Wednesday, August 17, 2022

MJUE JEAN 'JOHNNY' BOKELO ISENGE

 

 


 Jean ‘Johnny’ Bokelo Isenge alizaliwa mwaka 1939 nchini Kongo, nje kidogo ya jiji la Kinshasa. Familia yake ilikuwa ni ya wanamuziki. Johnny alikuwa mdogo wa Paul Ebengo’Dewayon’ Isenge mwanamuziki mwingine aliyekuwa mkubwa sana nchini Kongo toka mwanzoni mwa miaka ya 50. Huyu Dewayon alikuwa na bendi inaitwa Watam, hapa ndipo Johnny alipoanzia muziki akipiga na mtoto mwingine aliyekuja kutikisa ulimwengu wa muziki Franco Luambo Luanzo, wakati huo Franco akiwa na miaka 12 tu. Johnny Bokelo aliendelea kupiga katika bendi alizoanzisha kaka yake kama vile Conga Jazz na Orchèstre Cobantu, lakini mwaka 1958 Johhn akaanzisha bendi yake, Orchestre Conga Succès, akiwa na mdogo wake Mpia Mongongo maarufu kwa jina la Porthos Bokelo, ambaye alikuwa mpiga gitaa la rhythm mahiri sana. Kaka yao Dewayon, akaja kujiunga na kundi hilo1960 lakini miaka miwili baadae1962 Johnny na kaka yake wakatengana. Bokelo alifanikiwa kulijenga kundi lake kuwa na nguvu na likawa kwa namna fulani linafanana sana na OK Jazz. Hata tungo nyingine zilikuwa ni za kujibu tungo za OK Jazz au kuzungumzia mada ambayo imeanzishwa na OK Jazz. Hii haikuwa kwa ugomvi bali kutokana na ukaribu uliokuwa kati ya Franco na Johnny. Kuna wakati Bokelo alianzisha mtindo wa kutunga nyimbo alizozipa jina la Mwambe, kukawa na Mwambe no 1 na 2 mpaka 5 ambapo alikuwa akiongea na kushangaa jamii inaelekea wapi. Upigaji wa Bokelo Dewayon na Franco ulishabihiana, pengine ni kutokana na wote kuanzia Watam. Mwaka 1968 Johnny Bokelo akabadili jina la kundi lake la Conga succès” na kulita “Conga 68” akaanzisha label yake akaanza kutoa santuri, hii ilimuongezea kipato japo wanamuziki wake walitishia kuachana nae kwani walisema hawakuwa wanapata fedha zozote kutokana na mradi huo. Santuri nyingi wakati huu alikuwa akiziachia kwanza kutoka Ufaransa ili kupata mapato zaidi. Kati ya 1972 mpaka 1974 Bokelo Isengo alikuwa anatumia muda mwingi zaidi akiwa studio, kwenye mwaka 1970, viwanda vya kutengeneza santuri vya Kinshasa vikawa vimechoka hivyo bokelo akaanza kupeleka master zake Kenya ili kutengeneza santuri. Mwaka 1980 Bokelo aliachana sana na shughuli za muziki.

Bokelo alifariki 15 January 1995 baada ya kuugua kwa muda mrefu

 

 



No comments:

Post a Comment