Tuesday, July 12, 2022

TUZIKUMBUKE BENDI ZETU 3

 

SAFARI  yetu ya kuzikumbuka bendi mbalimbali nchini, wiki hii inatuingiza mkoa wa Iringa, lakini kati ya Iringa na Dodoma kuna wilaya inaitwa Mpwapwa. Hapa kulikuwa pia na bendi moja matata sana iliyoitwa  Mpwapwa Jazz Band. Bendi hii haikuwa ndogo kwani iliweza kurekodi nyimbo kadhaa ambazo zilipata umaarufu wa Kitaifa wakati wa uhai wake, ikiwemo wimbo Nilikuwa sina kazi, wimbo ambao unazungumzia hadithi ya kudumu ya kukimbiwa na mpenzi kutokana na kutokuwa na kipato.
Mji wa Iringa ulianza kama  ngome ya Wajerumani walipokuwa katika harakati za kumsaka Mutwa Mkwawa baada ya kuangusha ngome yake kule Kalenga. Hata jina Iringa limetokana na neno la Kihehe 'Lilinga' yaani ngome. Jeshi la Wajerumani likiwa na maafisa wachache wa Kijerumani, lilikuwa  na askari wengi wa Kiafrika kutoka pande mbalimbali za Afrika ya Mashariki na kati. Kulikuwa na askari wa Kinubi, askari wa Kimanyema, askari wa Kizaramo, askari wa Kinyamwezi na makabila mengine kadha wa kadha. Askari hawa wakaanza kuishi na familia zao maeneo yanayojulikana kama Miyomboni, jirani na kituo kikuu cha polisi ambapo haswa ndipo yalikuwa makao makuu ya jeshi la Wajerumani. 
Watoto na wajukuu wa askari hawa  walikuwa wakijitambulisha kuwa wao ndio wenyeji halali wa mji wa Iringa. Hivyo walikuwa na timu ya mpira iliyoitwa Boni kifupi cha Born Town, wakiwa wanamaananisha kuwa wao ndio wazawa haswa wa pale mjini. Na wakati huohuo wakaanzisha pia bendi iliyoitwa Born Jazz band, pengine kati ya bendi za awali za mji huu. Kama  ilivyokuwa Dodoma kuwa na bendi inaitwa Sextet Jazz band, Iringa kulikuwa na bendi inaitwa Habanero Jazz Band. Sextet na Habanero yalikuwa majina ya bendi mbili za huko Cuba. Katika zama hizo bendi za hapa nchini zilikuwa zikiiga muziki kutoka Cuba, si Congo. Bendi ya Iringa iliyokuja kupata umaarufu mkubwa ilikuwa Highland Stars Band. Mpiga gitaa Abel Balthazar ni moja ya wapigaji maarufu waliowahi kupitia bendi hii. Nyumbani kwa  mpiga solo maarufu wa Msondo Ngoma Ridhwani Abdul Pangamawe, ndipo yalipokuwa yakifanyika mazoezi ya Highland Stars Band. Mzee Abdul Pangamawe na mama Ridhwani wote walikuwa wakijua kupiga magitaa, si ajabu kabisa nyumba hiyo kutoa mpiga gitaa  na kinanda mahiri anayetingisha nchi mpaka leo. Moja ya wimbo wao maarufu wa Highland Stars ulikuwa ni Sitasita Mpenzi.

Bendi nyingine mjini Iringa ilikuwa ni Iringa Jazz Band, hii ilikuwa mali ya TANU Youth  League. Miji mingi sana ilikuwa na bendi za TANU Youth League katika miaka ya 60 na 70. 
Mkwawa High School, ambayo awali ilikuwa shule ya ‘Wazungu’ na iliyokuwa ikiitwa St George and St Michael European School, ilikuja kuwa na bendi nzuri sana ya wanafunzi iliyoitwa Orchestra Mkwawa. Wakiwa na mtindo wao waliouita Ligija walitoa burudani kila mwisho wa wiki katika ukumbi wa Welfare Center, katika utaratibu wa madansi ya mchana maarufu kama Buggy, wao kama wanafunzi hawakuwa na ruksa ya kuwa katika kumbi za dansi usiku, hivyo waliweza kupiga muziki huo mchana tu. Pia katika shule hiyo hiyo kulikuwa na bendi nyuingine iliyokuwa ikipiga muziki wa Kizungu na iliitwa Midnight Movers. Marehemu Eddy Hanspoppe, Deo Ishengoma, Martin Mhando walikuwa kati ya wanamuziki wa bendi hii. Vyombo walivyotumia vilikuwa ni vile ambavyo vilikuwa vikitumiwa na bendi iliyokuwa ya TANU Youth League. Magitaa ya bendi hii hatimae yalikuja kuchukuliwa na vijana wachache walioanzisha bendi iliyokuwa ikijulikana kama Chikwalachikwala. Chikwalachikwala ikajigawa na kukapatikana bendi iliyoitwa BOSE Ngoma, jina lililotokana na aina ya speaker walizokuwa nazo.

                                                    Chikwalachikwala Jukwaani Kijiji cha Mgama, 

Mwaka 1987 ikazaliwa Tancut Almasi Orchestra  bendi nyingine kubwa iliyowahi kutokea Iringa, bendi hii ilikuwa mali ya wafanyakazi wa kiwanda cha kuchonga almasi cha Diamond Cutting Company kilichokuwa pale Iringa. Majina ya wanamuziki maarufu waliopitia bendi hii ni mengi sana kati hao walikuweko mapacha Kasaloo Kyanga na Kyanga Songa, Banza Tax, Mafumu Bilali, Kawelee Mutimwana, Shaban Yohana Wanted, Kabeya Badu, Kalala Mbwebwe na wengine wengi akiwemo mwandishi wa makala hii.

TANCUT ALMASI ORCHESTRA JUKWAANI


Bendi nyingine iliyowahi kuweko Iringa  mjini ni Ruaha International Orchestra , iliyokuwa mali ya mfanya biashara mmoja aliyeitwa Mtandi. Bendi hii ilikuwa chini ya uongozi wa muimbaji marehemu Kalala Mbwebwe na wimbo wake Lutadila  ni kumbukumbu kubwa kwa wapenzi wa bendi hii. Bendi nyingine zilizowahi kuwa Iringa, zilikuwa ni VICO Stars iliyokuwa mali ya kanisa Katoliki, Living Light Band iliyokuwa mali ya hoteli ya Living Light.
Kumaliza mkoa huu bila kutaja bendi maarufu ya JKT Mafinga haitakuwa sawa. Bendi hii ilikuwa maarufu kwa jina la Kimulimuli, jina hili lilitokana na taa za disco zilizokuwa zinafungwa wakati bendi hii inapiga. Vyombo maarufu vya muziki aina ya Ranger FBT ambavyo vilikuwa vikitumika na bendi nyingi miaka ya 80 vilikuwa vinakuja na taa za disco, na wenyeji wa Mafinga walikuwa wakisema kwa Kihehe ‘Twibita kukina kimulimuli’ yaani tunaenda kucheza Kimulimuli, na hakika jina hilo ndilo likawa utambulisho wa bendi hiyo,  na hata bendi yenyewe ilitunga nyimbo kusifia jina lao la Kimulimuli.  Kati ya wanamuziki maarufu waliowahi kupitia bendi hii ni Zahiri Ally Zorro na Zakaria Daniel Mabula Tendawema ambaye niliandika alipata jina la Tendawema kutokana na kutunga wimbo ulioitwa Tenda wema nenda zako alipokuwa Shinyanga Jazz band. Safari inaendelea….

1 comment:

  1. Ni kweli kabisa eneo la miomboni ndiko kulikuwa na timu ya Born kama ulivyoeleze.
    Ukiizungumzia Ruaha Intenational namkumbuka mpiga gitaa Juma Msosi huyu Bwana alikuwa mtumishi wa Serikali akifanya kazi pale Regional Bloc

    ReplyDelete