HALILA TONGOLANGA, mwanamuziki wa siku nyingi ambaye alikuwa amelazwa katika hospitali ya Muhimbili amefariki dunia usiku wa kuamkia leo. Halila alikuwa amesafirishwa kutokea Ndanda kuja Muhimbili akihisiwa kuwa na matatizo ya figo. Licha ya kuwa alifika Muhimbili juzi Ijumaa usiku, lakini alikuwa hakufanyiwa vipimo vyovyote vikubwa mpaka umauti unamkuta. Jana Jumapili ililazimika kuanza kufanya jitihada za kupata daktari ambaye angemshughulikia kwa karibu zaidi, na daktari alipatikana ambaye aliahidi angeanza kufwatilia swala lake leo asubuhi lakini mapenzi ya Mungu yalikuwa tofauti. Juzi nilipomuona alinambia kuwa ana mengi anataka kunambia, lakini moja aliloweza kunambia pale ni kuwa yeye anajihisi ana kansa, 'Nilimuuliza anajuaje hilo, kwa vile hajapimwa hakuwa na jibu"
Wengi tutamkumbuka Tongolanga kwa wimbo wake wa Kimakonde aliouimba kwa mara ya kwanza akiwa na Les Mwenge 'Kila Munu Ave Na Kwao"
Mwili wa marehemu unategemewa kusafirishwa leo saa tano kuelekea kwao Newala. Habari zaidi zitawafikia kupia hapa
Mungu amlaze Pema peponi Halila Tongolanga
Monday, June 5, 2017
Saturday, June 3, 2017
TONGOLANGA ANASUBIRI VIPIMO
Katibu Mtendaji wa BASATA mwenye kitenge akiwa na Rais wa Shirikisho la Sanaa za Ufundi, walipomtembelea Tongolanga asubuhi ya leo. |
Halila Tongolanga kwa kweli anaumwa. Kwa maelezo ya mdogo wake, ni mwezi wa tatu sasa anaingia na kutoka hospitali mbalimbali. Mpaka jana alikuwa katika hospitali ya Ndanda, na kwa msaada wa Mbunge wa Tandahimba aliweza kupatiwa Ambulance na kufikishwa Muhimbili ambako amelazwa Kibasila No 10. Mpaka jioni ya leo alikuwa anasubiri vipimo.
Tongolanga ndie mtunzi na mwimbaji wa wimbo maarufu wa 'Kilamunu ave na kwao' aliouimba kwanza akiwa Les Mwenge bendi iliyo mali ya JWTZ.
Tongolanga ndie mtunzi na mwimbaji wa wimbo maarufu wa 'Kilamunu ave na kwao' aliouimba kwanza akiwa Les Mwenge bendi iliyo mali ya JWTZ.
Friday, April 28, 2017
SI KWELI KUWA HARRISON SATCHMO SIWALE ALIFIA GEREZANI,
Mar. Harrison Siwale-Satchmo |
......................
SIKILIZA HAPA GUITAR LA MZEE SIWALE...................
Tarehe 8 September 2013, niliandika katika blog hii habari niliyoipa kichwa cha habari, Harrison Siwale aliishia wapi? Ni habari ya kusikitisha.
Tarehe 8 September 2013, niliandika katika blog hii habari niliyoipa kichwa cha habari, Harrison Siwale aliishia wapi? Ni habari ya kusikitisha.
Niliandika hivi-----Nimetoka
kuongea na Mzee mmoja ambaye nilimuomba anitafutie habari za Harrison
Siwale aka ‘Satchmo’, ambaye alikuwa
mpiga rhythm mahiri na maarufu sana katika miaka ya sabini, Harrison alikuwa na
staili ya pekee ya upigaji wa gitaa wa kudokoa nyuzi na kupata aina ya pekee ya
mlio wa gitaa. Kati ya nyimbo ambazo upigaji huu unasikika ni katika nyimbo za
Jamhuri Jazz Band kama vile Mganga 1
na 2, Blandina na kadhalika. Pamoja na bendi nyingine Harisson aliwahi
kupigia Atomic na Jamhuri Jazz Band zote za Tanga, na kisha kuvuka mpaka na
kuwa na makazi Mombasa kwa muda mrefu ambako aliendelea na muziki. Kwa kadri ya
maelezo niliyopewa leo na huyu Mzee niliyemuomba anitafutie habari ili nijue yu
wapi huyu mwanamuziki siku hizi? Haya ndio aliyonambia.
'Baada
ya kufa kwa yale makundi ya Simba wa Nyika na Les Wanyika, Harrison Siwale
alianza kupiga muziki wa Injili katika eneo la Kilifi. Akawemo katika kundi
lililokuwa likifanya maonyesho yake katika miji mingi ikiwemo Mombasa na
Nairobi. Umahiri wake wa kazi ukamfanya mwenye vyombo vya hilo kundi
alilokuwemo Harrison kumuamini sana na kumuachia awe kiongozi wa kundi hilo na
kuwa huru kuzunguka sehemu mbalimbali. Inasemekana Harrison akapata tamaa ya
kuingia mitini na vyombo vile, hivyo ghafla akapotea. Taarifa zikamfikia mwenye
vyombo kuwa vyombo vyake viko njiani kuvushwa kungia Tanzania kupitia mji wa
Lungalunga. Mwenye vyombo akaweka mtego hapo na Harrison akakamatwa hapo akiwa
na vyombo hivyo, kesi ilifika mahakamani na akahukumiwa kifungo cha miaka
mitatu'. Baada ya hapa kuna hadithi mbili, moja ikisema alifia gerezani Shimo la
Tewa, na nyingine ikisema alifariki baada ya kumaliza kifungo chake.
Je,
nini hasa kilitokea? Najaribu kuwasiliana na watu mbalimbali kupata hadithi
zaidi kuhusu mwanamuziki huyu.
HATIMAE (2017 APRIL).... Kwa bahati sana nimeweza
kuanza kuwasiliana na mtoto wa Harrison Satchmo Siwale, ambae tuliweza
kukutana kupitia facebook. Kijana huyu ambaye jina lake ni Salehe Siwale aliweza
kunambia kuwa baba yake alimuoa mama yao na walizaliwa vijana wawili yeye na
kaka yake.
Na
niliweza kupata taarifa za ziada baada ya kuniunganisha na mama yake ambaye
ndie alikuwa mke wa Mzee Siwale nikaweza kuongea nae mubashara kupitia video call ya whatsapp. Kwanza kabisa mama huyo ansema kuwa katika
kipindi alichoishi na Mzee Siwale hakuwahi kufungwa wala kuzungumzia kuwa
aliwahi kufungwa. Na Mzee Siwale alifariki katika Kitongoji cha Rongai huko Nakuru na kuzikwa tarehe
31/3/2013. Ukiangalia kuwa taarifa ya awali niliyopewa ilikuwa katika miezi michache baada ya kifo chake, niwazi si kweli kuwa alifia Gerezani na kama angekuwa aliwahi kufungwa hakika
mkewe angekuwa anajua.
Mungu
Amlaze Pema Mchungaji Harrison ‘Satchmo’ Siwale
Saturday, April 22, 2017
KIFO CHA SOKOINE KILIIKUTA ORCHESTRA MAMBO BADO IKO SHINYANGA
Mwaka 1984 nilikuwa mwanamuziki wa bendi ya
Orchestra Mambo Bado, bendi iliyokuwa inaongozwa na Tchimanga Kalala Assossa.
Bendi ilikuwa ni moja ya bendi zilizokuwa pendwa wakati huo, mtindo wa bendi
ulikuwa unajulikana kama Bomoa. Neno hili lilitokana na wimbo wa Bomoa
Tutajenga Kesho, wimbo ambao baadae
kwa sababu ambazo mpaka leo sizijui, ulikuja kupigwa marufuku na Umoja wa
Vijana wa Mkoa wa Dar es Salaam wakati ule, usisike kwenye radio ya Taifa,
redio ambao ilikuwa pekee wakati huo. Orchestra Mambo Bado ilikuwa na watu
ishirini hivi, Tchimanga Assossa kiongozi na mwimbaji. George Mzee muimbaji,
Lucas Faustin muimbaji, Jenipher Ndesile muimbaji, Banza Tax muimbaji, Athumani
Cholilo muimbaji, John Kitime muimbaji, Likisi Matola mpiga gitaa la bezi, Andre
Milongo akipiga gitaa la second solo, Huluka Uvuruge na Kazembe wa Kazembe
wapiga gitaa la solo, William Maselenge akiwa kwenye gitaa la rhythm.
Kulikuweko na wacheza show wanne, mafundi mitambo watatu na mweka hazina mmoja
na meneja wa bendi. Masikani ya bendi yalikuwa katika ukumbi wa Lango la Chuma,
Mabibo Dar es Salaam
Tarehe 12 April 1984, kundi zima lilitua katika mji
wa Shinyanga baada ya kuwasili hapo kwa treni kutokea Dar es Salaam. Kwa
taratibu za miaka hiyo, pamoja na ratiba ya ziara ya bendi kutangazwa kwenye
gazeti la Uhuru, meneja wa bendi alikuwa akilazimika kutangulia mji ambao dansi
litapigwa kuwahi kufanya mikataba na kumbi ambazo dansi lingepigwa na pia kufuatilia vibali mbalimbali
vya kuruhusu onyesho kufanyika. Mawasiliano yalikuwa magumu na urasimu ulikuwa
mkubwa. Haikuwa kazi rahisi maana miaka hiyo ili bendi isafiri ililazimika
kupata kibali cha Afisa Utamaduni
wa Mkoa ambao ni masikani ya bendi kuruhusu bendi kutoka nje ya Mkoa na kisha
kibali hicho kupelekwa kwa Ofisa Utamaduni wa Mkoa ambao bendi inakwenda, nae
baada ya kuruhusu bendi kuingia mkoani kwake, unaomba kibali cha Afisa Utamaduni
wa Wilaya unakotaka kupiga muziki ili nae akuruhusu kufanya onyesho kwenye
wilaya yake. Baada ya hapo meneja hutafuta na mtu ambaye ana spika ya mkononi,
megaphone kuikodisha na kisha kutafuta mtu wa kutangaza onyesho. Ili kubana
matumizi kuna mara nyingine wanamuziki wenyewe ililazimika wapite mtaani na
spika hiyo kujitangaza. Kulikuwa na mji kama Mpanda wakati huo, ambapo
mtangazaji hakuwa na megaphone, mtu maalumu alipita mtaa kwa mtaa akiwa na
ngoma ambao aliipiga watu wakikusanyika basi anatangaza ujio wa bendi katika
mji wao.
Tarehe 12 April 1984, Orchestra Mambo Bado iliwasili
Shinyanga kwa treni ikitokea Dar es Salaam, kuanza ziara ya Kanda ya Ziwa.
Wanamuziki tulionyeshwa vyumba vya kulala, mambo yalionekana kuwa yatakuwa
mazuri kwa siku ile, matangazo yalikuwa yamebandikwa kwenye nguzo za umeme
sehemu mbalimbali za mji, na hali ya kuonyesha kuwa watu walikuwa na taarifa ya
ujio wetu ilikuwa dhahiri. Ilikuwa ni muda wa saa kumi hivi ilipotangazwa kuwa
nchi imepata msiba mkubwa sana. Waziri Mkuu Edward Moringe Sokoine amefariki
katika ajali ya gari jirani na Morogoro. Kwanza ilikuwa ni mshtuko, halafu
akili ilipotulia tulijua kuwa na sisi kama bendi tunaingia kwenye tatizo kubwa
sana, tulikuwa na nauli ya kuja tu mpaka Shinyanga, na fedha ya kula ya siku
moja tulikuwa tunategemea kupiga dansi ili kuweza kulipa malazi ya siku hiyo na
kupata fedha ya kula na kuendelea na safari kesho yake, tukitegemea mapato
mengine makubwa katika maonyesho ya Mwanza wikiendi iliyokuwa inafuata. Hayo
yote tulijua sasa yameharibika, tulirudisha vyumba vyote mara moja na kubaki na
viwili tu kimoja kikiwa cha wasichana waliokuwa kwenye bendi, wengine wote
ikalazimu tuhamishie mizigo yetu chumba kingine. Baadae tulikaa na Afisa
Utamaduni kutafakari kama dansi lingeweza kulia siku ile, na kama halitalia
nini hatima ya watu hawa 20 wageni kutoka Dar es Salaam? Kama kiasi cha saa
moja jioni, Afisa Utamaduni akaruhusu tupige dansi ili tuweze kupata nauli ya
kurudi Dar es Salaam, kwani ilijulikana wazi kitaanza kipindi cha maombolezo
ambacho hakuna mtu alijua kitaisha lini,
hivyo hakukuwa na sababu ya kuendelea na safari kutoka hapo. Vipindi vya
maombolezo huwa ni vipindi ambavyo pamoja na mambo mengine shughuli za muziki
husimamishwa. Kwa wanamuziki na wale wanaotegemea shughuli za muziki na familia
zao, kipindi hiki huwa kigumu sana. Lakini kinaleta ukakasi akilini kwani shughuli
za kupiga muziki kwenye kumbi husimamishwa, madisco hufungwa na vikundi vya
muziki haviruhusiwi kufanya kazi
lakini radio huendelea kupiga muziki uleule ambao umezuiwa kwenye kumbi, sehemu
za starehe kama baa huendelea kupiga muziki na kufanya biashara zao bila tatizo
ila wanamuziki ndio huzuiwa kufanya shughuli zao kwa maelezo kuwa ni kipindi
cha maombolezo. Nakumbuka sana misiba
mikubwa ya viongozi wetu ukiwemo wa Baba wa Taifa kwa sababu kubwa
mbili, kwanza uchungu wa kupoteza kiongozi wetu na njaa iliyofuatia baada ya
hapo.
Saturday, March 18, 2017
AMRI BILA TAFITI ZINAATHIRI SANA SEKTA YA MUZIKI
KATIKA
shughuli ambazo watu wengi huona ni rahisi kuendesha na kutoa maamuzi bila
utafiti ni soka na muziki. Ukisikiliza mazungumzo baada ya mechi za soka ndipo
utakaposikia watu wanavyotoa ushauri au kukosoa wachezaji, kocha refa, chama
cha mpira wa miguu, hakika ingewezekana watu hawa wakapata mamlaka, maamuzi
yangekuwa ya ajabu sana.
Hali
kadhalika kwenye muziki. Kwa mfano ukiuliza, kwanini muziki
wa bendi hauna umaarufu kama zamani? Hakika ukipita kila mtaa utapata majibu, wengine
watakwambia kosa la vyombo vya utangazaji , wengine watakwambia wanamuziki
wenyewe , wengine watakwambia serikali, na pia utapewa maelekezo mbalimbali ya
nini kifanyike. Bahati nzuri majibu haya ya mtaani hayana madhara kwani huishia
hapo hapo. Lakini bahati mbaya huja pale ambapo viongozi wenye mamlaka nao hugeuka
wataalamu wa muziki na wao kutoa maamuzi kadri ya mtizamo wao, lakini maamuzi
yao huwa amri, na amri inapotolewa bila utafiti wa kutosha madhara yake
yanaweza kuendelea miaka mingi baadae. Ninaloweza kusema kwa uhakika, ni kuwa
muziki wa Tanzania leo ungekuwa katika nafasi ya juu zaidi duniani kama
isingekuwa maamuzi ambayo yalitolewa bila utafiti miaka ya nyuma. Labda nitoe
mifano kadhaa. Mpaka miaka ya 70, wanamuziki wa Tanzania walikuwa wakienda
sambamba na wanamuziki wa nchi nyingine nyingi Afrika, licha ya kutokuwa na
miundo mbinu muhimu katika maendeleo ya muziki kama vile kutokuwa na kampuni za
kurekodi na kutengeneza santuri. Lakini kimuziki, wanamuziki wa kipindi hiki walikuwa
bega kwa bega na wenzao ambao walikuwa na miundo mbinu stahiki. Tanzania tulikuwa
na bendi ambazo zilikuwa zinapiga
muziki wa rumba, nyimbo nyingi za wakati huo mpaka leo bado zinasifika na
kupendwa katika anga za muziki. Pia tulikuwa na wanamuziki vijana ambao wengi wao walikuwa mashuleni,
hawa wakiwa na mtizamo mpana zaidi wa kutambulika duniani, wanamuziki hawa kama
ilivyokuwa sehemu nyingi Afrika walianza kupiga muziki uliojulikana kama Afro
Rock, muziki ambao ulichanganya mahadhi ya muziki asili wa Kitanzania na mapigo
ya kizungu, wakifuatia nyayo za kundi la Osibisa, na wanamuziki kama Ransome
Fela Kuti. Kukawa na makundi kama Afro 70, Trippers, Sun Burst, The Jets na
kadhalika kwa kuyataja machache, makundi ambayo yalianza kuingiza muziki wa
Tanzania kwenye soko kubwa zaidi la Kimataifa, kwa mfano wimbo wa Weekend wa
Afro70 uliingia kwenye Top Ten Nigeria miaka hiyo, wakati huo muziki wa Nigeria
haukuwa na umaarufu wowote nchini kwetu.
Kwa kuwa vijana hawa wengi walikuwa bado shuleni, na kufuatana na
maadili ya wakati ule, wanafunzi hawakuruhusiwa kushiriki madansa ya usiku, hivyo basi kulikuweko na
utamaduni wa madansa ya mchana yaliyoitwa Bugi. Hapo vijana walikusanyika
kupiga muziki wao kila mwisho wa wiki, shughuli zikianza saa nane mchana na
kuisha saa kumi na mbili jioni. Lakini siku moja kiongozi mmoja akatokea na
kupiga marufuku Bugi, hivyo kuwaondoa wanamuziki vijana wengi kwenye muziki kwani
wasingeruhusiwa kushiriki madansi ya usiku. Wakati vijana hao wanaacha muziki, vijana wengine Afrika
waliendelea mbele. Hata majirani zetu Kenya na Zambia wakawa na wanamuziki
wengi walioweza kuingia katika soko la Kimataifa, wanamuziki wetu walikosa
fursa hiyo. Pengo hili linaendelea kuwepo mpaka leo. Kuziba pengo hilo
kunahitaji kutafiti tulipojikwaa na kuangalia tunafanya nini kurekebisha hali
iliyopo. Swala la kupiga marufuku kazi za muziki si jambo geni katika historia
ya muziki, kulikuwa na maamuzi kadhaa ya kisiasa pia ambayo pia hayakuwa na
utafiti hivyo kudhoofisha maendeleo ya muziki Tanzania. Kwa mfano kulishawahi
kutolewa amri ya kupiga marufuku wacheza show, wakati huo karibu bendi zote
kubwa za muziki wa rumba kote Afrika Mashariki na Kati zilihakikisha kuwa
zinakuwa na kundi la wacheza show, na waimbaji maarufu kama Mbilia Bel na
Tshala Mwana wote awali walikuwa ni wacheza show. Kwa kipindi kirefu kulikuweko
na sinto fahamu ya wacheza show na ikalazimika taaluma hiyo irudi kinyemela
kwani makundi yote ya muziki kutoka nje yalipokuja nchini yalisindikizana na
wacheza show. Nyimbo kadhaa ziliwahi kupigwa marufuku na hatimae kuja kuonekana
ni za muhimu katika jamii, ukiwemo wimbo maarufu wa Super Matimila, Mambo kwa
Soksi, ambao ulipigwa marufuku na baade kuonekana ni wimbo muhimu kuhamasisha
watu kutumia kinga katika zama hizi za balaa la Ukimwi. Upigaji marufuku wa
tungo unakwaza watunzi na kuishia kutunga nyimbo nyepesi ambazo zina uhakika wa
kutokupigwa marufuku. Katika miaka ya karibuni kumewahi kufanyika maamuzi
kadhaa yasiyokuwa na utafiti kwa mfano, serikali iliwahi kununua mashine iliyoitwa Mastering Mixer
kwa gharama ya shilingi milioni 50, kwa maelezo kuwa ndio itakayowezesha
kumaliza wizi wa kazi za muziki. Sio siri wizi uko palepale. Hayo yalikuwa
maamuzi bila utafiti, ni vizuri kujua hiyo ‘mixer’ iko wapi ili kutathmini ni matokeo ya uamuzi huu
uliogharimiwa na serikali. Uamuzi mwingine ulikuwa ni ule wa kutunga sheria ya kuweka
stempu za TRA kwenye kazi za sanaa, kwa maelezo kuwa utamaliza wizi wa kazi za
muziki na filamu. Si mara moja taarifa imatolewa kuwa serikali ilitoa milioni
20 kwa mtafiti toka ‘Chuo Kikuu’ kuhakiki kuwa njia hiyo ndio itamaliza wizi wa
kazi za sanaa, hakuna ‘mtafiti’ anayejitokeza kuwa alipokea fedha na kufanya
utafiti huo, wala hakuna nakala ya utafiti huo, ni aina nyingine ya maamuzi
bila utafiti na matokeo yake wizi wa kazi za sanaa umeenea kila kona nchini na
mauzo halali ya kazi za muziki yamepotea. Ushauri tu kwa viongozi kuwa muziki
si shughuli ya kubahatisha ina misingi yake, ni muhimu kwa manufaa ya Taifa, umefika
wakati wa kufanya utafiti kwanza kabla ya kutoa maamuzi.
Tuesday, January 31, 2017
URAFIKI JAZZ BAND
Mzee Juma Mrisho aka Ngulimba wa Ngulimba liyekuwa Kiongozi wa Urafiki Jazz Band |
Bendi ya Urafiki (Urafiki Jazz Band), ilianzishwa mwaka 1970 na kiwanda cha nguo cha Urafiki kilichopo Ubungo. Jina rasmi la kiwanda lilikuwa ni FRIENDSHIP TEXTILE MILL. Kiwanda kilijengwa kwa msaada wa watu wa Jamhuri ya China na kwa urafiki huo kilipewa jina la Friendship Textile. Bendi ilianzishwa ili kutangaza bidhaa hasa Khanga na Vitenge za kiwanda hiki kwani wakati huo kulikuwa na viwanda vingine kadhaa vya nguo nchini kama vile Mwatex, Mutex, Kilitex, na kadhalika
Meneja Mkuu wa kiwanda cha Urafiki Bw. Joseph Rwegasira aliubariki mpango huo wa kuanzishwa bendi ya dansi ya kiwanda na hivyo aliidhinisha malipo ya hundi ya Shs. 50,000/= kununulia seti ya vyombo vya muziki kutoka katika duka la Dar Es Salaam Music House ambalo mpaka leo lipo katika mtaa wa Samora Avenue – Dar Es Salaam.
Ili kupata kundi lililo bora, Menejimenti ya kiwanda cha Nguo cha Urafiki ilimuajiri Juma Mrisho Feruzi maarufu kwa jina la Ngulimba wa Ngulimba na kumuagiza atafute wapigaji kutoka popote ili kuunda kundi imara.. Katika kuhakikisha bendi hiyo mpya inasimama, Ngulimba alichukua wapigaji watano kutoka Orchestre African Qwillado, bendi ambayo aliipigia kabla ya kuanza Urafiki. Na hii ndio maana nyimbo za mwanzoni za Urafiki Jazz Band zilionekana kama zina mahadhi ya Orch. Qwillado.
Wanamuziki aliowachukua Ngulimba kutoka Orch. Qwillado walikuwa ni Michael Vincent Semgumi, mpiga gitaa la Solo, Ayoub Iddi Dhahabu – Besi, Abassi Saidi Nyanga – Tenor Saxophone na Fida Saidi, Alto Saxophone. Ngulimba yeye akawa Muimbaji na pia Kiongozi wa Bendi.
Wanamuziki wengine wa mwanzo ambao waliungana na hao watano waliotoka Orch. Qwillado ambao tayari walikwisha ajiriwa kiwandani Urafiki, walikuwa – Juma Ramadhani Lidenge – Second Solo, Mohamed Bakari Churchil – gitaa la kati (rhythm), Ezekiel Mazanda – rhythm, Abassi Lulela – Besi, Hamisi Nguru – Muimbaji, Mussa Kitumbo – Muimbaji, Cleaver Ulanda – Muimbaji, Maarifa Ramadhani – Tumba, Juma Saidi – Manyanga (maraccass) na Hamisi Mashala – mpiga drums.
Mtindo walioanza nao Urafiki ulijulikana ‘Mchaka Mchaka’ na baadae ukabadilika na kuwa ‘Chaka Chua’ na hatimae mwisho mwisho bendi inaelekea ukingoni walipiga mtindo wa ‘Pasua’ na ‘Patashika’
Mwaka 1971 Gidion Banda, mwanamuziki kutoka bendi ya Morogoro Jazz alijiunga na kundi akiwa mpigaji wa Saxophone.
Aidha, Bendi ya Urafiki ilipitiwa na wanamuziki wengi baadhi wakiwemo Gideon Banda mpuliza saxophone kutoka Morogoro Jazz wengine wakiwemo Thobias Cosmas Chidumule na Frank Mahulu – Waimbaji waliotokea Western Jazz (Saboso) mwaka 1973 na kuongeza nguvu katika safu ya uimbaji. Waimbaji hao walishiriki nyimbo nyingi baadhi zikiwa Tausi Karuka, Jembe na Panga (Geza Ulole), Kosa la Nani, Mauaji ya Soweto, Rukia Hukusikia, Maonyesho ya Mtu Mweusi n.k.
Pia waliongezeka Mkali na Hidaya kutoka Morogoro wakipuliza matarumbeta, hao walikuja 1973 na Ali Saidi alietokea Cuban Marimba akipiga gitaa la kati (rhythm) na baadae mwaka 1975, Mganga Hemedi kutoka Tanga, akitokea Atomic Jazz, nae alijiunga na kuwa upande wa solo na rhythm.
Urafiki Jazz imetunga nyimbo nyingi, zaidi ya mia tatu zinazoelekeza kwenye siasa, mapenzi, nasaha na mafundisho na pia kukosoa. Baadhi ya nyimbo zake za siasa zilizopata umaarufu ni kama zile Mwenyekiti Nyerere, Mauaji ya Soweto, Jembe na Panga n.k..
Mwaka 1975 Bendi ilishiriki katika mashindano ya bendi za muziki wa dansi yaliyofanyika Mnazi Mmoja – D’Salaam na kushika nafasi ya tatu na Mzee Ngulimba, kama Kiongozi wa Urafiki aliiwakilisha Tanzania pamoja na bendi ya Afro 70 iliyopata nafasi ya kwanza na baadhi ya vikundi vya utamaduni kutoka Tanzania Bara na Zanzibar nchini Nigeria katika maonyesho ya mtu mweusi yaliyofanyika huko.
Saturday, November 12, 2016
RAJABU OMARY KUNGUBAYA APATA MGUU WA BANDIA KUTOKA KWA WAPENZI WA MUZIKI WA ZAMANI
Marehemu Omary Kungubaya |
Rajabu Kungubaya |
Rajabu
Omary Kungubaya, mtoto wa marehemu Omary Kungubaya, mwanamuziki ambaye alipata
umaarufu kutokana na wimbo wake wa ‘ Salamu za wagonjwa’ uliokuwa wimbo wa
kufungua na kufunga kipindi cha salamu za wagonjwa kilichokuwa kikirushwa na
Radio Tanzania, leo amepokea mguu wa bandia ili kumsaidia kutokana na mguu wake
wa kulia kuwa umekatwa kutokana na ajali ya bodaboda. Wanamuziki John Kitime na
Mjusi Shemboza walimuona Rajabu kwa mara ya kwanza siku walipoenda kumzika Mzee
Kungubaya na kuona umuhimu wa kumsaidia Rajabu kutokana na hali yake ya kutegemea magongo wakati
wa kutembea. Kwa kutumia kundi a Whatsapp la ZAMA ZILE, (kundi la wapenzi wa muziki wa zamani wanaosikiliza kipindi cha ZAMA ZILE kinachoendeshwa na John Kitime kupitia EFM 93.7fm kila Jumapili kuanzia saa 2-5 usiku), wanakikundi waliweza kuchanga fedha zilizowezesha kijana huyu kupata mguu wa bandia.
Rajabu ni mchangamfu anaeonekana kupendwa na kila mtu, kutokana na
majirani zake wote kumuunga mkono ikiwemo serikali ya mtaa wake. Mwenyekiti wa
serikali ya mtaa akiwa na wajumbe wengine wa serikali ya mtaa wake wote
walimsifu kwa tabia yake ambayo walisema ilikuwa ni mfano hasa kwa jitihada
zake za kutunza familia yake. Mke wa marehemu Mzee Kungubaya, ambaye ni mama mzazi wa Rajabu
alisema yeye alikuwa anategemea kuishi kwa kufanya kazi za kibarua katika
sehemu ambazo kuna ujenzi unaendelea, hufanya kazi kama kubeba maji na zege kuwasaidia wajenzi. Marehemu Kungubaya ameacha watoto wakiwemo wadogo
ambao mmoja yuko shule ya chekechekea na mwingine darasa la 6, wote hawa
wanamtegemea sasa kaka yao ambae ana mguu mmoja. Rajabu alikatika mguu kutokana
na gari kuovertake na kumfuata upande wake na kumgonga wakati akiwa kwenye
bodaboda, aliyemgonga, jina na namba ya simu ipo aliahidi kumsaidia lakini hajatimiza ahadi zake kwa kijaa huyu aliyempa ulemavu wa maisha.
Saturday, October 29, 2016
EXCLUSIVE- ANGALIA PAMBAMOTO LILIVYOKUWA LIKICHEZWA MIAKA YA 90 -VIDEO
Jukwaani wapiga magitaa
Miraji Shakashia- solo
John Kitime- Rythm
Manitu Musa - Bass
Drums- Juma Choka
Sax Rashid Pembe na Said Mohamed Ndula
Trumpet- Mawazo Hunja na Tuba
Uimbaji
Jerry Nashon, Mohamed Gotagota, na Abdallah Mgonahazelu
TOA MAONI
Friday, October 21, 2016
MAZISHI YA MZEE KUNGUBAYA
MWANAMUZIKI mkongwe ambaye alipata umaarufu kutokana na wimbo wake Salam za Wagonjwa amezikwa leo katika makaburi ya kifamilia Njeteni Kwembe. Msiba huo ulihudhuria na watu wengi wakiwemo majirani, ndugu, wanamuziki na wapenzi wa muziki wa Mzee Kungubaya.Tatu itakuwa siku ya Jumamosi 22/10/2016.
Jeneza likiwa nje ya nyumba ya marehemu |
Mwanamuziki Mjusi Shemboza akiongea na mmoja wa watoto wa marehemu Mzee Kungubaya |
Mjusi Shemboza akiwa na Mtendaji Mkuu wa COSOTA wa zamani Mzee Mtetewaunga |
Msafara wa kuelekea makaburini |
Mazishi ya Mzee Kungubaya |
Thursday, October 20, 2016
BURIANI OMARY KUNGUBAYA
Mzee Omari Kungubaya akipiga gitaa siku ya mkesha wa msiba wa Dr. Remmy Ongala |
Friday, October 7, 2016
BURIANI SALOME KIWAYA
Picha iliyopigwa Uingereza wakati Salome alipoenda huko na Shikamoo Jazz Band. Toka Kushoto Marehemu Salome Kiwaya, Marehemu Papa Wemba, na Marehemu Bi Kidude Mungu awalaze pema. |
Kwa masikitiko makubwa nimepokea taarifa za msiba wa Mama
Salome Kiwaya, mwanamuziki mkongwe. Taarifa zilinifikia kuwa Salome amefariki
katika ajali ya gari iliyotokea Dodoma sehemu za Meriwa. Nilimfahamu Salome kwa mara ya kwanza mwaka 1987, wakati nikiwa bendi ya Tancut Almasi Orchestra, tulipopiga kambi Dodoma Hotel
kwa muda wa miezi mitatu, tukitoa burudani kwanza kwa wajumbe wa mkutano wa Kizota, kisha wenyeji wa mji wa Dodoma. Katika kufahamiana kipindi hicho, tuliweza hata kupiga wimbo wake mmoja ulioitwa Tuhina, uliokuwa ukiimbwa na Kasaloo Kyanga na Kyanga Songa, ambao nao ni marehemu. Siku moja nilipita mtaani Dodoma na
kununua kanda za muziki wa Salome, nilizipenda sana nyimbo zake na nikamuahidi kuwa ningejitahidi
kuzipeleka kwa watu wenye uwezo wa kuendeleza kazi zile. Nilizipeleka kanda kwa Ronnie
Graham, Mscotch mmoja mwenye upenzi na uelewa mkubwa wa muziki wa Kiafrika na
hasa rumba, na huyu Mscotch ndie aliyewezesha kuanzishwa kwa bendi ya Shikamoo Jazz Band.
Baada ya kuzisikia nyimbo zile akaamua kuwa Salome asindikizane na bendi ya
Shikamoo kwenye ziara yao ya Uingereza kama muimbaji wa kike. Salome alienda
Uingereza na aliporudi ndipo alipoanza kununa vyombo na kuunda kundi la Saki
Stars, ikiwa ni kifupi cha Salome Kiwaya Stars. Mume wake Mzee Kiwaya nae ni
msanii maarufu aliyekuwa kiongozi wa kikundi cha Utamaduni cha CDA miaka hiyo ya 80.
Kuanzia hapo nimekuwa karibu sana na Salome, miaka ya 90 wakati nikiwa
Mwenyekiti wa CHAMUDATA, Salome ndie alikuwa mwenyekiti wa chama hicho katika
mkoa wa Dodoma baada ya mkutano mkubwa wa wanamuziki uliofanyika mwezi June
1998, kule Bagamoyo, ambapo wanamuziki 265 waliweza kukusanyika pamoja na kukaa
siku nne katika mji wa Bagamoyo wakifanya warsha za fani mbalimbali za muziki.
Katika miaka ya karibuni Salome alishughulika na sanaa ya urembo akiwa wakala wa Miss Tanzania kwa kanda ya Kati na kuweza kutoa MIss Tanzania mmoja, baadae aliingia katika siasa na kufikia kuwa Mwenyekiti wa UWT wa Mkoa wa Dodoma, lakini aliendelea na muziki katika maisha yake
yote.
Mungu Amlaze Pema Salome Kwaya. Ucheshi wako hatutausahau.
JOHN KITIME
JOHN KITIME
Friday, September 23, 2016
TANGA MJI ULIKOANZA MUZIKI WA DANSI
Wiki
hii nilipata bahati ya kutembelea mji wa Tanga, mji ambao sifa zake zilianza kusikika kuanzia
enzi za utawala wa Wajerumani, jiji ambalo shule ya kwanza ya serikali ilijengwa
hapa enzi hizo hizo za utawala wa Wajerumani, jiji ambalo liliendelea kukua sana
kutokana na kilimo cha katani na hivyo kukusanya vijana toka kila kona ya nchi
kuja kutafuta kazi katika mashamba makubwa ya katani wakati huo. Tanga mji
ambao kutokana na uwingi wa vijana wakati huo, shughuli za burudani ya muziki nazo
zilifikia kiwango cha juu kuliko sehemu nyingi Tanzania.
Ukizungumzia
historia ya muziki wa dansi, huwezi kukwepa kuzungumzia Tanga, kwani historia
inatueleza kuwa kabla ya kuanza vikundi vya muziki wa dansi kulianzishwa klabu
za kucheza dansi. Klabu hizo zikitumia muziki wa santuri, wanachama wake
walicheza na hata kushindana kucheza muziki kwa mitindo mbali mbali ya kigeni ikiwemo
waltz, tango, chacha, rumba na kadhalika. Klabu za kwanza nchini zilianzia
Tanga. Kulikuwa na klabu kama Young Noverty miaka michache baada ya vita ya
kwanza ya dunia, wakati huo nchi ya Tanganyika ikiwa bado changa kabisa. Mtindo
huu wa vilabu vya dansi ulienea na baadae kuingia Dar es Salaam na miji mingine
iliyokuwa imeshaanza wakati huo. Vilabu hivi ndivyo baadae vikaanzisha vikundi
vya kwanza vya muziki wa dansi. Hata majina ya vikundi hivyo vya kwanza
yalihusiana na klabu za burudani za wakati huo. Kulikuwa na vikundi kama Coast
Social Orchestra, Dar es Salaam Social Orchestra na kadhalika. Hivyo mji wa Tanga ulikuwa katika ndoto
za vijana enzi hizo. Kwa vile vijana wengi walikusanyika katika jiji hili nchi,
kulianzishwa pia klabu ambazo zilikuwa kwa ajili ya vijana waliokuwa wakitoka
kabila moja. Klabu hizo zikiwa na nia ya wananchama wao kusaidiana katika shida
na raha, na vilabu hivi pia vilikuwa ni sehemu muhimu katika kutoa burudani kwa
vijana waliotoka sehemu moja. Kati ya klabu hizi kulikuweko na klabu iliyoitwa
Young Nyamwezi, kama jina lake lilivyo ilikuwa ni klabu ya vijana kutoka
Unyamwezini. Hatimae mwaka 1955 klabu hii ilianzisha bendi yake iliyoitwa Young
Nyamwezi Band, bendi hii ilikuja kukua na baada ya Uhuru ilibadili jina na
kuitwa Jamhuri Jazz Band. Hakika kwa vijana waliokuwa wapenzi wa muziki miaka
ya 60 na 70 ilikuwa lazima uifahamu Jamhuri Jazz Band, muziki wake, au kwa
lugha ya enzi zile, ‘vibao’ vyake vilijulikana Afrika ya Mashariki nzima. Bendi
hii ilikuwa ikibadili mitindo ya upigaji wake na kupiga katika mitindo ya
‘Toyota’ na hatimae ‘Dondola’. Aliyekuja kumiliki bendi hii, ambayo wapenzi
wake pia waliita JJB alikuwa Joseph Bagabuje, kulikuwa hata maelezo wakati fulani kuwa JJB ilikuwa kifupi
cha Joseph Jazz Band na si Jamhuri Jazz band. Kama ilivyokuwa kawaida ya bendi
za wakati ule Jamhuri Jazz Band ilisafiri sana na kufanya maonyesho katika kila
kona ya nchi yetu, jambo hilo pamoja na kuwa bendi hii ilirekodi na kutoa
santuri kupitia kampuni za kurekodi za Kenya na pia kurekodi nyimbo zake katika
radio ya Taifa uliifanya bendi hii kuwa maarufu sana. Upigaji wa aina ya pekee
wa gitaa la rhythm wa bendi hii, ambao uligunduliwa na Harrison Siwale, maarufu
kwa jina la Sachmo, uliigwa na wapiga magitaa ya rhythm wengi nchini. Uimbaji
wa kutumia waimbaji wawili tu, uliopendelewa na bendi za Tanga wakati huo
ikiwemo bendi nyingine maarufu wakati huo, Atomic jazz Band, ulikuwa ni wa aina
yake pia. Jamhuri Jazz Band pia ndio kilikuwa chanzo cha bendi maarufu ya Simba
wa Nyika na bendi zilizozaliwa baada ya hapo. Nilibahatika kukutana mtu
aliyekuweko siku ya kwanza ya safari ya kuja kuzaliwa kwa Simba wa Nyika,
hakika ni hadithi yake ilikuwa ya kusisimua. Inasemekana kuwa siku hiyo Jamhuri
Jazz Band ilikuwa imekodishwa kwa ajili ya kupiga kwenye harusi kule Muheza.
Wanamuziki walikuwa wakilazimika kukusanyika katika jengo la klabu lililokuwa
Barabara ya 15 ili kupata usafiri wa kwenda Muheza. Siku hiyo wanamuziki wengine walikusanyika lakini
George na Wilson Peter, Luza Elian a wengine wachache hawakuonekana, baada ya
upelelezi mfupi ikajulikana kuwa wamejificha au wameondoka mjini Tanga, hivyo
ikalazimika kutafuta wanamuziki viraka wa haraka haraka kuweza kufanikisha
onyesho la siku hiyo, msimuliaji alinambia kuwa japo yeye hakuwa mwanamuziki
bali shabiki tu wa bendi aliweza kupanda jukwaani na kuimba katika harusi hiyo,
hali haikuwa mbaya kwani alijitokeza mteja mwingine akitaka bendi ikapige kwenye
harusi yake pia, lakini ombi lake lilikataliwa kwani wanamuziki walijua kuwa
hawakuwa kwenye kiwango chao. Na baada ya hapo kikaanza kipindi kigumu kwa
Jamhuri Jazz Band kujitahidi kurudisha hadhi na ubora wa bendi, na pia ikaanza
safari iliyokuja kubadili historia ya muziki wa dansi Afrika mashariki kwa
vijana hawa waliotoroka kuelekea Arusha ambako walianzisha Arusha Jazz Band na
hatimae kuvuka mpaka na kuingia Kenya ambako walianzisha Simba wa Nyika
ambayo mafanikio yake yanatingisha
hisia za wapenzi wa muziki wa dansi mpaka leo.
Wednesday, September 14, 2016
JAMHURI JAZZ BAND
Kwa mara ya
kwanza niliwaona 'Live', Jamhuri Jazz Band wakipiga katika ukumbi wa Community
Centre Iringa, ukumbi maarufu kwa wenyeji wakati huo kwa jina la Olofea senta
(Welfare Centre). Ni vigumu kuelezea jinsi nilivyokuwa najisikia kwani nilikuwa
sidhani kama kutakuja kuweko na wanamuziki wanapiga vizuri namna ile. Lakini
katika wote mpiga rythm guitar Harison Siwale, aliyejulikana kwa jina la
Satchmo, alikuwa na anabakia kuwa mpiga gitaa aliyenifurahisha kuliko wote.
Kwanza alikuwa na staili ya peke yake, na mpaka leo nikisikiliza nyimbo zake
kama vile Blandina, Mganga no 1, Maria bembeleza mwana au Ewe ndege, nabaki
kusifia kuwa huyu bwana alikuwa na kipaji cha pekee. Kuna rafiki yangu aliwahi
kumuuliza wakati ule huwa anapataje mawazo ya kupiga gitaa lake kwa staili ile?
alijibu kuwa huwa anajaribu kupiga sauti za viumbe mbalimbali wa porini katika
gitaa lake.
Wanamuziki waliokuwa katika bendi ya Mkwawa High School, Manji, Sewando, Danford Mpumilwa, Askofu Kakobe watakumbuka jinsi walivyoweza kupata nafasi ya kupiga pamoja na bendi hii kila ilipokuja Iringa mjini, maana hizo ndiyo zilikuwa taratibu wakati huo lazima bendi kubwa ikija, wanamuziki wadogo huomba Kijiko, na kama unaweza kuimba au kupiga vizuri unaachiwa nafasi ili muhusika akatafute mpenzi. Bendi ikifika katika mji, kama mji ule una bendi basi nao watapata nafasi ya kushirikiana na wageni. Bendi hii ilianza kwenye miaka ya 50 ikiwa ikijulikana kama Yanga Nyamwezi Band, Kiukweli ilikuwa ni Young Nyamwezi Band, bendi iliyokuwa imetengenezwa kwa ajili ya Vijana toka Tabora waliokuja kukata mkonge katika mashamba ya mkonge yaliyokuweko Tanga miaka hiyo. Na baada ya Uhuru ikajulikana kama Jamhuri Jazz Band, kifupi JJB japo kifupi hicho baadae kilidaiwa kuwa kilikuwa kifupi cha jina mwenye bendi Joseph Bagabuje. Wakati wa uhai wa Jamhuri Jazz bendi Tanga kulikuwa kuna waka moto kwa vikundi maarufu katika Afrika ya Mashariki kuwa vyote katika mji huo. Atomic Jazz, Amboni Jazz, Lucky Star, Black Star. Kwa vyovyote Tanga ulikuwa mji wa starehe wakati huo, hasa ukikumbuka kuwa kulikuweko na bendi nyingine ambazo hazikuwa maarufu labda kutokana na aina ya muziki zilizokuwa zinapiga. Kama vile ile bendi ya Magoa The Love Bugs ambayo ndiyo hatimae ilikuja kuwa The Revolutions na sasa Kilimanjaro Band
Wanamuziki waliokuwa katika bendi ya Mkwawa High School, Manji, Sewando, Danford Mpumilwa, Askofu Kakobe watakumbuka jinsi walivyoweza kupata nafasi ya kupiga pamoja na bendi hii kila ilipokuja Iringa mjini, maana hizo ndiyo zilikuwa taratibu wakati huo lazima bendi kubwa ikija, wanamuziki wadogo huomba Kijiko, na kama unaweza kuimba au kupiga vizuri unaachiwa nafasi ili muhusika akatafute mpenzi. Bendi ikifika katika mji, kama mji ule una bendi basi nao watapata nafasi ya kushirikiana na wageni. Bendi hii ilianza kwenye miaka ya 50 ikiwa ikijulikana kama Yanga Nyamwezi Band, Kiukweli ilikuwa ni Young Nyamwezi Band, bendi iliyokuwa imetengenezwa kwa ajili ya Vijana toka Tabora waliokuja kukata mkonge katika mashamba ya mkonge yaliyokuweko Tanga miaka hiyo. Na baada ya Uhuru ikajulikana kama Jamhuri Jazz Band, kifupi JJB japo kifupi hicho baadae kilidaiwa kuwa kilikuwa kifupi cha jina mwenye bendi Joseph Bagabuje. Wakati wa uhai wa Jamhuri Jazz bendi Tanga kulikuwa kuna waka moto kwa vikundi maarufu katika Afrika ya Mashariki kuwa vyote katika mji huo. Atomic Jazz, Amboni Jazz, Lucky Star, Black Star. Kwa vyovyote Tanga ulikuwa mji wa starehe wakati huo, hasa ukikumbuka kuwa kulikuweko na bendi nyingine ambazo hazikuwa maarufu labda kutokana na aina ya muziki zilizokuwa zinapiga. Kama vile ile bendi ya Magoa The Love Bugs ambayo ndiyo hatimae ilikuja kuwa The Revolutions na sasa Kilimanjaro Band
Mbaruku Hamisi,Abdallah Hatibu, Zuheni Mhando |
Eliah John, Alloyce Kagila, Musa Mustafa |
Yusuf Mhando, Joseph Bagabuje, Rajabu Khalfani |
George Peter, Harrison Siwale, Wilson Peter |
Subscribe to:
Posts (Atom)