AUDAX(kushoto) akiwa na Kasongo Mpinda |
Thursday, April 23, 2015
MWANAMUZIKI MKONGWE MUTOMBO LUFUNGULA AUDAX HATUNAE TENA
Tuesday, April 21, 2015
MWANAMUZIKI WA SIKU NYINGI PAUL GAMA AFARIKI DUNIA
KWA MASIKITIKO MAKUBWA TUMETAARIFIWA KUWA MWANAMUZIKI WA ZAMANI PAUL GAMA AMEFARIKI DUNIA HUKO DODOMA TAREHE 16.4.2015 MUDA WA SAA NNE ASUBUHI. NARUDIA MAKALA HII YA HISTORIA YA PAUL GAMA KADRI ALIVYOTUELEZA MWENYEWE
Paul Daniel Gama |
Paul
Daniel Gama alizaliwa Barabara ya 11 Dodoma (1947). Baba yake alikuwa ni
mwanajeshi wa KAR mwenye asili ya Songea na mama yake alikuwa na asili ya
Usangu alikuwa anafanya kazi
katika
Spokes Mashiyane na filimbi yake |
hospitali ya Mirembe ambayo wakati huo ilikuwa ni hospitali kubwa
ya majeruhi wa vita ya pili ya dunia. Aliingia shule na alipofika darasa la
nne alijikuta akiwa na kipaji kukubwa cha kupiga filimbi, wakati huo wapiga
filimbi walipenda sana kumuiga mpiga filimbi maarufu kutoka Africa ya Kusini
Spokes Mashiyane. Akiwa na wenzie walianzisha kikundi ambacho kilikuwa na
maskani eneo la Mji Mpya pale Dodoma. Vijana hao pia walikuwa wakiiga nyimbo za wanamuziki maarufu wa wakati
huo, kama Salum Abdallah na Cuban
Marimba, pia Salum Zahor na Kiko Kids. Katika kufanya fani yao hiyo kama kitu
cha kujipa burudani waliligusa sikio la
aliyekuwa mwalimu wa Elimu ya Watu Wazima katika Community Center ya
pale Dodoma. Mwalimu huyu aliwasaidia kuwaazimia amplifaya moja kutoka kwenye
bendi nyingine ilikuweko Dodoma wakati huo, The Jolly Sextet Band. Band
iliyokuwa ikimilikiwa na Mkenya mmoja ambaye alifika Dodoma kama mfanya kazi wa
East African Postal and Telecommunication Services, huyu bwana alikuja na vyombo vingi akaanzisha
bendi ambayo mmoja wa wapigaji wake alikuwa Mzee Mnenge ambaye hatimaye alitua
NUTA Jazz Band.
Bongos |
Hiki
kikundi cha Gama na wenzie kilikuwa katika mfumo wa Jazz Band za zamani
ambapo walikuwa na ngoma na filimbi tu,ikisindikizwa na kuimba, lakini waliweza
kukonga nyoyo hata za wanamuziki wengine, na Gama akawa anasakwa na bendi
kubwa iliyokuweko wakati ule Central Jazz band. Alipomaliza darasa la saba tu
ndugu yake aliyeitwa Titus Olaf Gama alimshawishi aingie Central Jazz lakini
hakuwa tena mpiga filimbi bali mpiga Bongos, fani aliyoiweza sana hata kuipenda na hasa baada ya kuwaona
wanamuziki wa NUTA akiwemo Muhidin Gurumo
ambaye wakati huo alikuwa akipiga Bongos na kuimba. Bongos no ngoma
ndogo zilizokuwa muhimu katika kundi wakati huo ambapo hakukuweko na drums wala
tumba. Taratibu akaanza kupata hamu ya kupiga bass, wanamuziki wenzie
walimkatisha sana tamaa kwa kuambiwa kuwa vidole vyake vilifaa sana kwa kupiga
bongos na si kupiga gitaa.
Katika
jitihada zake za kujifunza gitaa la bezi alikuwa kila mara akiwahi mazoezi na
kujaribu kujifunza gitaa la bezi. Hilo lilikuwa gumu mpaka pale bendi ya Lake Jazz Band ilipotembelea Dodoma.
Bendi hiyo wakati huo ikiwa na wanamuziki kama Shem Karenga akiwa anapiga gitaa la bezi, Mzee alum
ambaye alikuwa na ulemavu wa macho, mwanzo alikuwa akipiga gitaa la solo na
baadae akahamia kupiga gitaa la rhythm wakati gitaa solo lilikuja kupigwa na
jamaa aliyeitwa Kally. Kutokana na simulizi ni wazi kuwa wanamuziki wa kutoka
Burundi walikuwa wengi sana nchini wakati huo. Pia katika bendi hiyo alikuweko
Mzee Juma Kitambi, mtunzi wa wimbo maarufu wa Rangi ya Chungwa.
Gama
alichukua nafasi hii kumfuata Mzee Salum ili aweze kumfundisha gitaa. Kwa kuwa
wanamuziki wengine walikuwa wakitoka kwenda kutembea Mzee Salum alibaki
nyumbani na hivyo Gama alichukua nafasi hiyo kumnunulia sigara Mzee Salum ana
kumsihi amfundishe gitaa nae alifanya hivyo na Gama akatokea kuwa mpiga bezi
mahiri.
Katika
kipindi hiki akatokea mfanya biashara Mohamed Omar Badwel, huyu alikuwa na
gereji na studio ya kupiga picha, aliweza kwenda Mombasa na kurudi na seti ya
vyombo na kuanzisha Dodoma Jazz Band. Gama akahama Central Jazz Band na
kujiunga na wanamuziki wengine walioanzisha Dodoma Jazz. Band ilianza ikiwa na
mpiga solo Hassan Mursali mwanamuziki mweny asili ya Malawi, siku hizo ikiitwa
Nyasaland alikuwa ndie mpiga solo, lakini aliwaacha baadae na kujiunga na NUTA
Jazz Band, upigaji wake wa solo unaweza kuusikia katika kusikiliza kibao kimoja
maarufu cha NUTA, kilichoitwa Dunia Njema
Kukaa Wawili.
Hasan
alikuwa mtu wa kuhama hama hatimae alipoteza uwezo wa kusikia jambo ambalo
lilihusishwa na kuhamham kwake kwani ushirikina ulitawala sana wakati huo, kama
maelezo yanayofuata yanavyoonyesha. Dodoma Jazz ilikuwa pia inafanya ziara
katika sehemu nyingi , kama vile Iringa, Mbeya ,Tabora, Dar es Salaam na
kadhalika, lakini safari moja ya kwenda Kilosa ilifanyika ikiwa na lengo la
kumfuata Abel Barthazal aliyekuwa akipiga katika bendi ya Kilosa Jazz.
Bendi ilipokelewa vizuri na wakafanya
maonyesho yao Kilosa na hatimae kuondoka na Abel. Siku chache baade wakati huo
Mzee Mohamed Omar, mwenye bendi
alikuwa kasha mnunulia suti kadhaa Abel, ukaja ugeni toka Kilosa wakiwa na
barua yenye maelezo kuwa ikiwa Abel Hatarudi Kilosa, mmoja wa wanamuziki wa
Dodoma Jazz atafariki, na barua hii ililetwa kwa mkono na mjumbe ambae
alisisitiza wakishaisoma mbele yake ndio anaondoka. Abel alirudishwa Kilosa
mara moja.
Baada
ya hapo aliyekuwa meneja wa bendi Ramadhan Waziri alitumwa Burundi kwenda
kutafuta wapigaji, siku alipokuwa anarudi na wapigaji wapya akakutana kwenye
treni na Rashid Hanzuruni, mpiga solo mahiri sana ambaye upigaji wake husikika
katika wimbo Napenda nipate lau nafasi
Hanzuruni
alikuwa kaiacha Tabora Jazz baada ya
kutokea ugomvi mkubwa ambapo alipoteza meno kadhaa, hivyo alikuwa kwenye
hilo treni akielekea Dar es Salaam kumfuata mpigaji mwenzie Samba ambae alikuwa
NUTA Jazz. Ramadhani aliweza kumshawishi hanzuruni akabaki Dodoma Jazz ambako
alikaa kwa muda na hatimae akaja kuchukuliwa na Sama ili aingie NUTA Jazz,
ndoto hiyo haikufanikiwa kwana NUTA alikuweko mpigaji mahiri Hamisi Franco, hii ndiyo ilipelekea
Hanzuruni kwenda Western Jazz Band
Friday, January 16, 2015
IMETIMIA MIAKA 36 TOKA KIFO CHA MBARAKA MWINSHEHE, MUZIKI WAKE BADO UKO HEWANI
Mbaraka
Mwinshehe Mwaruka alizaliwa mjini Morogoro Juni 27, 1944. Siku ya
Januari 12, 1979 ulimwengu wa muziki Tanzania ulitikiska kwa simanzi
baada ya kusikika kifo cha mwanamuziki huyo, mpiga gitaa muimbaji,
mtunzi na kiongozi wa bendi wa miaka mingi na ambaye bendi yake ilikuwa
imepiga karibu kila wilaya ya nchi hii. Taarifa ziliingia jioni ya siku
ile kupitia redio ya Taifa kuwa nguli huyu alifia katika hospitali
katika jiji la Mombasa nchini Kenya muda wa saa 1:55 jioni kufuatia
ajali ya gari...........ENDELEA HUKU
Tuesday, December 16, 2014
HATIMAE SHEM IBRAHIM KARENGA AZIKWA
HATIMAE
mwanamuziki mkongwe mpiga gitaa muimbaji na mtunzi mahiri Shem Ibrahim
Karenga amezikwa katika makaburi ya Kisutu jioni ya leo. Shughuli hiyo
ilianza kwa utata baada ya kuwa makaburini hapo kulikuwa na misiba minne
hivyo kila lilipokuja jeneza wanamuziki, ndugu na wapenzi wa muziki
walijikuta wakisindikiza jeneza na..........INAENDELEA HUKU
Monday, December 15, 2014
BURIANI SHEM IBRAHIM KARENGA
LEO
Jumatatu tarehe 15 Desemba 2014, majira ya saa nne asubuhi taarifa
zilianza kusambaa kuwa mwamba mwingine wa muziki wa dansi Tanzania
umedondoka. Mzee Shem Karenga hatunae tena,kwa vyovyote waliohudhuria
dansi alilopiga Ijumaa na Jumamosi iliyopita pale Mwembeyanga watakuwa
hawaamini, lakini imekuwa mapenzi ya Mungu, kwamba asubuhi ya leo
aliamka hajisikii vizuri na alipelekwa hospitali ya Amana lakini
hakukuweza kufanyika kitu Mzee akarudi kwa Muumba wake. Mungu aipokee
roho yake. Miezi michache iliyopita tulipata muda mrefu wa kuongea na
Mzee Shem Karenga ili kujua alikotokea na mawazo yake kwa sasa
mazungumzo yalikuwa kama ifuatavyo;................................. ENDELEA HUKU
Monday, November 10, 2014
LEO NIMEKUMBUKA KIBAO MASAFA MAREFU CHA TANCUT ALMASI...angalia video
Saturday, November 8, 2014
HISTORIA FUPI YA TAARAB
Taarab
ina historia ndefu katika muziki wa Tanzania kama ulivyokuwa muziki wa
dansi. Wapenzi wa taarbu wa zamani waliiweka taarabu katika vyanzo kama
Taarab ya Tanga, Taarab ya Dar es Salaam,Taarab ya Zanzibar na Taarab ya
Mombasa. Taarab ya Zanzibar wakati huo........INAENDELEA HUKU
Wednesday, October 22, 2014
MIAKA KUMI YA KUMBUKUMBU YA KIFO CHA NDALA KASHEBA
LEO
tunatimiza miaka kumi toka kifo cha mwanamuziki mahiri Freddy Supreme
au maarufu kama Ndala Kasheba. Freddy alianza kufundishwa gitaa na baba
yake wakati akiwa na umri wa miaka 12. Baba yake alijua kupiga gitaa
japo hakufanya kazi ya uanamuziki, alikuwa akipiga gitaa nyumbani baada
ya saa za kazi. Moja ya bendi maarufu ambazo zilimtambulisha sana Fredd
ilikuwa Orchestra Fauvette, Freddy alieleza kuwa bendi ya Orchestra
Fauvette ilianza tarehe 7 mwezi wa sita mwaka 1964 katika jiji la
Lubumbashi huko Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo. Jina hilo Fauvette........ENDELEA HUKU
Saturday, October 11, 2014
ALLY RASHID AZIKWA KEKO
Umati mkubwa wa watu ulijitokeza kumzika Ally Rashid mwanamuziki wa
siku nyingi ambaye alifariki jana mchana. Mazishi yalifanyika katika
makaburi ya Keko Machungwa kaburi lake likiwa jirani kabisa na la
mwanamuziki mwingine nguli Moshi William. Mazishi ya Mzee Alyy
yalifanyika muda wa saa nne asubuhi pia na kuhudhuriwa na wanamuziki
wengi wa zamani na hata wa sasa akiwemo Mchizi Mox ambaye alikuwa
kimwita marehemu baba yake mdogo.
MUNGU AMLAZE PEMA ALLY RASHID KWA PICHA INGIA HAPA
MUNGU AMLAZE PEMA ALLY RASHID KWA PICHA INGIA HAPA
Friday, October 10, 2014
MPIGA SAXAPHONE MKONGWE ALLY RASHID 'SABOSO' AFARIKI DUNIA
Mwanamuziki
wa zamani aliyekuwa mpiga saxaphone aliyejulikana pia kama Mzee Saboso,
Ally Rashid amefariki dunia leo mchana. Mzee Ally kwa mara ya mwisho
alikuwa bendi ya Msondo Ngoma. Wiki chache zilizopita mtandao wetu
ulifanya mahojiano marefu na Mzee Ally hivyo soma hapa historia ndefu ya
Mzee huyu. Mpaka muda huu ndugu zake hasa wa Zanzibar ambako ndio kwao
walikuwa hawajatoa taarifa ya taratibu za maziko. Mara tutakapopata
taarifa zaidi tutawataarifu.
Mungu Amlaze Pema peponi Mzee Ally Rashid
HISTORIA YA ALLY RASHID KHAMIS ‘SABOSO’ ISOME HAPA
Mungu Amlaze Pema peponi Mzee Ally Rashid
HISTORIA YA ALLY RASHID KHAMIS ‘SABOSO’ ISOME HAPA
Thursday, September 11, 2014
Saturday, August 30, 2014
IFAHAMU HISTORIA YA MAFUMU BILALI BOMBENGA =SUPER SAX
HAPA AKIPIGA TUMBA SIKU YA MKESHA WA MAZISHI YA REMMY ONGALA |
AKIWA NA MPULIZA SAX MWENZIE JOSEPH BERNARD |
Bombenga anakumbuka kuwa, wakati akiwa na African Stars ambayo hata jina lake alilibuni yeye, walitamba na vibao kama ‘Sakatu Sakatu’, ‘Mayanga’, ‘Maya’, ‘Afrika’ na ‘Dance Dance’.
Baadhi ya wanamuziki waliokuwa wakiunda kundi hilo la African Stars linalojulikana zaidi hivi sasa kama ‘Twanga Pepeta’, ni Bob Gady, Andy Swebe, Alfa Nyuki, Palmena Mahalu, Pamela pamoja na Kayumbu ‘Amigolas’.
“Historia yangu kimuziki, inaanzia mwaka 1972 nilipojiunga na bendi ya Morogoro Jazz, wakati huo nikitokea jeshini Makutupola,” anasema Bombenga.
Mwaka 1973 aliingia na Western Jazz alioshiriki nao kupiga Saxophone, kwenye vibao kadhaa vya bendi hiyo, vikiwamo ‘Hakika’, ‘Kazi ni Kazi’ na ‘Sadaka’, kabla ya mwaka 1978 kutimkia Dar International.
Pamoja na kupuliza kiustadi Saxophone pamoja na kuimba kwenye nyimbo kemkemu, zikiwamo ‘Mayasa’ na ‘Zuena’, lakini pia Bombenga alishiriki kucharaza gitaa la Solo katika kibao ‘Vick’.
Mwaka 1979 alibeba mabegi na kutua Vijana Jazz Band alikotunga kibao ‘Taabu’ na pia kushiriki kukiimba, huku kadhalika akipuliza Saxophone kwenye vibao kama ‘Chiku’ na ‘Matata Ndani ya Nyumba’.
Mwaka 1980 alihamia Maquis ambapo alitesa kwa kupuliza Saxophone kwenye vibao viiingi, baadhi yake ni ‘Zoa’, ‘Sina Ndugu’, ‘Noel’ pamoja na ‘Maige’.
“Nilikaa Maquis hadi mwaka 1984 nilipochomoka tena na kuhamia Bima Lee nilikokutana na wakali kama Jerry Nashon ‘Dudumizi’, Shaaban Dede ‘Super Motisha’, ‘Joseph Mulenga ‘Spoiller’,” anasema Bombenga.
Mwaka 1985 Bombenga alikuwa mwanzilishi wa bendi ya MK Group ‘Ngoma za Maghorofani’, kabla ya mwaka 1986 kuwa tena mmoja wa waanzilishi wa Tancut Almas ya Iringa.
Mwaka 1987 alirejea tena MK Group ambapo nyimbo yake ya kwanza kupuliza Saxophone awamu hii ya pili ilikuwa ni ‘Utakuja Kuanguka Kwenye Matope’.
Mwaka 1989, kaka yake Adam Kinguti alirudi nchini akitokea Sudan alipokuwa akifanyakazi kwenye ofisi za ubalozi, wakaanzisha Bicco Stars na yeye kushiriki kupuliza Saxophone kwenye vibao kadhaa kama vile; ‘Magret Mage’, ‘Wapangaji’ na Kisamvu’.
Mwaka 1991 alitoka Bicco akiwa na mpapasaji kinanda mahiri wa kike ambaye kwa sasa ni marehemu, Asia Daruweshi, baada ya kutokea hali ya kutoelewana kati yake na Kinguti, wakaanzisha Zanzibar Sound.
“Tukiwa na Zanzibar Sound, tulipata mkataba katika Hoteli ya Mount Meru, Arusha na mwaka mmoja baadaye mwanamuziki mwenzetu kwenye bendi hiyo, Kanku Kerry alipata mkataba Japan tukaondoka naye kwa sharti la sasa kujiita Kilimanjaro Connection,” anasema Bombenga.
Walizunguka nchi nyingi za bara la Asia wakiwa na Kilimanjaro Connection, waliporudi mwaka 1994 alijitoa na baadaye kidogo Asia naye alijitoa na kurudisha upya bendi yake ya Zanzibar Sound na kurejea mkataba wake Bahari Beach Hotel.
Bombenga wakati huu akabaki bila bendi, ambapo muda si muda Asia alipata kazi nchini Bahrain na kumuachia Bombenga mkataba wa Bahari Beach.
Baada ya kuona ameachiwa mkataba wakati hana bendi, Bombenga ndipo alipomfuata Baraka Msirwa na kumuomba vyombo vya muziki ambapo alimpa kwavile havikuwa na kazi kutokana na kufa kwa bendi za MK Group, MK Beat na MK Sound zilizokuwa zikivitumia.
“Hicho ndio kilikuwa chanzo cha bendi ya African Stars niliyoibuni mwenyewe hadi jina, iliyoniletea uhasama mkubwa na dada yangu Asha Baraka baada ya kujitoa,” anasema Bombenga.
Kwa upande wa warithi, Bombenga ana wanawe wawili wanaoonekana kufuata vema nyayo zake, ambao ni Feruzi (22) anayepapasa kinanda na Aziza (19) ambaye ni mwimbaji.
Bombenga mwenye miaka 40 katika muziki na aliyejifunza mengi kupitia sanaa hiyo, anavutiwa na waimbaji; Isha Mashauzi, Nasseeb Abdul ‘Diamond’, Flora Mbasha na Hassan Bitchuka.
Anatoa ushauri kwa wanamuziki wa Dansi kuketi na vyombo vya habari na kuzungumza, ili kuangalia namna ya kuurejesha kwenye chati muziki wao ambao umekuwa ukiporomoka kila uchao.
Mikakati ya baadaye ya Bombenga ni kustaafu muziki na kujihusisha na ujasiriamali, baada ya kwenda nchini Kinshasa na kufanya maonesho na baadhi ya mastaa wa huko.
“Mimi ni mtoto wa tano katika familia ya mzee Bilali Mafumu, niliyepata elimu yangu ya msingi katika shule ya H.H Agakhan, Kigoma nilikofaulu na kujiunga na shule ya sekondari Kazima, Tabora nilikosoma hadi kidato cha nne,” anasema Bombenga.
Baada ya kumaliza elimu ya sekondari, Bombenga aliyesoma shule moja ya sekondari na mbunge wa Tabora, Ismail Aden Rage, anasema kuwa 1972 alijiunga na JKT kwa mujibu wa sheria ya enzi hizo, alikojifunza kuimba na kupuliza Saxophone.
Anaishi Vingunguti, jijini Dar es Salaam na familia yake ambayo ni mkewe na watoto saba, huku akitamani kuongeza wake wengine hadi wawe watatu.
Friday, August 29, 2014
MFAHAMU MKONGWE WA SAXOPHONE RASHID PEMBE
RASHID PEMBE |
“TUKIO la kuutumikia Umoja wa Vijana kwa muda wa miaka 18 na kulipwa mafao ya sh. Mil 1.6, baada ya kustaafu, ndilo linalosumbua kichwa changu hadi leo, ambalo kiukweli sitakaa nikalisahau,” ndivyo anavyoanza kueleza Rashid Pembe.
Pembe ni kati ya wanamuziki nguli wa miondoko ya Dansi, aliyetokea mbali hadi sasa ambapo anaonekana amepata mafanikio kiasi kupitia sanaa hiyo.
Mwaka 2005 aliomba kustaafu kuitumikia bendi ya Vijana Jazz aliyokuwa nayo tangu Aprili, 1987, baada ya kuona imeanza kuyumba na kupoteza mwelekeo na kilichomkuta ndio hicho ambacho wakati fulani aliwahi kujutia kuwa mwanamuziki wa Dansi.
Kwa sasa Pembe anamiliki bendi yake binafsi, inayojulikana kama Mark Band, ambayo chanzo cha jina ‘MARK’ ni herufi moja moja za majina ya mwanzo ya wanamuziki wanne wanzilishi wa bendi hiyo.
Wanamuziki hao na nafasi zao kwenye mabano, ni pamoja na Mgazija (Bass), Alex (Solo), Rashid (Saxophone) na Karamazoo (Saxophone).
Mark Band iliasisiwa rasmi mwaka 2006, ambapo baada ya kuiunda, waliamua kuwaongeza wanamuziki wengine kama Said Majivu (Drums), Said Makelele (Tarumbeta) pamoja na Noel Minja na Balusi Kitembo ambao ni waimbaji.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Pembe anasema kuwa, kama ilivyo kwa bendi nyingine nyingi, walipoanzisha bendi hiyo walikumbana na changamoto kemkemu, ikiwa ni pamoja na kukodi vyombo kwa gharama kubwa.
“Hata hivyo, Mungu alitujalia kwani baadaye tulipata mkataba wa kutumbuiza siku tatu katika wiki, kwenye Hoteli ya See Criff, jijini Dar es Salaam, tukaanza kujipanga kwa ununuzi wa vyombo vyetu wenyewe,” anasema Pembe.
Anamtaja Waziri wa zamani wa Mambo ya Ndani, Mheshimiwa Mohammed Seif Khatibu kuwa ni kati ya watu waliochangia kuwakwamua ndani ya Mark Band kwa kuwaombea mkopo wa sh. Mil 3, kwenye Hoteli ya See Criff walioilipa polepole kwa kufanya shoo hapo.
Waliitumia pesa hiyo kwa kuchanganya na nyingine walizipata kupitia maonesho yao mengine na kununua vyombo kidogo kidogo hadi sasa wanapomiliki vyombo vyenye thamani zaidi ya sh. Mil 50.
Mwaka 2010 waliingia mkataba na Kampuni ya Kijerumani iitwayo ‘Mother Africa’ wa kutumbuiza nchi mbalimbali kama vile; Misri, Sweden, na nchi za Amerika ya Kusini kama vile Chile na Peru na pia Ufaransa pamoja na Ujerumani yenyewe.
“Tumekuwa na maisha ya namna hiyo kwa muda mrefu sasa, ya kutumbuiza nje, huku hapa nchini tukifanya shoo nyakati za likizo zetu tu,” anasema Pembe.
Pembe anasema, tayari kwa upande wa nyimbo, Mark Band imeshafyatua albamu nzima, ambapo ni kibao kimoja tu kiitwacho ‘Matukio’ ndicho walichokisambaza kwenye vituo mbalimbali vya radio na runinga hapa nchini.
Vibao vingine kwenye albamu hiyo waliyoirekodia katika Studio za Bakunde Production, jijini Dar es Salaam, ni ‘The Girl From Tanzania’, ‘Baba Kaleta Panya Remix’, ‘Amani’, ‘Anjela’ na ‘Pombe’.
Pembe anasema, mafanikio ndani ya Mark Band ni kumiliki vyombo vya thamani, kuwa na akaunti nono na kujulikana duniani kote, huku mafanikio kwa upande wake ikiwa ni kuwasomesha wanawe na kuanza kuwanunulia viwanja kila mmoja na chake.
Akielezea namna alivyojifunza muziki, Pembe anasema kuwa mwaka 1981 alijiunga na Jeshi la Polisi kama fundi ujenzi, baada ya kumaliza masomo yake ya Sekondari.
“Nikiwa Polisi, wakati najiandaa kupelekwa chuo cha ufundi, Marehemu Tx Moshi William aliyekuwa kwenye bendi ya jeshi hilo wakati huo, alinishauri kuachana na ufundi na kujiunga na kitengo cha Bendi,” anafahamisha Pembe.
Pembe anasema, Tx Moshi alimshauri hivyo kwasababu waliishi mtaa mmoja kabla hawajawa polisi, ambapo alikuwa akimuona namna alivyokuwa ‘mtundu’ kwenye gitaa la Solo.
Kiongozi wa polisi wakati huo, Mzee Mayagilo akamuombea Pembe uhamisho, lakini pia wakati anasubiri kwenda kuendelezwa ujuzi wa kupiga gitaa, mpigaji Saxophone wao, Abdul Mwalugembe akastaafu.
“Tukio hilo lilimfanya Mayagilo kunibadilisha na nikaanza kusomea upulizaji Saxophone, ambapo nilisoma nadharia mwezi mmoja na nusu na vitendo pia muda kama huo, nikawa fiti kabisa,” anasema Pembe.
Anasema kuwa, alirekodi nyimbo nyingi Polisi Jazz, baada ya zile zilizoambatana na ‘Mwaka wa Watoto’, ambazo hata hivyo hazikuchukua chati.
Mwaka 1987 alistaafu ligwaride akiwa askari mwenye cheo cha Koplo, kwa kununua mkataba, baada ya kuvunjika ghafla kwa ahadi aliyopewa na Jeshi, ya kupelekwa nchini Korea kuendelezwa kimasomo, kwa sababu alihisi ndoto zake za kufika mbali kielimu zilishagonga ukuta wa zege.
Akiwa na Vijana Jazz aliyojiunga nayo wakati imetoka kuipua vibao kama ‘Mari Maria’, ‘Ambha’ na ‘Bujumbura’, Pembe anasema kuwa, kibao chake cha kwanza kurekodi kilikuwa ni kile kinachokwenda kwa jina la ‘Miaka 10 ya Umoja wa Vijana’.
“Hadi nafungasha virago Vijana Jazz, niliyoitumikia na kushika nyadhifa mbalimbali za Kiuongozi, nilikuwa nimetunga vibao vinne ambavyo ni ‘Siri ya Ndani’, ‘Baba Sammy’, ‘Mwanamke Salo’ na ‘Dar es Salaam’,” anasema Pembe.
Pembe asiyependa kuona bendi haina maendeleo na ambaye katika muziki anawakubali King Enock na Elias Nyoni, anasema hajapata mafanikio wakati wa Vijana Jazz, zaidi ya kusafiri nchini Zambia pekee.
Kwa mtazamo wake, Pembe anaona biashara huria na udhamini katika vipindi, kwenye vituo mbalimbali vya radio na runinga ndivyo vinavyochangia kwa kiasi kikubwa kuliua Dansi.
Anasema mfumuko wa vituo vingi vya radio na runinga umefanya kuwapo na upendeleo binafsi kwa badhi ya mitindo ya muziki, huku mingine ikididimizwa kwa makusudi kwa manufaa ya watu wachache kama si mtu mmoja.
“Watoto wangu wanaoonekana kufuata kwa karibu zaidi nyayo zangu baba yao, ni Omary (21) ambaye yuko Kisiwani Zanzibar hivi sasa akijishughulisha na muziki wa Hoteli na Mwajuma (15), ambaye bado ni mwanafunzi wa darasa la saba,” anasema Pembe.
Tayari Pembe aliye mbioni kufungua chuo cha Saxophone, ameshawaambukiza wengi kipaji cha upulizaji chombo hicho, badhi yao wakiwa ni wanamuziki wa Dansi, Injili pamoja na miondoko mingine.
Aidha, badhi ya wasanii wa miondoko ya muziki wa Bongofleva waliomshirikisha kupuliza Saxophone kwenye vibao vyao, ni pamoja na Q Chillah, Kikosi cha Mizinga na Cindi katika nyimbo ya pamoja na Ommy Dimpoz.
Huyo ndiye Rashid Pembe, baba wa familia mwenye mke na watoto sita ambao ni Rehema, Pembe, Amina, Omary, Khalid na Mwajuma.
Alizaliwa mwaka 1957, Kisarawe Pwani na kupata elimu ya msingi katika shule nne tofauti ambazo ni Kisarawe, Vikindu, Sotele na Kisiju zote za mkoani Pwani, kuanzia mwaka 1966 hadi mwaka 1972
Subscribe to:
Posts (Atom)