Showing posts with label ushauri. Show all posts
Showing posts with label ushauri. Show all posts

Thursday, August 18, 2022

KIKI, PROMO, PROPAGANDA, WATOTO WA BABA MMOJA

 


Kiki ni neno ambalo limekuwa maarufu zama hizi za Bongofleva. Kiki ni neno lilitokana na neno la Kiingereza, ‘kick’ yaani teke. Hivyo kiki maana yake katika ulimwengu wa wasanii ni kutafuta tukio ambalo litashtua jamii na kupaisha sifa yao au ya kazi yao. Ni kama vile ambavyo ukimpiga teke chura ndio unamsaidia kuruka. Hivyo wasanii wa zama hizi hutafuta kiki za aina mbalimbali ili kupaisha sifa za kazi zao, wengine hujitangaza kuwa wamefariki, wengine utakasikia wamefumaniwa, au wengine wameachana au wengine kutangaza wamerudiana au wameoana, au mara nyingine kueneza taarifa kuwa wimbo wao umeibiwa studio, na imefikia hata wazazi wa wasanii wengine kuingia kikamilifu katika shughuli za kiki kwa kutoa matamshi tata kuhusu kazi za watoto wao ili tu watu waelekeze masikio na macho yao kwenye kazi mpya. Pamoja na neno kiki kuwa jipya lakini hakika kutafuta kiki hakukuanza na Bongofleva. Makampuni yenye kutaka kutangaza bidhaa mpya sokoni, yamekuwa yakifanya matukio mengi makubwa kutafuta kiki. Makampuni hupitisha magari yenye maspika makubwa mitaani na kutangaza bidhaa zao, au hufanya matamasha makubwa, au huanzisha hata misemo tata ili tu kupata kiki ya bidhaa zao. Lakini hapa haiitwi kiki inaitwa promosheni. Wanasiasa nao hakika ni mabingwa wa kiki,wakati wa kutafuta kura, kila aina ya vituko hufanyika. Tumeshaona wanasiasa wanapiga magoti kuomba kura, wengine hata kugaragara chini wakiomba kura, hao wanaoamua kucheza ngoma za kiasili au dansi jukwaani ni kawaida sana.  Na wakifungua mdomo kueleza sifa walizonazo na watakachokifanya vyote ni kujinadi ili kuonekana bora, ila huku haiitwi kiki inaitwa siasa, au wengine huiita propaganda. Zama hizi hata viongozi wa dini nao wamo katika kutafuta kiki, utasikia wakishusha sifa za uwezo wao kama katika vyombo mbalimbali vya matangazo, wengine wamefikia mpaka kuingilia matatizo ya wasanii maarufu ili nao wajulikane kuwa wapo. Kutokana na malezi duni ya baadhi ya wasanii, kiki hizi zimekuwa zikichukua sura mpya siku hadi siku. Kwa sasa zimefikia hata kuongea, kutangaza au kuonyesha vitu vya faragha hadharani, ikiwa kama njia ya kutafuta kiki, na hapo ndipo ugomvi na watu wenye busara zao unapoanza.

Kama nilivyosema mwanzo neno kiki ni geni lakini shughuli zake si ngeni kabisa. Bendi za zamani zilikuwa na njia kuu moja tu ya kupata pesa nayo ilikuwa kwa  kiingilio mlangoni, gate collection, na hakika kulilazimika kuweko na mbinu za kujitangaza, au kutafuta kiki. Kulikuwa na njia kuu tatu za kutangaza onyesho,  kwanza ni kupitia redioni na pili kupitia magazeti, na tatu kwa kubandika matangazo kwenye kuta na nguzo za umeme. Magazeti yaliyokuwa yakishughulika na muziki yalikuwa ni magazeti ya serikali, magazeti ya Chama Cha Mapinduzi na magazeti ya chama cha wafanyakazi, NUTA na baadae JUWATA.  Vyombo hivi havikuwa na maadili ya kuruhusu ‘kiki’ za maisha binafsi ya wanamuziki, matangazo yalilazimika kuwa yanayohusu muziki tu.  Hivyo ubunifu ulikuweko, bendi zilijinadi kwa staili zake zenye mvuto ili kutafuta kiki. Kulikuweko staili kama  Katakata mwendo wa jongoo vumbi nyuma, Bomoa tutajenga kesho, Super mnyanyuo, Sikinde ngoma ya ukae, Mahepe ngoma ya wajanja, Dunda dunda, Bayankata, Kokakoka balaa  na majina mengine mengi. Matangazo kwenye magazeti yaliwekwa picha za wanamuziki au kuchorwa picha za kujinadi kwa njia moja au nyingine. Maswala ya kuachana, kupendana, kuhongana, kufumaniana hayakuhusika kabisa katika kutangaza kazi ya muziki. Nikifikiria sana nadhani vitu ambavyo wasanii wa sasa hufanya katika kutafuta kiki, vingefanywa na wasanii wa miaka ile na kutangazwa kama ilivyo sasa ingekuwa ndio mwisho wa msanii huyo, jamii ingemtema.

Nadhani moja ya sababu ya kuweko kwa kiki za ajabu katika zama hizi, ni kujaribu kujazia mapungufu yaliyomo kwenye sanaa husika. Msanii anakuwa anajua hata yeye kuwa kazi yake ni duni,  hivyo anazua kitu kisichohusika kabisa na kazi yake ya sanaa ili kuweza kuwafanya wateja japo wasikilize kazi yake kwa muda.

Taratibu za kurekodi siku hizi nazo zinafanya msanii asiwe na uhakika wa mpokeo ya wimbo wake hivyo kulazimisha vituko ili kujulikana kama ana kazi mpya. Msanii wa kizazi cha sasa anaweza kutunga wimbo asubuhi akaingia studio na kukamilisha wimbo na jioni wimbo uko tayari youtube na umeanza kurushwa kwenye vyombo ya utangazaji mbalimbali,

Hali haikuwa hivyo zamani, ukiwa na wazo la wimbo unalipeleka kwenye bendi yako yenye watu zaidi ya saba, wao wanakusikiliza na kuamua kama uchukuliwe na bendi au la, wakikubali ndipo mnaanza kuujenga wimbo, magitaa, ngoma. vyombo vya upulizaji, kila mtu anatoa wazo lake. Wimbo ulichukua japo siku mbili kukamilika, ingawa kuna nyimbo zilichukua hata zaidi ya wiki kuwa tayari. Bendi ikiridhika , wimbo ulianza kupigwa kwenye maonyesho, na hapa ndipo wapenzi wa bendi walikuwa wakiingia na kutoa maoni yao, mkikubaliana ndipo unaenda kurekodiwa. Mara nyingi bendi zilikuwa zinajua kabla hata ya kwenda kurekodi wimbo gani utakuwa maarufu kutokana na maoni ya wapenzi. Kwa taratibu hizo kiki za kujidhalilisha zilikuwa hazina nafasi, kazi ilikuwa inajiuza yenyewe.

Friday, August 12, 2022

HAKIKA DANSI LIMEBADILIKA SANA

 


Kweli dansi limebadilika sana.

Kumbukumbu zangu huwa zinanirudisha Iringa nilipokuwa na umri wa miaka minne hivi. Nadhani ndipo nilipoanza kutambua kuwa wazazi wangu walikuwa wanajitayarisha kwenda dansini, nakumbuka wakituaga na kutumbuambia ‘Haya laleni sisi tunaenda dansini’. Moja ya dansi nakumbuka lilikuwa limepigwa na Cuban Marimba wakiongozwa na Salum Abdallah, nakumbuka kwa sababu kesho yake Mwalimu Nyerere alikuja kuhutubia kwenye uwanja ambapo upo sasa ni uwanja wa Samora. Wakati huo ulikuwa ni uwanja wa mpira wa shule ya Middle School na baba yangu alikuwa Headmaster wa shule ile, na nyumba yetu ilikuwa pembeni tu ya uwanja huo wa mpira.
Siku alipokuja kuhutubia Mwalimu Nyerere, wimbo uliokuwa ukisikika kwenye spika ukirudia rudia, ulikuwa wimbo wa Cuban Marimba na baadhi ya  maneno yake yalikuwa ‘ Tutie jembe mpini, twendeni tukalime’. Mama akatuambia na wadogo zangu kuwa wimbo huo walikuwa wameucheza jana yake dansini. Kwa kweli toka nikiwa mtoto, dansi kwangu ni neno la furaha  kwenye maisha yangu. Nikiwa mdogo  wazazi wangu walikuwa wakituonyesha namna ya kucheza aina mbalimbali za dansi, zikiwemo tap dancing, aina ya dansi ambayo viatu lazima uvigonge sakafuni wakati wa kucheza kufuatia mapigo ya muziki, wazazi walitufundisha kucheza  chacha, waltz na aina nyingine za dansi ambazo sijapata hata  kujua majina yake.
Nyakati hizo na miaka mingi baadae, mtu akiaga anakwenda dansini, jambo la muhimu atakalolifanya huko ni kucheza nyimbo nyingi kadri atavyoweza. Kesho yake mazungumzo kuhusu dansini ni kuulizana nyimbo ngapi zilichezesha. Mpenzi wa muziki kurudi nyumbani akiwa kachoka kwa kucheza ilikuwa ndio dalili ya kufurahia kwa usiku ule.

Miaka mingi baadae hatimae nikaja kuwa mwanamuziki wa muziki wa bendi,  aina ya muziki ambao miaka ya 80 ulianza kuitwa muziki wa dansi, ulipewa jina hili kuutofautisha na aina nyingine za muziki kama vile taarab,  kwaya, muziki wa asili na aina nyingine za muziki. Muziki huu wa dansi ulikuwa ni ule uliopigwa kwa vifaa vya kisasa na kutegemea kuwa lazima utachezwa, tena kwa mtindo maalumu.  
Katika miaka ya hamsini na mwanzoni mwa miaka ya sitini, bendi zilikuwa zikitangaza aina muziki itakaoupiga, kwa mfano kiongozi wa bendi aliweza kutoa maelezo yafuatayo kabla ya kupiga wimbo. ‘ Muziki ufuatao unaitwa Dada Adija, umepigwa katika mtindo wa Cha Cha’. Basi muziki ukianza wapenzi wa muziki huingia uwanjani na kuonyesha umahiri wao wa kucheza ChaCha. Na hivyo hivyo kama wimbo ni Twist, Bolelo, Charanga na kadhalika. 

Utunzi wa zamani

Utunzi wa nyimbo mpya za bendi ulikamilishwa kwa muungano wa mawazo kutoka kwa wanamuziki mbalimbali katika bendi. Mtunzi wa awali aliweza kuleta  mashahiri, mara nyingine yakiambatana na melodia na kuwaimbia wenzie ambao kama wangeukubali, walianza kutunga vipande mbalimbali vya wimbo kupitia  vyombo mbalimbali wanavyovipiga. Tungo nyingi za awali zilianza kwa rumba, na ilipofika katikati mwendo ulibadilika na kuingia katika kile tulichokuwa tukikiita ‘chemka’.
 Chemka mara nyingi ilianza kwa kuimba na kisha kuingia kipande cha gitaa la solo. Hapa ndipo wapiga solo walikuwa wakipimwa kwa umahiri wao wa kutunga na kupiga vipande vya solo ambavyo vingeweza kuwateka akili wasikilizaji na kuwafanya wacheze dansi.
Katika bendi nilizopitia kama vile TANCUT Almasi na Vijana Jazz Band, baada ya bendi kukamilisha wimbo, ulianza kupigwa katika maonyesho mbalimbali, lakini jambo la muhimu ambalo wanamuziki wote tulikuwa tunaliangalia lilikuwa Je, watu wanaucheza wimbo mpya? Ikionekana wimbo  umekosa hamasa ya kuwasimamisha  wachezaji, wimbo huo ulirudishwa mazoezini na kubadilisha vitu tulivyohisi vinafanya watu wasipende kucheza wimbo ule. Na mara nyingine wimbo huo ulitupwa pembeni moja kwa moja kama haukuchezesha, mamia ya nyimbo  katika bendi mbalimbali ziliishia kupigwa kwenye kumbi mara moja tu na hazikurudiwa tena, kwa kuwa tu watu hawakuchangan mkia kuzicheza.
Siku hizi mambo yako tofauti kabisa, unaweza kuingia kwenye onyesho la muziki wa Taarab, muziki ambao kwa asili ulikuwa ukisifika kwa kuwa muziki wa kusikiliza tu, ukakuta wapenzi wakitiririka jasho kwa kucheza nyimbo mbalimbali za Taarab, halafu ukaingia katika onyesho la ‘muziki wa dansi’, ukakuta waimbaji wakitoka mishipa ya shingo lakini hakuna anaeshughulika kucheza dansi hilo. Kama ingekuwa  zamani, hiyo ni dalili ya moja kwa moja kuwa muziki huo hauwafurahishi wapenzi. Lakini hizi ni zama nyingine.

Katika zama hizi, bendi huwa na wacheza show wake au hata waimbaji nao wakatengeneza show, kisha wakawa wanapiga muziki na kucheza wao wenyewe. Sijui nilinganisha na kujitekenya halafu kucheka mwenyewe?
Teknolojia imeleta aina nyingine ya kuonyesha upenzi na unazi wa muziki. Wapenzi wa muziki siku hizi huonyesha upenzi wao wa muziki kwa kuchukua simu na kurekodi video za  bendi zikiimba na kucheza, wao wenyewe wakiwa wamekaa kwenye viti wakiendelea kunywa vinywaji vyao, kisha vipande hivi vya video husambazwa kwenye makundi ya Whatsapp, vikiambatana na sifa kuhusu ubora wa bendi hizi. Ndio namna ya ‘ku appreciate’ muziki zama hizi.
Lakini pia kuna madansi ambayo utakuta wapenzi wamechangamka wanacheza sana, lakini ukiangalia kila mtu anacheza akili inavyomtuma, hakuna tena mpangilio wa kucheza staili maalumu ya muziki. Ile staili ya wapenzi kukumbatiana kwa hisia wakati wa kucheza rumba imepotea, si ajabu kabisa kumkuta mtu na mpenzi wake wanacheza wimbo wa taratibu, lakini kila mtu na staili yake na juu ya hayo kila mmoja anatuma meseji kwenye simu yake.
Hakika dansi limebadilika sana

 

Wednesday, August 10, 2022

WANAMUZIKI WA SASA WANAKUBALI KUKOSOLEWA?

 

Top Ten Show 1989

Jana nilikuwa naangalia maktaba yangu ya kanda za video za zamani, nikaiona kanda moja iliyonirudisha miaka mingi sana nyuma. Ilikuwa ni kanda ya video ya onyesho moja la bendi ya Tancut Almasi Orchestra lililofanyika katika ukumbi wa klabu ya bendi hiyo eneo la Sabasaba pale Iringa.
Mwaka 1989 yalianza kufanyika mashindano ya bendi yaliyoitwa Top Ten Show, mashindano haya yalifikia kilele mwaka 1990. Yalikuwa ni mashindano makubwa sana ya muziki wa dansi na mpaka leo hayajawahi kufanyika mashindano ya bendi yenye ukubwa ule. Mashindano haya yaliyotayarishwa kwa ushirikiano wa CHAMUDATA, Radio Tanzania na Umoja wa Vijana wa CCM, yalianza tarehe 29 Julai 1989 na kufikia kilele tarehe 25 November 1989. Bendi zilizoshiriki zilikuwa 50 kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Arusha , Kilimanjaro, Tanga, Iringa,  Mbeya,  Morogoro, Rukwa , Kigoma na Pwani. Hii ilikuwa maendeleo kwani Top Ten Show ya mwaka 1988 ilikuwa na bendi 27 tu. Wafanyakazi wa Radio Tanzania Dar es Salaam  walizunguka katika mikoa mbalimbali na bendi za huko zilifanya maonyesho ambayo yaliyorushwa ‘live’  redioni na hivyo kuwapa wasikilizaji nchi nzima nafasi ya kusikiliza na kufuatilia mashindano hayo katika hatua zote.  Mwaka huo nilishiriki mashindano haya wakati nikiwa mmoja wa wanamuziki wa bendi ya TANCUT Almasi Orchestra iliyokuwa na masikani yake mjini Iringa.  Masharti ya mashindano tulipewa mapema sana. Kila bendi ilitakiwa ijitayarishe kwa nyimbo tatu, mmoja uwe unaitwa Nakulilia Afrika, wimbo wa pili ulikuwa lazima utokane na wimbo wa tuni ya asili ya kabila mojawapo la Tanzania na wimbo wa tatu uwe wimbo wowote ambao bendi ilipendelea kuupiga. Tulianza kufanya mazoezi makali  ya nyimbo hizo. Marehemu Kasaloo Kyanga na pacha wake Kyanga Songa wakaja na tungo yao ya wimbo Afrika Nakulilia, na mimi nikatoa mchango wa wimbo wa asili ya Kihehe ulioitwa Lung’ulye, kwa pamoja tukaamua kuwa wimbo wetu wa tatu uwe Ngoma za Afrika uliokuwa utunzi wa Kalala Mbwebwe.
Baada ya mazoezi makali tuliamua kufanya onyesho lisilo la kiingilio na kuwakaribisha wapenzi wa muziki wa dansi pale Iringa kuja kutoa maoni yao kuhusu matayarisho yetu hayo.  Mkuu wa Mkoa wa Iringa wakati huo, Mama Mary Chipungahelo alikuwa mgeni rasmi  wa onyesho hilo. Kilichofanyika pale siku ile, kilikuwa si kitu ambacho naona kitawezekana kwa urahisi katika zama hizi. Baada ya kupiga nyimbo zile wapenzi walikaribishwa jukwaani  kuongea ukweli kuhusu nyimbo zile, tuliomba waliotaka kutoa sifa wakae nazo, tulichokuwa nania nacho ni mapungufu katika matayarisho hayo. Hakika kulikuweko maneno makali ambayo sidhani wasanii wengi siku hizi wangekubali kukosolewa vile. Kulikuwa na kukosoa kuanzia mavazi, uchezaji na hata tungo zenyewe. Tungo ya Afrika Nakulilia iliyotungwa na akina Kasaloo ilikataliwa kwani ilionekana ilitokana na wimbo wa Pepe Kalle, hivyo muimbaji Kalala Mbwebwe na mpiga gitaa la solo Kawele Mutimwana wakaleta tungo nyingine ambayo ndio ilikuwa moja ya kete zetu katika mashindano yale.



Baada ya kuvuka kigingi cha wapenzi wetu wa Iringa, tulikuja Dar es Salaam na tulikuwa tumepangiwa katika kituo cha ukumbi wa Silent Inn uliokuwa eneo la Mpakani Dar es Salaam. Katika onyesho hilo, tulikuwa jukwaani pamoja na bendi iliyokuwa ikiitwa Orchestra Linga Linga Stars wakati huo muimbaji wake mahiri alikuwa Karama Regesu ambaye kwa sasa yupo Msondo Music Band. Tancut tukaibuka kuwa katika bendi kumi bora na kuja kushiriki fainali za onyesho lile zilizofanyika uwanja wa Taifa. 
Baadhi ya bendi zilifika kumi bora  zilikuwa, Tancut Almasi, Super Matimila, MK Group, Salna Brothers, Varda Arts, Bima Lee, Kilimanjaro Band na Vijana Jazz Band, hakika Uwanja wa Taifa palipendeza siku ile. Lakini kwangu mimi mambo yalikuwa na utata kidogo kwani siku ya fainali, nilikuwa nimeshamia Vijana Jazz Band, lakini kwa siku hiyo nilirudi bendi yangu ya zamani ya  Tancut Almasi  kwani wakati wa mashindano nilishiriki katika bendi hiyo. Uwanja wa Taifa ulijaa wanamuziki wengi sana, na kwa kuwa bendi zilikuwa na ustaarabu wa kuvaa sare, basi sare za aina mbalimbali zilitawala siku hiyo.

Ushindi wa TANCUT

 Hatimae matokeo yalitangazwa na kila wimbo ulikuwa na mshindi wa kwanza mpaka wa kumi, washindi watatu wa kwanza wakipata zawadi mbalimbali. Wimbo wangu wa asili ya Kihehe, ulishinda zawadi ya kwanza katika nyimbo za kiasili na washiriki wote tulipewa ‘radio cassette’ zilizotolewa na Ubalozi wa Uholanzi. Wimbo Afrika Nakulilia ulishika nafasi ya pili na wimbo uliokuwa chaguo la bendi ulikuwa Ngoma za Kwetu uliokuwa utunzi wa Kalala Mbwebwe ulichukua nafasi ya nne katika kundi lake, Kwa ujumla matokeo yalikuwa mazuri sana kwa bendi ya TANCUT Almasi.
Wanamuziki na viongozi wa TANCUT ALMASI Orchestra wakiwa na zawadi zao


 Art Critic

Katika nchi ambazo sanaa imekuwa, huwa kuna watu wanaoitwa ‘art critics’, hawa kwa kweli ni mabingwa katika fani za sanaa wanazo shughulikia na wao kazi yao moja kubwa ni kukosoa kazi mbalimbali za sanaa na hatimae hata kuzipa grade. Kwa mtizamo wa haraka haraka utaweza kudhani kuwa kukosoa kwao kunaweza kuharibu soko la sanaa husika, lakini kwa kuwa hawa watu huwa wakweli na wenye uzoefu, wasanii huwa wanafuatia sana watu hawa wanasemaje kuhusu kazi zao. Kupasishwa na watu hawa hupandisha thamani ya sanaa husika. Wakosoaji hawa pia huwafanya wasanii wawe makini katika kazi zao na hivyo ubora wa sanaa nzima unapanda.  Kitendo cha bendi ya TANCUT kuruhusu kukosolewa kabla ya kuingia katika mashindano ilikuwa sababu moja wapo ya bendi kupata ushindi mnono katika mashindano yale. Wasanii wa sasa hapa nchini wako tayari kukosolewa?