Monday, November 23, 2015

MFAHAMU MBARAKA YUSUPH MWANAMUZIKI WA NATIONAL PANASONIC NA POWER IRANDA

“NIMEACHANA na muziki wa dansi hivi sasa na nimeamua kugeukia sanaa ya filamu, ambapo sababu kubwa ni kupungua kwa kasi yangu ya ucharazaji gitaa, kutokana na kupata mara mbili kwa nyakati tofauti, ugonjwa wa kupooza.”
Hayo ni maneno ya Mbaraka Yusuph, kati ya wacharazaji mahiri wa zamani wa magitaa yote pamoja na Saxophone, aliyewahi kuzitumikia bendi mbalimbali hapa nchini, zikiwamo, The Smashers, National Panasonic, OSS ‘Power Iranda’, Seven Blind Beats na the Big Africa ya Arusha..ENDELEA HUKU

Thursday, April 23, 2015

MWANAMUZIKI MKONGWE MUTOMBO LUFUNGULA AUDAX HATUNAE TENA

AUDAX(kushoto) akiwa na Kasongo Mpinda
Mwanamuziki muimbaji na mtunzi mashuhuri wa bendi ya Maquis Original Mutombo Lufungula Audax, amefariki dunia usiku wa kuamkia leo, huko Kimara Michungwani. Mwili wake umepelekwa kuhifadhiwa Mwananyamala Hospitali. Audax alikuwa ndie mmoja wa wanamuziki asili wa kundi la Maquis Du Zaire. Kundi la Maquis lilianza katika mji wa Kamina, jimbo la Shaba, huko Kongo. Awali kundi lilianza kwa kuitwa Super Teo, kisha kubadili jina na kuitwa Rocken, ......INAENDELEA

Tuesday, April 21, 2015

MWANAMUZIKI WA SIKU NYINGI PAUL GAMA AFARIKI DUNIA

KWA MASIKITIKO MAKUBWA TUMETAARIFIWA KUWA MWANAMUZIKI WA ZAMANI PAUL GAMA AMEFARIKI DUNIA HUKO DODOMA TAREHE 16.4.2015 MUDA WA SAA NNE ASUBUHI. NARUDIA MAKALA HII YA HISTORIA YA PAUL GAMA KADRI ALIVYOTUELEZA MWENYEWE

Paul Daniel Gama
Paul Daniel Gama alizaliwa Barabara ya 11 Dodoma (1947). Baba yake alikuwa ni mwanajeshi wa KAR mwenye asili ya Songea na mama yake alikuwa na asili ya Usangu alikuwa anafanya kazi  katika 
Spokes Mashiyane na filimbi yake
hospitali ya Mirembe ambayo wakati huo ilikuwa ni hospitali kubwa ya majeruhi wa vita ya pili ya dunia. Aliingia shule na alipofika darasa la nne alijikuta akiwa na kipaji kukubwa cha kupiga filimbi, wakati huo wapiga filimbi walipenda sana kumuiga mpiga filimbi maarufu kutoka Africa ya Kusini Spokes Mashiyane. Akiwa na wenzie walianzisha kikundi ambacho kilikuwa na maskani eneo la Mji Mpya pale Dodoma. Vijana hao pia walikuwa wakiiga  nyimbo za wanamuziki maarufu wa wakati huo, kama Salum Abdallah na  Cuban Marimba, pia Salum Zahor na Kiko Kids. Katika kufanya fani yao hiyo kama kitu cha kujipa burudani waliligusa sikio la  aliyekuwa mwalimu wa Elimu ya Watu Wazima katika Community Center ya pale Dodoma. Mwalimu huyu aliwasaidia kuwaazimia amplifaya moja kutoka kwenye bendi nyingine ilikuweko Dodoma wakati huo, The Jolly Sextet Band. Band iliyokuwa ikimilikiwa na Mkenya mmoja ambaye alifika Dodoma kama mfanya kazi wa East African Postal and Telecommunication Services, huyu bwana alikuja na vyombo vingi akaanzisha bendi ambayo mmoja wa wapigaji wake alikuwa Mzee Mnenge ambaye hatimaye alitua NUTA Jazz Band.
Bongos
Hiki kikundi cha Gama na wenzie kilikuwa katika mfumo wa Jazz Band za zamani ambapo walikuwa na ngoma na filimbi tu,ikisindikizwa na kuimba, lakini waliweza kukonga nyoyo hata za wanamuziki wengine, na Gama akawa anasakwa na bendi kubwa iliyokuweko wakati ule Central Jazz band. Alipomaliza darasa la saba tu ndugu yake aliyeitwa Titus Olaf Gama alimshawishi aingie Central Jazz lakini hakuwa tena mpiga filimbi bali mpiga Bongos, fani aliyoiweza sana hata  kuipenda na hasa baada ya kuwaona wanamuziki wa NUTA akiwemo Muhidin Gurumo  ambaye wakati huo alikuwa akipiga Bongos na kuimba. Bongos no ngoma ndogo zilizokuwa muhimu katika kundi wakati huo ambapo hakukuweko na drums wala tumba. Taratibu akaanza kupata hamu ya kupiga bass, wanamuziki wenzie walimkatisha sana tamaa kwa kuambiwa kuwa vidole vyake vilifaa sana kwa kupiga bongos na si kupiga gitaa.

Katika jitihada zake za kujifunza gitaa la bezi alikuwa kila mara akiwahi mazoezi na kujaribu kujifunza gitaa la bezi. Hilo lilikuwa gumu mpaka pale bendi  ya Lake Jazz Band ilipotembelea Dodoma. Bendi hiyo wakati huo ikiwa na wanamuziki kama Shem Karenga  akiwa anapiga gitaa la bezi, Mzee alum ambaye alikuwa na ulemavu wa macho, mwanzo alikuwa akipiga gitaa la solo na baadae akahamia kupiga gitaa la rhythm wakati gitaa solo lilikuja kupigwa na jamaa aliyeitwa Kally. Kutokana na simulizi ni wazi kuwa wanamuziki wa kutoka Burundi walikuwa wengi sana nchini wakati huo. Pia katika bendi hiyo alikuweko Mzee Juma Kitambi, mtunzi wa wimbo maarufu wa Rangi ya Chungwa.
Gama alichukua nafasi hii kumfuata Mzee Salum ili aweze kumfundisha gitaa. Kwa kuwa wanamuziki wengine walikuwa wakitoka kwenda kutembea Mzee Salum alibaki nyumbani na hivyo Gama alichukua nafasi hiyo kumnunulia sigara Mzee Salum ana kumsihi amfundishe gitaa nae alifanya hivyo na Gama akatokea kuwa mpiga bezi mahiri.
Katika kipindi hiki akatokea mfanya biashara Mohamed Omar Badwel, huyu alikuwa na gereji na studio ya kupiga picha, aliweza kwenda Mombasa na kurudi na seti ya vyombo na kuanzisha Dodoma Jazz Band. Gama akahama Central Jazz Band na kujiunga na wanamuziki wengine walioanzisha Dodoma Jazz. Band ilianza ikiwa na mpiga solo Hassan Mursali mwanamuziki mweny asili ya Malawi, siku hizo ikiitwa Nyasaland alikuwa ndie mpiga solo, lakini aliwaacha baadae na kujiunga na NUTA Jazz Band, upigaji wake wa solo unaweza kuusikia katika kusikiliza kibao kimoja maarufu cha NUTA, kilichoitwa Dunia Njema Kukaa Wawili.
Hasan alikuwa mtu wa kuhama hama hatimae alipoteza uwezo wa kusikia jambo ambalo lilihusishwa na kuhamham kwake kwani ushirikina ulitawala sana wakati huo, kama maelezo yanayofuata yanavyoonyesha. Dodoma Jazz ilikuwa pia inafanya ziara katika sehemu nyingi , kama vile Iringa, Mbeya ,Tabora, Dar es Salaam na kadhalika, lakini safari moja ya kwenda Kilosa ilifanyika ikiwa na lengo la kumfuata Abel Barthazal aliyekuwa akipiga katika bendi ya Kilosa Jazz. Bendi  ilipokelewa vizuri na wakafanya maonyesho yao Kilosa na hatimae kuondoka na Abel. Siku chache baade wakati huo Mzee  Mohamed Omar, mwenye bendi alikuwa kasha mnunulia suti kadhaa Abel, ukaja ugeni toka Kilosa wakiwa na barua yenye maelezo kuwa ikiwa Abel Hatarudi Kilosa, mmoja wa wanamuziki wa Dodoma Jazz atafariki, na barua hii ililetwa kwa mkono na mjumbe ambae alisisitiza wakishaisoma mbele yake ndio anaondoka. Abel alirudishwa Kilosa mara moja.
Baada ya hapo aliyekuwa meneja wa bendi Ramadhan Waziri alitumwa Burundi kwenda kutafuta wapigaji, siku alipokuwa anarudi na wapigaji wapya akakutana kwenye treni na Rashid Hanzuruni, mpiga solo mahiri sana ambaye upigaji wake husikika katika wimbo  Napenda nipate lau nafasi
Hanzuruni alikuwa kaiacha Tabora Jazz baada ya  kutokea ugomvi mkubwa ambapo alipoteza meno kadhaa, hivyo alikuwa kwenye hilo treni akielekea Dar es Salaam kumfuata mpigaji mwenzie Samba ambae alikuwa NUTA Jazz. Ramadhani aliweza kumshawishi hanzuruni akabaki Dodoma Jazz ambako alikaa kwa muda na hatimae akaja kuchukuliwa na Sama ili aingie NUTA Jazz, ndoto hiyo haikufanikiwa kwana NUTA alikuweko mpigaji mahiri  Hamisi Franco, hii ndiyo ilipelekea Hanzuruni kwenda Western Jazz Band



Friday, January 16, 2015

IMETIMIA MIAKA 36 TOKA KIFO CHA MBARAKA MWINSHEHE, MUZIKI WAKE BADO UKO HEWANI

Mbaraka Mwinshehe Mwaruka alizaliwa mjini Morogoro Juni 27, 1944. Siku ya Januari 12, 1979 ulimwengu wa muziki Tanzania ulitikiska kwa simanzi baada ya kusikika kifo cha mwanamuziki huyo, mpiga gitaa muimbaji, mtunzi na kiongozi wa bendi wa miaka mingi na ambaye bendi yake ilikuwa imepiga karibu kila wilaya ya nchi hii. Taarifa ziliingia jioni ya siku ile kupitia redio ya Taifa kuwa nguli huyu alifia katika hospitali katika jiji la Mombasa nchini Kenya muda wa saa 1:55 jioni kufuatia ajali ya gari...........ENDELEA HUKU

Tuesday, December 16, 2014

HATIMAE SHEM IBRAHIM KARENGA AZIKWA

HATIMAE  mwanamuziki mkongwe mpiga gitaa muimbaji na mtunzi mahiri Shem Ibrahim Karenga amezikwa katika makaburi  ya Kisutu jioni ya leo. Shughuli hiyo ilianza kwa utata baada ya kuwa makaburini hapo kulikuwa na misiba minne hivyo kila lilipokuja jeneza wanamuziki, ndugu na wapenzi wa muziki walijikuta wakisindikiza jeneza na..........INAENDELEA HUKU

Monday, December 15, 2014

BURIANI SHEM IBRAHIM KARENGA

LEO Jumatatu tarehe 15 Desemba 2014, majira ya saa nne asubuhi taarifa zilianza kusambaa kuwa mwamba mwingine wa muziki wa dansi Tanzania umedondoka. Mzee Shem Karenga hatunae tena,kwa vyovyote waliohudhuria dansi alilopiga Ijumaa na Jumamosi iliyopita pale Mwembeyanga watakuwa hawaamini, lakini imekuwa mapenzi ya Mungu, kwamba asubuhi ya leo aliamka hajisikii vizuri na alipelekwa hospitali ya Amana lakini hakukuweza kufanyika kitu Mzee akarudi kwa Muumba wake. Mungu aipokee roho yake. Miezi michache iliyopita tulipata muda mrefu wa kuongea na Mzee Shem Karenga ili kujua alikotokea na mawazo yake kwa sasa mazungumzo yalikuwa kama ifuatavyo;................................. ENDELEA HUKU

Monday, November 10, 2014

LEO NIMEKUMBUKA KIBAO MASAFA MAREFU CHA TANCUT ALMASI...angalia video


Kasaloo Kyanga ndie mtunzi wa kibao hiki maarufu, kilirekodiwa RTD Dar es Salaam katika awamu ya pili ya recording za Tancut Almasi. Recording hii ilitaka kuvunja bendi kwa kuwa wakati bendi ikiwa studio, Said Mabela alipita studio na Katibu wa bendi akamuuliza kwa siri anausikiaje muziki? Sijui kwa sababu gani lakini Mabela alijibu, "Hapa hakuna kitu nasikia solo tupu". Katibu wa bendi ambaye pia wakati huo alikuwa Katibu wa tawi la JUWATA la Tancut, akatujia juu wanamuziki wa Tancut kuwa tunapiga solo tupu na hivyo tuache kurekodi na bendi irudi Iringa kwa mazoezi zaidi. Ulikuwa ugomvi mkubwa, wakati huo Mabela amekwisha ondoka hata kumuuliza alikuwa ana maana gani haikuwezekana. Fundi wa RTD James Muhilu ndie aliyemtuliza Katibu huyo kwa kumueleza kuwa nae haelewi maana ya maneno ya Mabela na recording ikaendelea na dunia ikapata bahati ya kusikia kibao hiki. Nakumbuka katika awamu ya kwanza ya kurekodi Sidi Morris alikuja studio na kupiga tumba katika vibao kadhaa kikiwemo Wifi utunzi wa mwenye blog hii John Kitime. Hili lilileta mzozo Maquis ambako Sidi alikuwa akifanyia kazi na hivyo akasimamishwa bendi kwa kushiriki kurekodi

Saturday, November 8, 2014

HISTORIA FUPI YA TAARAB

Taarab ina historia ndefu katika muziki wa Tanzania kama ulivyokuwa muziki wa dansi. Wapenzi wa taarbu wa zamani waliiweka taarabu katika vyanzo kama Taarab ya Tanga, Taarab ya Dar es Salaam,Taarab ya Zanzibar na Taarab ya Mombasa. Taarab ya Zanzibar wakati huo........INAENDELEA HUKU

Wednesday, October 22, 2014

MIAKA KUMI YA KUMBUKUMBU YA KIFO CHA NDALA KASHEBA

ndala-kasheba_2255445LEO tunatimiza miaka kumi toka kifo cha mwanamuziki mahiri Freddy Supreme au maarufu kama Ndala Kasheba. Freddy alianza kufundishwa gitaa na baba yake wakati akiwa na umri wa miaka 12. Baba yake alijua kupiga gitaa japo hakufanya kazi ya uanamuziki, alikuwa akipiga gitaa nyumbani baada ya saa za kazi. Moja ya bendi maarufu ambazo zilimtambulisha sana Fredd ilikuwa Orchestra Fauvette, Freddy alieleza kuwa bendi ya Orchestra Fauvette ilianza tarehe 7 mwezi wa sita mwaka 1964 katika jiji la Lubumbashi huko Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo. Jina hilo Fauvette........ENDELEA HUKU

Saturday, October 11, 2014

ALLY RASHID AZIKWA KEKO

Umati mkubwa wa watu ulijitokeza kumzika Ally Rashid mwanamuziki wa siku nyingi ambaye alifariki jana mchana. Mazishi yalifanyika katika makaburi ya Keko Machungwa  kaburi lake likiwa jirani kabisa na la mwanamuziki mwingine nguli Moshi William. Mazishi ya Mzee Alyy yalifanyika muda wa saa nne asubuhi pia na kuhudhuriwa na wanamuziki wengi wa zamani na hata wa sasa akiwemo Mchizi Mox ambaye alikuwa kimwita marehemu baba yake mdogo.
MUNGU AMLAZE PEMA ALLY RASHID KWA PICHA INGIA HAPA

Friday, October 10, 2014

MPIGA SAXAPHONE MKONGWE ALLY RASHID 'SABOSO' AFARIKI DUNIA

Mwanamuziki wa zamani aliyekuwa mpiga saxaphone aliyejulikana pia kama Mzee Saboso, Ally Rashid amefariki dunia leo mchana. Mzee Ally kwa mara ya mwisho alikuwa bendi ya Msondo Ngoma. Wiki chache zilizopita mtandao wetu ulifanya mahojiano marefu na Mzee Ally hivyo soma hapa historia ndefu ya Mzee huyu. Mpaka muda huu ndugu zake hasa wa Zanzibar ambako ndio kwao walikuwa hawajatoa taarifa ya taratibu za maziko. Mara tutakapopata taarifa zaidi tutawataarifu.
Mungu Amlaze Pema peponi Mzee Ally Rashid


   HISTORIA YA ALLY RASHID KHAMIS ‘SABOSO’ ISOME HAPA

Thursday, September 11, 2014