilikuwa mali ya TANU Youth League, au Jumuiya ya Vijana wa TANU. Jamhuri Jazz Band hii ya  ilikuweko kabla ya Jamhuri Jazz Band ile ya Tanga, japo tutakapofika mkoa wa Tanga tutapata historia ndefu zaidi ya bendi hiyo.

Wakati tukiwa bado Lindi, haiwezekani kutoitaja Mitonga Jazz Band. Bendi hii ilifanya makubwa kwa kutoa mfululizo wa vibao pendwa, kikiwemo Mariana na Sitaoa tena Mchinga, ambavyo vikipigwa mpaka leo bado wanaovisikia hata kwa mara ya kwanza huvipenda. Album ya wimbo Mariana ilirekodiwa na mafundi mitambo wa Radio Tanzania Dar es Salaam kwenye ukumbi wa Polisi pale Lindi, lakini ubora wake unazishinda nyimbo nyingi zilizorekodiwa kwenye studio za kisasa, jambo linaloonyesha umahiri wa wanamuziki wa bendi hiyo, na umahiri wa mafundi mitambo.
Tukitoka Lindi tuingie mji wa Masasi, mji huu nao ulikuwa na bendi nyingi na ni mji ambao umewahi kutoa wanamuziki wengi ambao walikuja kuwa maarufu Afrika ya Mashariki nzima. Tuanze na Masasi Jazz Band, bendi hii ilitoa wanamuziki  maarufu kama  Gerald Nangati, wapiga gitaa la rhythm wawili mahiri, Ally Makunguru aliyekuja kupigia bendi za JKT Kimbunga Stereo, Mlimani Park, International Orchestra Safari Sound na hatimae kuhamia Kenya ambako pia alipiga muziki katika bendi kubwa maarufu za huko. Masasi Jazz Band ndiko alikotoka  Charles Kasembe ambaye alikuja kupiga na Mbaraka Mwinshehe, akapitia Dodoma International Orchestra na hatimae akahamia Kenya alikokuwa na bendi yake ya Les Volcano.

Bendi nyingine iliyokuweko Masasi ilikuwa Umoja Jazz Band, pia kulikuweko na TANU Youth League Jazz Band katika mji huo, jambo lililokuwa kawaida katika miji mingi, ni wazi kulikuwa na sera za makusudi za TANU kuhakikisha kila wilaya kuna kuwa na bendi ya vijana wa TANU. Bendi hii ya TANU Youth League Jazz Band ndio ilikuwa bendi ya kwanza ya mwanamuziki mwingine aliyekuja kuwa mpiga solo mahiri sana katika bendi za JKT Kimbunga Stereo na DDC Mlimani Park Orchestra Mzee Henry Mkanyia.
Kwa mara ya kwanza nilipokutana na Ally Makunguru mwaka 1975, alinambia kuwa alipokuwa Masasi pia alikuwa akipigia bendi iliyokuwa ikiitwa Kochoko Jazz band, hiyo ni bendi nyingine ya mji huyo. Masasi ulikuwa mji mdogo sana wakati huo lakini ulikuwa na bendi nyingi kiasi hiki, na hizi nilizotaja hapa, ni zile zilizoko katika kumbukumbu zangu tu.

Nachingwea nako hakukuwa kimya kulikuwa na bendi iliyoitwa Mondomondo Jazz band, bendi iliyokuwa ikileta burudani kwa wakazi wa mji huo.
Mtwara ulikuwa mji mwingine wa maraha kule kusini mwa Tanzania, toka miaka hiyo mpaka leo Mtwara imeendelea kutoa wanamuziki mahiri ambao wamekuwa waking’aa kitaifa na kimataifa. Kati ya bendi zilizowahi kuweko Mtwara tuanze na bendi iliyochukua jina la mji huo Mtwara Jazz Band, pia mapema baada ya Uhuru ilikuweko bendi iliyoitwa Honolulu Jazz Band. Mamlaka ya Bandari katika miaka ya zamani ilikuwa inajihusisha sana katika michezo na utamaduni, na hapo Mtwara ikaanzisha bendi ilioyoitwa Bandari Mtwara Jazz Band. Lakini pia ziliwahi kuweko bendi nyingine zaidi katika mji huu, kulikuwa na Mambo Jazz Band na bendi nyingine iliyoitwa Bantu Jazz Band… Kwa leo nimalizie kwa kuitaja bendi iliyokuweko mji ambao hautajwi sana linapokuja swala la bendi nao ni Kilwa Masoko. Mji huu nao ulikuwa na bendi yake iliyoitwa Lucky Star Jazz Band


Friday, July 15, 2022

TUZIKUMBUKE BENDI ZETU 4

Kama Franco Luambo Luanzo angekuwa hai mwaka huu angekuwa anatimiza miaka 84 kwani alizaliwa tarehe 6 Julai 1938, lakini kwa mapenzi ya Mungu alifariki tarehe 12 Oktoba 1989 akiwa na umri wa miaka 51 tu. Wakati Franco akiwa na umri wa miaka 6 tu Morogoro Jazz Band ilianzishwa katika mji wa Morogoro. Kuna somo kubwa hapa, kwa bahati mbaya kutokana na Tanzania kutokuandika historia yake ya muziki, watu wengi na hata wanamuziki wengi wa kizazi hiki hudhani kuwa nchi yetu iliiga toka Kongo maswala ya muziki wa bendi, lakini historia inaonyesha kuwa mambo hayakuwa hivyo hata kidogo kama tarehe hizo hapo juu zinavyoashiria wazi, pengine wanamuziki wetu wa zama hizo hawakujua hata kama Kongo kuna wanamuziki.

Leo safari yetu ya kuzikumbuka bendi zetu, imetuleta mkoa wa Morogoro, na kama unavyoona wakazi wa Morogoro tayari waliakuwa wakifurahia muziki wa bendi kabla hata ya vita ya piti kumalizika.
Morogoro Jazz band inajulikana na wengi mpaka leo hasa katika kipindi alichokuwepo Mbaraka Mwinyshehe Mwaluka. Wimbo maarufu wa Jogoo la shamba ni moja kati ya nyimbo za bendi hiyo ambazo hata watoto wadogo wa kizazi hiki wanaufahamu, na kuutumia katika kutaniana tena kwa utani unaofanana sana na nia ya kutungwa kwa wimbo huo.

Mwaka 1948 nguli mwingine wa Morogoro, Salum Yazidu Abdallah (SAY), mwanamuziki aliyezaliwa kutoka kwa baba Mwarabu na mama Mlugulu, alianzisha bendi yake aliyoiita La Paloma, neno la Kispayola likiwa na maana Njiwa. Wanamuziki na wapenzi wa rumba miaka hiyo, kwa ujumla walikuwa wakisikiliza santuri z Kispanyola kutoka Cuba. Santuri hizo zilizokuwa na namba zilizoanzia GV 1 na kuendelea hadi zaidi kidogo ya GV 200 zilikuwa na muziki kutoka bendi mbalimbali za Cuba, wanamuziki wa huku wakawa wanapiga muziki kuiga huo wa Cuba na hata kuunda bendi zao nazo kuzipa majina ya bendi zile za kule Cuba, ndio maana tukaziona bendi za Sextet Jazz ya Dodoma na Habanero Jazz Band ya Iringa. 
Salum Abdallah aliwahi kutoroka toka kwao Morogoro  na kwenda Mombasa ili azamie meli na kwenda Cuba kujifunza muziki, bahati mbaya kipindi hicho vita ya dunia ya pili ilikuwa imepamba moto na hivyo safari yake ikaishia Mombasa, alipata taabu sana Mombasa hatimae Umoja wa Waarabu wa Mombasa walimtaarifu baba yake aliyekuja kumrudisha mwanawe Morogoro.
Aliporudi Morogoro ndipo akaanzisha bendi yenye jina la ‘La Paloma’ jina lilitokana na wimbo maarufu wa Cuba ambao mpaka leo bado unapigwa na bendi zetu nyingi kama muziki wa ala mapema kabla ya kuanza rasmi kwa dansi.
La Paloma Band ilibadili jina na kujiita Cuban Marimba Band mwaka 1952, chini ya Salum Abdallah bendi ilirekodi nyimbo nyingi ambazo mpaka leo bado zinapendwa hata na vijana wa leo. Nyimbo kama Wangu Ngaiye, Shemeji Shemeji wazima taa, Wanawake na kadhalika  si ngeni masikioni mwa wapenzi wa muziki hata leo. Cuban Marimba ilikuwa maarufu kiasi cha kampuni za kurekodi kutoka Mombasa zilikuwa zikiifuata bendi  Morogoro ili kuirekodi. Wimbo maarufu wa Wanawake Tanzania ulirekodiwa Korogwe, baada ya kampuni ya kurekodi ya Assanand kuifuata bendi Morogoro na kukuta imesafiri. Baada ya kuitafuta hatimae wakakutana Korogwe. Wakati Assand akiwa njiani gari lake lilikwama kwenye matope, na aliomba msaada wa kusukumwa, wanawake wakajitokeza na kulisukuma gari lile. Asanand  alipomuhadithia mkasa ule Salumu Abdallah ndipo ulipotungwa wimbo maarufu wa Wanawake Tanzania.
Kwa mapenzi ya Mungu Salum Abdallah alifariki katika ajali ya ajabu mwaka 1965. Cuban Marimba ikawa chini ya Juma Kilaza. Kilaza aliendelea na bendi hiyo miaka kadhaa alipoiacha akaanzisha bendi yake iliyoitwa TK Lumpopo, ambayo mata nyingine alikuwa akiita TK Lumpopo National. Mbaraka Mwinyshehe nae alikuja kuicha Morogoro Jazz Band na kuanzisha bendi yake ya Super Volcano.
Kwa kipindi kifupi kwenye mwaka 1985 ilitokea bendi iliyoitwa Les Cuban. Vyombo vya bendi hii vilikuwa mali ya Chama Cha Mapinduzi  mkoa wa Morogoro, na alikabidhiwa Mzee Juma Kilaza ili kuona uwezekano wa kurudisha hadhi ya muziki Morogoro. Mzee Kilaza aliwaleta wanamuziki wa bendi ya Orchestra Vina Vina toka Nairobi, vijana aliyorekodi nao huko na kuwaona wako vizuri sana. Kati ya waliokuja na Orchestra Vina Vina alikuweko muimbaji mlemavu wa macho Nico Zengekala. Les Cuban  ikawa sasa inajitambulisha kwa mtindo wa Vina vina, ili kutokupoteza jina lao la awali, walifanya kazi kubwa ya kukumbukwa, nyimbo kama Kifuko cha Zambarau au Jackie ni wimbo bado maarufu mpaka leo. Lakini bendi iliingia katika matatizo ya kiutawala na kufa mapema sana.

Cuban Marimba chini ya Juma Kilaza wa kwanza kulia




Tukirudi nyuma katika miaka ya sitini na sabini, bendi hizi mbili, Morogoro Jazz Band na Cuban Marimba Band ziliuchangamsha sana mji wa Morogoro kiasi cha kwamba siku za mwisho wa wiki, wapenzi wa muziki walikuwa wakisafiri kutoka Dar es Salaam na kwenda Morogoro kustarehe. Wakati huo usafiri ulikuwa mgumu kwani sehemu kubwa ya barabara kati ya miji hii miwili ilikuwa ni ya vumbi.
Watu wa mkoa wa Morogoro hupenda sana muziki, kulikuwa na bendi. Inawezekana kabisa kuwa katika miaka ya 70 na 80 mkoa wa Morogoro ndio ulikuwa na bendi nyingi zaidi. Hasa ukizingatia kuwa karibu kila wilaya ilikuwa na bendi na tena zilizokuwa zikifahamika Kitaifa.
Kati ya bendi za Mkoa wa Morogoro zilizokuwa Mahenge ni Mahenge Jazz Band na Taifa Jazz Band, hii bendi ya pili ilianzishwa na  Joakim Ufuta ‘Dokta’, huyu alikuja kuwa mpiga gitaa  la solo maarufu sana katika bendi ya Cuban Marimba na TK Lumpopo. Mahenge pia kulikuwa na bendi ya wanafunzi wa shule ya sekondari ya Kwiro, Kwiro Jazz Band. Bendi hii ilirekodi mara kadhaa RTD, na wanamuziki wa bendi hiyo si mara moja walilalamika kuwa Morogoro Jazz Band iliwaibia mtindo wao wa Mahoka. Mpiga solo wa bendi ya shule ya sekondari ya Mkwawa, Orchestra Mkwawa, Simon Sewando alikuwa fundi mitambo wa bendi ya Kwiro kabla hajahamia shule ya Mkwawa. Alijulikana kwa jina ya ‘The mad scientist’ kutokana na kufumua fumua na kutengeneza amplifaya za bendi hiyo. Sewando amestaafu akiwa mwalimu wa electronics Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Kulikuwa na Kilosa Jazz band ambako alitokea Abel Balthazar na mkasa wake wa kuhamia Dodoma Jazz band niliuandikia katika makala kuhusu bendi za mkoa wa Dodoma. Kulikuweko na Ifakara Jazz Band pia  Sukari Jazz band bendi iliyokuwa mali ya kiwanda cha Sukari cha Kilombelo, kulikuweko na  Ulanga Jazz band toka Ulanga na bila kusahau Njohole Jazz Band. Njohole Jazz Band walikuwa na nyimbo zao nyingi maarufu Afrika ya Mashariki nzima, kwa sababu walikuwa wakienda Nairobi kurekodi santuri za nyimbo zao. Lakini bendi hii ilikufa kutokana na mkasa wa kusikitisha sana. Walikuwa wakisafiri katika lori ambalo ndani yake pia kulikuwa na mzigo wa vinywaji, gari lile likapinduka na wanamuziki wote wakafa palepale, akabaki kiongozi wao tu aliyekuwa ametangulia kwa usafiri mwingine. Mungu awalaze pema…..Safari Iendelee.

Thursday, July 14, 2022

ZAMANI WATU WALIENDA DANSINI WAKAKUTA POMBE, SIKU HIZI WANAENDA KWENYE POMBE WANAKUTA DANSI

 

Kumbukumbu zangu huwa zinanirudisha Iringa nilipokuwa na umri wa miaka sita au saba hivi. Nadhani ndipo nilipoanza kutambua kuwa watu huwa wanaenda dansini. Maana mara kwa mara wazazi wangu walikuwa wanajitayarisha wanavaa nguo nzuri halafu wanatuaga ‘Haya laleni sisi tunaenda dansini’.
Moja ya dansi nakumbuka lilikuwa limepigwa na Cuban Marimba wakiongozwa na Salum Abdallah, nakumbuka kwa sababu kesho yake Mwalimu Nyerere alikuja kuhutubia watu wa Iringa kwenye uwanja ambapo upo sasa ni uwanja wa Samora. Wakati huo ulikuwa ni uwanja wa mpira wa shule ya Mshindo Middle School, na baba yangu alikuwa Headmaster wa shule ile. Nyumba yetu ilikuwa pembeni tu ya uwanja huo wa mpira. Siku hiyo alipokuja kuhutubia Mwalimu Nyerere, wimbo uliokuwa ukisikika kwenye spika ukirudia rudia, ulikuwa wimbo wa Cuban Marimba na baadhi ya  maneno yake yalikuwa ‘ Tutie jembe mpini, twendeni tukalime’, lazima ilikuwa baada ya Uhuru maana ndio nyimbo baada ya Uhuru zilivyokuwa na ujumbe wa kuhamasisha wananchi kujenga nchi mkoloni kisha ondoka.
 Wakati wimbo huo ukiimba, mama yangu akatuambia na wadogo zangu kuwa wimbo huo walikuwa wameucheza jana yake dansini. 

Kwa kweli toka nikiwa mtoto, dansi kwangu ni neno la furaha  kwenye maisha yangu. Nikiwa mdogo  wazazi wangu walikuwa wakituonyesha namna ya kucheza aina mbalimbali za dansi, zikiwemo tap dancing, aina ya dansi ambayo visigino vya viatu lazima uvigonge kwa nguvu sakafuni wakati wa kucheza kufuatia mapigo ya muziki, hivyo basi vinatoa beat fulani kufuatana na wimbo, dansi moja ngumu kuicheza maana inachosha baada ya dakika moja tu. Tulifundishwa kucheza  chachacha, waltz, foxtrot na aina nyingine za dansi ambazo sijapata hata  kujua majina yake.

Nyakati hizo na miaka mingi baadae, mtu akiaga anakwenda dansini, jambo la muhimu atakalolifanya huko ni kucheza nyimbo nyingi kadri atavyoweza. Kesho yake mazungumzo kuhusu dansini ni kuulizana nyimbo ngapi zilichezesha. Mpenzi wa muziki kurudi nyumbani akiwa kachoka kwa kucheza ilikuwa ndio dalili ya kufurahia kwa usiku ule.

Miaka mingi baadae hatimae nikaja kuwa mwanamuziki wa muziki wa dansi.  Hii aina ya muziki  uliokuja kuitwa muziki wa dansi, ulipewa jina hili kuanzia mwaka 1986 baada ya mkutano mkubwa wa wanamuziki ulioitishwa na Baraza la Muziki Tanzania kuja na wazo la kuwa na vyama vya muziki, ili kutofautisha na muziki wa Taarab, ndipo kikaundwa Chama cha Muziki wa Dansi na dhana ya muziki wa bendi ambao nia yake ilikuwa kucheza ukaitwa 'muziki wa dansi'.

Muziki wa bendi ambao sasa unaitwa muziki wa dansi, ulitungwa na hatimae kupigwa kwa vifaa vya kisasa na lengo kubwa ni kuwa wapenzi wa muziki huo watacheza.  Katika miaka ya hamsini na mwanzoni mwa miaka ya sitini, bendi zilikuwa zikitangaza aina muziki itakaoupiga, kwa mfano kiongozi wa bendi aliweza kutoa maelezo yafuatayo kabla ya kupiga wimbo. ‘Muziki ufuatao unaitwa Dada Adija, umepigwa katika mtindo wa Cha Cha’. Basi muziki ukianza wapenzi wa muziki wangeingia uwanjani na kucheza ChaCha. Na hivyo hivyo kama wimbo ni Twist, Bolelo, Charanga na kadhalika, hata kucheza kulikuwa na mpangilio unaoeleweka.

Tungo za zamani zilikamilishwa kwa muungano wa mawazo kutoka kwa wanamuziki mbalimbali katika bendi. Mtunzi wa awali aliweza kuleta  mashahiri, mara nyingine yakiambatana na melodia na kuwaimbia wenzie ambao walianza kutunga vipande vyao kupitia  vyombo mbalimbali wanavyovipiga. Tungo nyingi za awali zilianza kwa rumba, na ilipofika katikati mwendo ulibadilika na kuingia katika kile tulichokuwa tukikiita ‘chemka’.
 Chemka mara nyingi ilianza kwa kuimba na kisha kuingia kipande cha gitaa la solo. Hapa ndipo wapiga solo walikuwa wakipimwa kwa umahiri wao wa kutunga na kupiga vipande vya solo ambavyo vingeweza kuwateka akili wasikilizaji na kuwafanya wacheze dansi.



Katika bendi nilizopitia kama vile TANCUT Almasi na Vijana Jazz Band, baada ya bendi kukamilisha kuufanyia mazoezi wimbo, wimbo huo ulianza kupigwa katika maonyesho mbalimbali, lakini jambo la muhimu ambalo wanamuziki wote tulikuwa tukiliangalia lilikuwa ni Je, watu wanaucheza wimbo mpya? Ikionekana wimbo  umekosa hamasa ya kuwasimamisha  wachezaji, wimbo huo ulirudishwa mazoezini na kubadilisha vitu tulivyohisi vinafanya watu wasipende kucheza wimbo ule. Na mara nyingine wimbo huo ulitupwa pembeni moja kwa moja, mamia ya nyimbo  katika bendi mbalimbali ziliishia kupigwa kwenye kumbi mara moja tu na hazikurudiwa tena, kwa kuwa tu watu hawakuchangamkia kuzicheza.
Siku hizi mambo yako tofauti kabisa, unaweza kuingia kwenye onyesho la muziki wa Taarab, muziki ambao zamani ulikuwa ukisifika kwa kuwa muziki wa kusikiliza tu, ukakuta wapenzi wakitiririka jasho kwa kucheza nyimbo mbalimbali za Taarab. Na ukaingia katika onyesho la ‘muziki wa dansi’, ukakuta waimbaji wakitoka mishipa ya shingo, solo likapigwa kwa ufasaha, vyombo vingine vikachangia lakini hakuna anaeshughulika kucheza dansi hilo. Kama ingekuwa  zamani, hiyo ni dalili ya moja kwa moja kuwa muziki huo hauwafurahishi wapenzi. Lakini hizi ni zama nyingine.

Katika zama hizi, bendi huwa na wacheza show wake au hata waimbaji wa bendi nao wakatengeneza show yao, kisha wakawa wanapiga muziki na kucheza wao wenyewe. Ni kama nilinganishe na msemo maarufu wa  'kujitekenya halafu kucheka mwenyewe'. Wimbo ukiisha  wanamuziki huanza wimbo mwingine bila  kuhisi kuwa kuna tatizo.
Teknolojia imeleta aina nyingine ya kuonyesha upenzi na unazi wa muziki. Wapenzi wa muziki siku hizi huonyesha upenzi wao wa muziki kwa kuchukua simu na kurekodi  bendi ikiimba na kucheza, hawachezi wala kutikisika, kazi yao ni kunyanyua simu na kurekodi. Vipande hivi vya video husambazwa kwenye makundi ya Whatsapp, vikiambatana na sifa kuhusu ubora wa bendi hizi. Ndio namna ya zama hizi kufurahia muziki.
 Hakika kuna nyimbo ambazo wapenzi huchangamkia  kwa kucheza sana, lakini ukiangalia kila mtu anacheza akili inavyomtuma, hakuna tena mpangilio wa kucheza staili maalumu ya muziki. Ile staili ya wapenzi kukumbatiana kwa hisia wakati wa kucheza rumba imepotea, si ajabu kabisa kumkuta mtu anacheza na mpenzi wake, kila mtu na staili yake na wakati huohuo kila mmoja anatuma meseji kwenye simu. kweli zama zimebadilika mno.

Mwisho nimalizie na sentensi ya hali ninayoiona  katika muziki wa dansi, 'ZAMANI WATU WALIKWENDA DANSINI NA KUKUTA POMBE, SIKU HIZI WATU WANAENDA KWENYE POMBE NA KUKUTA DANSI'


 

Tuesday, July 12, 2022

TUZIKUMBUKE BENDI ZETU 3

 

SAFARI  yetu ya kuzikumbuka bendi mbalimbali nchini, wiki hii inatuingiza mkoa wa Iringa, lakini kati ya Iringa na Dodoma kuna wilaya inaitwa Mpwapwa. Hapa kulikuwa pia na bendi moja matata sana iliyoitwa  Mpwapwa Jazz Band. Bendi hii haikuwa ndogo kwani iliweza kurekodi nyimbo kadhaa ambazo zilipata umaarufu wa Kitaifa wakati wa uhai wake, ikiwemo wimbo Nilikuwa sina kazi, wimbo ambao unazungumzia hadithi ya kudumu ya kukimbiwa na mpenzi kutokana na kutokuwa na kipato.
Mji wa Iringa ulianza kama  ngome ya Wajerumani walipokuwa katika harakati za kumsaka Mutwa Mkwawa baada ya kuangusha ngome yake kule Kalenga. Hata jina Iringa limetokana na neno la Kihehe 'Lilinga' yaani ngome. Jeshi la Wajerumani likiwa na maafisa wachache wa Kijerumani, lilikuwa  na askari wengi wa Kiafrika kutoka pande mbalimbali za Afrika ya Mashariki na kati. Kulikuwa na askari wa Kinubi, askari wa Kimanyema, askari wa Kizaramo, askari wa Kinyamwezi na makabila mengine kadha wa kadha. Askari hawa wakaanza kuishi na familia zao maeneo yanayojulikana kama Miyomboni, jirani na kituo kikuu cha polisi ambapo haswa ndipo yalikuwa makao makuu ya jeshi la Wajerumani. 
Watoto na wajukuu wa askari hawa  walikuwa wakijitambulisha kuwa wao ndio wenyeji halali wa mji wa Iringa. Hivyo walikuwa na timu ya mpira iliyoitwa Boni kifupi cha Born Town, wakiwa wanamaananisha kuwa wao ndio wazawa haswa wa pale mjini. Na wakati huohuo wakaanzisha pia bendi iliyoitwa Born Jazz band, pengine kati ya bendi za awali za mji huu. Kama  ilivyokuwa Dodoma kuwa na bendi inaitwa Sextet Jazz band, Iringa kulikuwa na bendi inaitwa Habanero Jazz Band. Sextet na Habanero yalikuwa majina ya bendi mbili za huko Cuba. Katika zama hizo bendi za hapa nchini zilikuwa zikiiga muziki kutoka Cuba, si Congo. Bendi ya Iringa iliyokuja kupata umaarufu mkubwa ilikuwa Highland Stars Band. Mpiga gitaa Abel Balthazar ni moja ya wapigaji maarufu waliowahi kupitia bendi hii. Nyumbani kwa  mpiga solo maarufu wa Msondo Ngoma Ridhwani Abdul Pangamawe, ndipo yalipokuwa yakifanyika mazoezi ya Highland Stars Band. Mzee Abdul Pangamawe na mama Ridhwani wote walikuwa wakijua kupiga magitaa, si ajabu kabisa nyumba hiyo kutoa mpiga gitaa  na kinanda mahiri anayetingisha nchi mpaka leo. Moja ya wimbo wao maarufu wa Highland Stars ulikuwa ni Sitasita Mpenzi.

Bendi nyingine mjini Iringa ilikuwa ni Iringa Jazz Band, hii ilikuwa mali ya TANU Youth  League. Miji mingi sana ilikuwa na bendi za TANU Youth League katika miaka ya 60 na 70. 
Mkwawa High School, ambayo awali ilikuwa shule ya ‘Wazungu’ na iliyokuwa ikiitwa St George and St Michael European School, ilikuja kuwa na bendi nzuri sana ya wanafunzi iliyoitwa Orchestra Mkwawa. Wakiwa na mtindo wao waliouita Ligija walitoa burudani kila mwisho wa wiki katika ukumbi wa Welfare Center, katika utaratibu wa madansi ya mchana maarufu kama Buggy, wao kama wanafunzi hawakuwa na ruksa ya kuwa katika kumbi za dansi usiku, hivyo waliweza kupiga muziki huo mchana tu. Pia katika shule hiyo hiyo kulikuwa na bendi nyuingine iliyokuwa ikipiga muziki wa Kizungu na iliitwa Midnight Movers. Marehemu Eddy Hanspoppe, Deo Ishengoma, Martin Mhando walikuwa kati ya wanamuziki wa bendi hii. Vyombo walivyotumia vilikuwa ni vile ambavyo vilikuwa vikitumiwa na bendi iliyokuwa ya TANU Youth League. Magitaa ya bendi hii hatimae yalikuja kuchukuliwa na vijana wachache walioanzisha bendi iliyokuwa ikijulikana kama Chikwalachikwala. Chikwalachikwala ikajigawa na kukapatikana bendi iliyoitwa BOSE Ngoma, jina lililotokana na aina ya speaker walizokuwa nazo.

                                                    Chikwalachikwala Jukwaani Kijiji cha Mgama, 

Mwaka 1987 ikazaliwa Tancut Almasi Orchestra  bendi nyingine kubwa iliyowahi kutokea Iringa, bendi hii ilikuwa mali ya wafanyakazi wa kiwanda cha kuchonga almasi cha Diamond Cutting Company kilichokuwa pale Iringa. Majina ya wanamuziki maarufu waliopitia bendi hii ni mengi sana kati hao walikuweko mapacha Kasaloo Kyanga na Kyanga Songa, Banza Tax, Mafumu Bilali, Kawelee Mutimwana, Shaban Yohana Wanted, Kabeya Badu, Kalala Mbwebwe na wengine wengi akiwemo mwandishi wa makala hii.

TANCUT ALMASI ORCHESTRA JUKWAANI


Bendi nyingine iliyowahi kuweko Iringa  mjini ni Ruaha International Orchestra , iliyokuwa mali ya mfanya biashara mmoja aliyeitwa Mtandi. Bendi hii ilikuwa chini ya uongozi wa muimbaji marehemu Kalala Mbwebwe na wimbo wake Lutadila  ni kumbukumbu kubwa kwa wapenzi wa bendi hii. Bendi nyingine zilizowahi kuwa Iringa, zilikuwa ni VICO Stars iliyokuwa mali ya kanisa Katoliki, Living Light Band iliyokuwa mali ya hoteli ya Living Light.
Kumaliza mkoa huu bila kutaja bendi maarufu ya JKT Mafinga haitakuwa sawa. Bendi hii ilikuwa maarufu kwa jina la Kimulimuli, jina hili lilitokana na taa za disco zilizokuwa zinafungwa wakati bendi hii inapiga. Vyombo maarufu vya muziki aina ya Ranger FBT ambavyo vilikuwa vikitumika na bendi nyingi miaka ya 80 vilikuwa vinakuja na taa za disco, na wenyeji wa Mafinga walikuwa wakisema kwa Kihehe ‘Twibita kukina kimulimuli’ yaani tunaenda kucheza Kimulimuli, na hakika jina hilo ndilo likawa utambulisho wa bendi hiyo,  na hata bendi yenyewe ilitunga nyimbo kusifia jina lao la Kimulimuli.  Kati ya wanamuziki maarufu waliowahi kupitia bendi hii ni Zahiri Ally Zorro na Zakaria Daniel Mabula Tendawema ambaye niliandika alipata jina la Tendawema kutokana na kutunga wimbo ulioitwa Tenda wema nenda zako alipokuwa Shinyanga Jazz band. Safari inaendelea….