Saturday, April 22, 2017

KIFO CHA SOKOINE KILIIKUTA ORCHESTRA MAMBO BADO IKO SHINYANGA


Mwaka 1984 nilikuwa mwanamuziki wa bendi ya Orchestra Mambo Bado, bendi iliyokuwa inaongozwa na Tchimanga Kalala Assossa. Bendi ilikuwa ni moja ya bendi zilizokuwa pendwa wakati huo, mtindo wa bendi ulikuwa unajulikana kama Bomoa. Neno hili lilitokana na wimbo wa Bomoa Tutajenga Kesho, wimbo ambao  baadae kwa sababu ambazo mpaka leo sizijui, ulikuja kupigwa marufuku na Umoja wa Vijana wa Mkoa wa Dar es Salaam wakati ule, usisike kwenye radio ya Taifa, redio ambao ilikuwa pekee wakati huo. Orchestra Mambo Bado ilikuwa na watu ishirini hivi, Tchimanga Assossa kiongozi na mwimbaji. George Mzee muimbaji, Lucas Faustin muimbaji, Jenipher Ndesile muimbaji, Banza Tax muimbaji, Athumani Cholilo muimbaji, John Kitime muimbaji, Likisi Matola mpiga gitaa la bezi, Andre Milongo akipiga gitaa la second solo, Huluka Uvuruge na Kazembe wa Kazembe wapiga gitaa la solo, William Maselenge akiwa kwenye gitaa la rhythm. Kulikuweko na wacheza show wanne, mafundi mitambo watatu na mweka hazina mmoja na meneja wa bendi. Masikani ya bendi yalikuwa katika ukumbi wa Lango la Chuma, Mabibo Dar es Salaam
Tarehe 12 April 1984, kundi zima lilitua katika mji wa Shinyanga baada ya kuwasili hapo kwa treni kutokea Dar es Salaam. Kwa taratibu za miaka hiyo, pamoja na ratiba ya ziara ya bendi kutangazwa kwenye gazeti la Uhuru, meneja wa bendi alikuwa akilazimika kutangulia mji ambao dansi litapigwa kuwahi kufanya mikataba na kumbi  ambazo dansi lingepigwa na pia kufuatilia vibali mbalimbali vya kuruhusu onyesho kufanyika. Mawasiliano yalikuwa magumu na urasimu ulikuwa mkubwa. Haikuwa kazi rahisi maana miaka hiyo ili bendi isafiri ililazimika kupata  kibali cha Afisa Utamaduni wa Mkoa ambao ni masikani ya bendi kuruhusu bendi kutoka nje ya Mkoa na kisha kibali hicho kupelekwa kwa Ofisa Utamaduni wa Mkoa ambao bendi inakwenda, nae baada ya kuruhusu bendi kuingia mkoani kwake, unaomba kibali cha Afisa Utamaduni wa Wilaya unakotaka kupiga muziki ili nae akuruhusu kufanya onyesho kwenye wilaya yake. Baada ya hapo meneja hutafuta na mtu ambaye ana spika ya mkononi, megaphone kuikodisha na kisha kutafuta mtu wa kutangaza onyesho. Ili kubana matumizi kuna mara nyingine wanamuziki wenyewe ililazimika wapite mtaani na spika hiyo kujitangaza. Kulikuwa na mji kama Mpanda wakati huo, ambapo mtangazaji hakuwa na megaphone, mtu maalumu alipita mtaa kwa mtaa akiwa na ngoma ambao aliipiga watu wakikusanyika basi anatangaza ujio wa bendi katika mji wao.
Tarehe 12 April 1984, Orchestra Mambo Bado iliwasili Shinyanga kwa treni ikitokea Dar es Salaam, kuanza ziara ya Kanda ya Ziwa. Wanamuziki tulionyeshwa vyumba vya kulala, mambo yalionekana kuwa yatakuwa mazuri kwa siku ile, matangazo yalikuwa yamebandikwa kwenye nguzo za umeme sehemu mbalimbali za mji, na hali ya kuonyesha kuwa watu walikuwa na taarifa ya ujio wetu ilikuwa dhahiri. Ilikuwa ni muda wa saa kumi hivi ilipotangazwa kuwa nchi imepata msiba mkubwa sana. Waziri Mkuu Edward Moringe Sokoine amefariki katika ajali ya gari jirani na Morogoro. Kwanza ilikuwa ni mshtuko, halafu akili ilipotulia tulijua kuwa na sisi kama bendi tunaingia kwenye tatizo kubwa sana, tulikuwa na nauli ya kuja tu mpaka Shinyanga, na fedha ya kula ya siku moja tulikuwa tunategemea kupiga dansi ili kuweza kulipa malazi ya siku hiyo na kupata fedha ya kula na kuendelea na safari kesho yake, tukitegemea mapato mengine makubwa katika maonyesho ya Mwanza wikiendi iliyokuwa inafuata. Hayo yote tulijua sasa yameharibika, tulirudisha vyumba vyote mara moja na kubaki na viwili tu kimoja kikiwa cha wasichana waliokuwa kwenye bendi, wengine wote ikalazimu tuhamishie mizigo yetu chumba kingine. Baadae tulikaa na Afisa Utamaduni kutafakari kama dansi lingeweza kulia siku ile, na kama halitalia nini hatima ya watu hawa 20 wageni kutoka Dar es Salaam? Kama kiasi cha saa moja jioni, Afisa Utamaduni akaruhusu tupige dansi ili tuweze kupata nauli ya kurudi Dar es Salaam, kwani ilijulikana wazi kitaanza kipindi cha maombolezo ambacho hakuna mtu alijua kitaisha lini,  hivyo hakukuwa na sababu ya kuendelea na safari kutoka hapo. Vipindi vya maombolezo huwa ni vipindi ambavyo pamoja na mambo mengine shughuli za muziki husimamishwa. Kwa wanamuziki na wale wanaotegemea shughuli za muziki na familia zao, kipindi hiki huwa kigumu sana. Lakini kinaleta ukakasi akilini kwani shughuli za kupiga muziki kwenye kumbi husimamishwa, madisco hufungwa na vikundi vya muziki haviruhusiwi kufanya  kazi lakini radio huendelea kupiga muziki uleule ambao umezuiwa kwenye kumbi, sehemu za starehe kama baa huendelea kupiga muziki na kufanya biashara zao bila tatizo ila wanamuziki ndio huzuiwa kufanya shughuli zao kwa maelezo kuwa ni kipindi cha maombolezo. Nakumbuka sana misiba  mikubwa ya viongozi wetu ukiwemo wa Baba wa Taifa kwa sababu kubwa mbili, kwanza uchungu wa kupoteza kiongozi wetu na njaa iliyofuatia baada ya hapo.

No comments:

Post a Comment