Tuesday, December 16, 2014

HATIMAE SHEM IBRAHIM KARENGA AZIKWA

HATIMAE  mwanamuziki mkongwe mpiga gitaa muimbaji na mtunzi mahiri Shem Ibrahim Karenga amezikwa katika makaburi  ya Kisutu jioni ya leo. Shughuli hiyo ilianza kwa utata baada ya kuwa makaburini hapo kulikuwa na misiba minne hivyo kila lilipokuja jeneza wanamuziki, ndugu na wapenzi wa muziki walijikuta wakisindikiza jeneza na..........INAENDELEA HUKU

Monday, December 15, 2014

BURIANI SHEM IBRAHIM KARENGA

LEO Jumatatu tarehe 15 Desemba 2014, majira ya saa nne asubuhi taarifa zilianza kusambaa kuwa mwamba mwingine wa muziki wa dansi Tanzania umedondoka. Mzee Shem Karenga hatunae tena,kwa vyovyote waliohudhuria dansi alilopiga Ijumaa na Jumamosi iliyopita pale Mwembeyanga watakuwa hawaamini, lakini imekuwa mapenzi ya Mungu, kwamba asubuhi ya leo aliamka hajisikii vizuri na alipelekwa hospitali ya Amana lakini hakukuweza kufanyika kitu Mzee akarudi kwa Muumba wake. Mungu aipokee roho yake. Miezi michache iliyopita tulipata muda mrefu wa kuongea na Mzee Shem Karenga ili kujua alikotokea na mawazo yake kwa sasa mazungumzo yalikuwa kama ifuatavyo;................................. ENDELEA HUKU

Monday, November 10, 2014

LEO NIMEKUMBUKA KIBAO MASAFA MAREFU CHA TANCUT ALMASI...angalia video


Kasaloo Kyanga ndie mtunzi wa kibao hiki maarufu, kilirekodiwa RTD Dar es Salaam katika awamu ya pili ya recording za Tancut Almasi. Recording hii ilitaka kuvunja bendi kwa kuwa wakati bendi ikiwa studio, Said Mabela alipita studio na Katibu wa bendi akamuuliza kwa siri anausikiaje muziki? Sijui kwa sababu gani lakini Mabela alijibu, "Hapa hakuna kitu nasikia solo tupu". Katibu wa bendi ambaye pia wakati huo alikuwa Katibu wa tawi la JUWATA la Tancut, akatujia juu wanamuziki wa Tancut kuwa tunapiga solo tupu na hivyo tuache kurekodi na bendi irudi Iringa kwa mazoezi zaidi. Ulikuwa ugomvi mkubwa, wakati huo Mabela amekwisha ondoka hata kumuuliza alikuwa ana maana gani haikuwezekana. Fundi wa RTD James Muhilu ndie aliyemtuliza Katibu huyo kwa kumueleza kuwa nae haelewi maana ya maneno ya Mabela na recording ikaendelea na dunia ikapata bahati ya kusikia kibao hiki. Nakumbuka katika awamu ya kwanza ya kurekodi Sidi Morris alikuja studio na kupiga tumba katika vibao kadhaa kikiwemo Wifi utunzi wa mwenye blog hii John Kitime. Hili lilileta mzozo Maquis ambako Sidi alikuwa akifanyia kazi na hivyo akasimamishwa bendi kwa kushiriki kurekodi

Saturday, November 8, 2014

HISTORIA FUPI YA TAARAB

Taarab ina historia ndefu katika muziki wa Tanzania kama ulivyokuwa muziki wa dansi. Wapenzi wa taarbu wa zamani waliiweka taarabu katika vyanzo kama Taarab ya Tanga, Taarab ya Dar es Salaam,Taarab ya Zanzibar na Taarab ya Mombasa. Taarab ya Zanzibar wakati huo........INAENDELEA HUKU

Wednesday, October 22, 2014

MIAKA KUMI YA KUMBUKUMBU YA KIFO CHA NDALA KASHEBA

ndala-kasheba_2255445LEO tunatimiza miaka kumi toka kifo cha mwanamuziki mahiri Freddy Supreme au maarufu kama Ndala Kasheba. Freddy alianza kufundishwa gitaa na baba yake wakati akiwa na umri wa miaka 12. Baba yake alijua kupiga gitaa japo hakufanya kazi ya uanamuziki, alikuwa akipiga gitaa nyumbani baada ya saa za kazi. Moja ya bendi maarufu ambazo zilimtambulisha sana Fredd ilikuwa Orchestra Fauvette, Freddy alieleza kuwa bendi ya Orchestra Fauvette ilianza tarehe 7 mwezi wa sita mwaka 1964 katika jiji la Lubumbashi huko Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo. Jina hilo Fauvette........ENDELEA HUKU

Saturday, October 11, 2014

ALLY RASHID AZIKWA KEKO

Umati mkubwa wa watu ulijitokeza kumzika Ally Rashid mwanamuziki wa siku nyingi ambaye alifariki jana mchana. Mazishi yalifanyika katika makaburi ya Keko Machungwa  kaburi lake likiwa jirani kabisa na la mwanamuziki mwingine nguli Moshi William. Mazishi ya Mzee Alyy yalifanyika muda wa saa nne asubuhi pia na kuhudhuriwa na wanamuziki wengi wa zamani na hata wa sasa akiwemo Mchizi Mox ambaye alikuwa kimwita marehemu baba yake mdogo.
MUNGU AMLAZE PEMA ALLY RASHID KWA PICHA INGIA HAPA

Friday, October 10, 2014

MPIGA SAXAPHONE MKONGWE ALLY RASHID 'SABOSO' AFARIKI DUNIA

Mwanamuziki wa zamani aliyekuwa mpiga saxaphone aliyejulikana pia kama Mzee Saboso, Ally Rashid amefariki dunia leo mchana. Mzee Ally kwa mara ya mwisho alikuwa bendi ya Msondo Ngoma. Wiki chache zilizopita mtandao wetu ulifanya mahojiano marefu na Mzee Ally hivyo soma hapa historia ndefu ya Mzee huyu. Mpaka muda huu ndugu zake hasa wa Zanzibar ambako ndio kwao walikuwa hawajatoa taarifa ya taratibu za maziko. Mara tutakapopata taarifa zaidi tutawataarifu.
Mungu Amlaze Pema peponi Mzee Ally Rashid


   HISTORIA YA ALLY RASHID KHAMIS ‘SABOSO’ ISOME HAPA

Thursday, September 11, 2014

Saturday, August 30, 2014

IFAHAMU HISTORIA YA MAFUMU BILALI BOMBENGA =SUPER SAX

HAPA AKIPIGA TUMBA SIKU YA MKESHA WA MAZISHI YA REMMY ONGALA


AKIWA NA MPULIZA SAX MWENZIE JOSEPH BERNARD
African Beat ilianzishwa mwaka 1998, baada ya Mafumu Bilali Bombenga kujiengua kutoka katika bendi ya African Stars ambayo nayo ilianzishwa mnamo mwaka 1994 kwenye Hoteli ya Bahari Beach, jijini Dar es Salaam, huku yeye akiwa ndiye  muanzilishi.
Bombenga anakumbuka kuwa, wakati akiwa na African Stars ambayo hata jina lake alilibuni yeye, walitamba na vibao kama ‘Sakatu Sakatu’, ‘Mayanga’, ‘Maya’, ‘Afrika’ na ‘Dance Dance’.
Baadhi ya wanamuziki waliokuwa wakiunda kundi hilo la African Stars linalojulikana zaidi hivi sasa kama ‘Twanga Pepeta’, ni Bob Gady, Andy Swebe, Alfa Nyuki, Palmena Mahalu, Pamela pamoja na Kayumbu ‘Amigolas’.
“Historia yangu kimuziki, inaanzia mwaka 1972 nilipojiunga na bendi ya Morogoro Jazz, wakati huo nikitokea jeshini Makutupola,” anasema Bombenga.
Mwaka 1973 aliingia na Western Jazz alioshiriki nao kupiga Saxophone, kwenye vibao kadhaa vya bendi hiyo, vikiwamo ‘Hakika’, ‘Kazi ni Kazi’ na ‘Sadaka’, kabla ya mwaka 1978 kutimkia Dar International.
Pamoja na kupuliza kiustadi Saxophone pamoja na kuimba kwenye nyimbo kemkemu, zikiwamo ‘Mayasa’ na ‘Zuena’, lakini pia Bombenga alishiriki kucharaza gitaa la Solo katika kibao ‘Vick’.
Mwaka 1979 alibeba mabegi na kutua Vijana Jazz Band alikotunga kibao ‘Taabu’ na pia kushiriki kukiimba, huku kadhalika akipuliza Saxophone kwenye vibao kama ‘Chiku’ na ‘Matata Ndani ya Nyumba’.
Mwaka 1980 alihamia Maquis ambapo alitesa kwa kupuliza Saxophone kwenye vibao viiingi, baadhi yake ni ‘Zoa’, ‘Sina Ndugu’, ‘Noel’ pamoja na ‘Maige’.
“Nilikaa Maquis hadi mwaka 1984 nilipochomoka tena na kuhamia Bima Lee nilikokutana na wakali kama Jerry Nashon ‘Dudumizi’, Shaaban Dede ‘Super Motisha’, ‘Joseph Mulenga ‘Spoiller’,” anasema Bombenga.
Mwaka 1985 Bombenga alikuwa mwanzilishi wa bendi ya MK Group ‘Ngoma za Maghorofani’, kabla ya mwaka 1986 kuwa tena mmoja wa waanzilishi wa Tancut Almas ya Iringa.
Mwaka 1987 alirejea tena MK Group ambapo nyimbo yake ya kwanza kupuliza Saxophone awamu hii ya pili ilikuwa ni ‘Utakuja Kuanguka Kwenye Matope’.
Mwaka 1989, kaka yake Adam Kinguti alirudi nchini akitokea Sudan alipokuwa akifanyakazi kwenye ofisi za ubalozi, wakaanzisha Bicco Stars na yeye kushiriki kupuliza Saxophone kwenye vibao kadhaa kama vile; ‘Magret Mage’, ‘Wapangaji’ na Kisamvu’.
Mwaka 1991 alitoka Bicco akiwa na mpapasaji kinanda mahiri wa kike ambaye kwa sasa ni marehemu, Asia Daruweshi, baada ya kutokea hali ya kutoelewana kati yake na Kinguti, wakaanzisha Zanzibar Sound.
“Tukiwa na Zanzibar Sound, tulipata mkataba katika Hoteli ya Mount Meru, Arusha na mwaka mmoja baadaye mwanamuziki mwenzetu kwenye bendi hiyo, Kanku Kerry alipata mkataba Japan tukaondoka naye kwa sharti la sasa kujiita Kilimanjaro Connection,” anasema Bombenga.
Walizunguka nchi nyingi za bara la Asia wakiwa na Kilimanjaro Connection, waliporudi mwaka 1994 alijitoa na baadaye kidogo Asia naye alijitoa na kurudisha upya bendi yake ya Zanzibar Sound na kurejea mkataba wake Bahari Beach Hotel.
Bombenga wakati huu akabaki bila bendi, ambapo muda si muda Asia alipata kazi nchini Bahrain na kumuachia Bombenga mkataba wa Bahari Beach.
Baada ya kuona ameachiwa mkataba wakati hana bendi, Bombenga ndipo alipomfuata Baraka Msirwa na kumuomba vyombo vya muziki ambapo alimpa kwavile havikuwa na kazi kutokana na kufa kwa bendi za MK Group, MK Beat na MK Sound zilizokuwa zikivitumia.
“Hicho ndio kilikuwa chanzo cha bendi ya African Stars niliyoibuni mwenyewe hadi jina, iliyoniletea uhasama mkubwa na dada yangu Asha Baraka baada ya kujitoa,” anasema Bombenga.
Kwa upande wa warithi, Bombenga ana wanawe wawili wanaoonekana kufuata vema nyayo zake, ambao ni Feruzi (22) anayepapasa kinanda na Aziza (19) ambaye ni mwimbaji.  
Bombenga mwenye miaka 40 katika muziki na aliyejifunza mengi kupitia sanaa hiyo, anavutiwa na waimbaji; Isha Mashauzi, Nasseeb Abdul ‘Diamond’, Flora Mbasha na Hassan Bitchuka.
Anatoa ushauri kwa wanamuziki wa Dansi kuketi na vyombo vya habari na kuzungumza, ili kuangalia namna ya kuurejesha kwenye chati muziki wao ambao umekuwa ukiporomoka kila uchao.
Mikakati ya baadaye ya Bombenga ni kustaafu muziki na kujihusisha na ujasiriamali, baada ya kwenda nchini Kinshasa na kufanya maonesho na baadhi ya mastaa wa huko.
“Mimi ni mtoto wa tano katika familia ya mzee Bilali Mafumu, niliyepata elimu yangu ya msingi katika shule ya H.H Agakhan, Kigoma nilikofaulu na kujiunga na shule ya sekondari Kazima, Tabora nilikosoma hadi kidato cha nne,” anasema Bombenga.
Baada ya kumaliza elimu ya sekondari, Bombenga aliyesoma shule moja ya sekondari na mbunge wa Tabora, Ismail Aden Rage, anasema kuwa 1972 alijiunga na JKT kwa mujibu wa sheria ya enzi hizo, alikojifunza kuimba na kupuliza Saxophone.
Anaishi Vingunguti, jijini Dar es Salaam na familia yake ambayo ni mkewe na watoto saba, huku akitamani kuongeza wake wengine hadi wawe watatu.





  

Friday, August 29, 2014

MFAHAMU MKONGWE WA SAXOPHONE RASHID PEMBE

RASHID PEMBE


 “TUKIO la kuutumikia Umoja wa Vijana kwa muda wa miaka 18 na kulipwa mafao ya sh. Mil 1.6, baada ya kustaafu, ndilo linalosumbua kichwa changu hadi leo, ambalo kiukweli sitakaa nikalisahau,” ndivyo anavyoanza kueleza Rashid Pembe.
Pembe ni kati ya wanamuziki nguli wa miondoko ya Dansi, aliyetokea mbali hadi sasa ambapo anaonekana amepata mafanikio kiasi kupitia sanaa hiyo.
Mwaka 2005 aliomba kustaafu kuitumikia bendi ya Vijana Jazz aliyokuwa nayo tangu Aprili, 1987, baada ya kuona imeanza kuyumba na kupoteza mwelekeo na kilichomkuta ndio hicho ambacho wakati fulani aliwahi kujutia kuwa mwanamuziki wa Dansi.
Kwa sasa Pembe anamiliki bendi yake binafsi, inayojulikana kama Mark Band, ambayo chanzo cha jina ‘MARK’ ni herufi moja moja za majina ya mwanzo ya wanamuziki wanne wanzilishi wa bendi hiyo.
Wanamuziki hao na nafasi zao kwenye mabano, ni pamoja na Mgazija (Bass), Alex (Solo), Rashid (Saxophone) na Karamazoo (Saxophone).
Mark Band iliasisiwa rasmi mwaka 2006, ambapo baada ya kuiunda, waliamua kuwaongeza wanamuziki wengine kama Said Majivu (Drums), Said Makelele (Tarumbeta) pamoja na Noel Minja na Balusi Kitembo ambao ni waimbaji.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Pembe anasema kuwa, kama ilivyo kwa bendi nyingine nyingi, walipoanzisha bendi hiyo walikumbana na changamoto kemkemu, ikiwa ni pamoja na kukodi vyombo kwa gharama kubwa.
“Hata hivyo, Mungu alitujalia kwani baadaye tulipata mkataba wa kutumbuiza siku tatu katika wiki, kwenye Hoteli ya See Criff, jijini Dar es Salaam, tukaanza kujipanga kwa ununuzi wa vyombo vyetu wenyewe,” anasema Pembe.
Anamtaja Waziri wa zamani wa Mambo ya Ndani, Mheshimiwa Mohammed Seif Khatibu kuwa ni kati ya watu waliochangia kuwakwamua ndani ya Mark Band kwa kuwaombea mkopo wa sh. Mil 3, kwenye Hoteli ya See Criff walioilipa polepole kwa kufanya shoo hapo.
Waliitumia pesa hiyo kwa kuchanganya na nyingine walizipata kupitia maonesho yao mengine na kununua vyombo kidogo kidogo hadi sasa wanapomiliki vyombo vyenye thamani zaidi ya sh. Mil 50.
Mwaka 2010 waliingia mkataba na Kampuni ya Kijerumani iitwayo ‘Mother Africa’ wa kutumbuiza nchi mbalimbali kama vile; Misri, Sweden, na nchi za Amerika ya Kusini kama vile Chile na Peru na pia  Ufaransa pamoja na Ujerumani yenyewe.
“Tumekuwa na maisha ya namna hiyo kwa muda mrefu sasa, ya kutumbuiza nje, huku hapa nchini tukifanya shoo nyakati za likizo zetu tu,” anasema Pembe.
Pembe anasema, tayari kwa upande wa nyimbo, Mark Band imeshafyatua albamu nzima, ambapo ni kibao kimoja tu kiitwacho ‘Matukio’ ndicho walichokisambaza kwenye vituo mbalimbali vya radio na runinga hapa nchini.
Vibao vingine kwenye albamu hiyo waliyoirekodia katika Studio za Bakunde Production, jijini Dar es Salaam, ni ‘The Girl From Tanzania’, ‘Baba Kaleta Panya Remix’, ‘Amani’, ‘Anjela’ na ‘Pombe’.
Pembe anasema, mafanikio ndani ya Mark Band ni kumiliki vyombo vya thamani, kuwa na akaunti nono na kujulikana duniani kote, huku mafanikio kwa upande wake ikiwa ni kuwasomesha wanawe na kuanza kuwanunulia viwanja kila mmoja na chake.
Akielezea namna alivyojifunza muziki, Pembe anasema kuwa mwaka 1981 alijiunga na Jeshi la Polisi kama fundi ujenzi, baada ya kumaliza masomo yake ya Sekondari.
“Nikiwa Polisi, wakati najiandaa kupelekwa chuo cha ufundi, Marehemu Tx Moshi William aliyekuwa kwenye bendi ya jeshi hilo wakati huo, alinishauri kuachana na ufundi na kujiunga na kitengo cha Bendi,” anafahamisha Pembe.
Pembe anasema, Tx Moshi alimshauri hivyo kwasababu waliishi mtaa mmoja kabla hawajawa polisi, ambapo alikuwa akimuona namna alivyokuwa ‘mtundu’ kwenye gitaa la Solo.
Kiongozi wa polisi wakati huo, Mzee Mayagilo akamuombea Pembe uhamisho, lakini pia wakati anasubiri kwenda kuendelezwa ujuzi wa kupiga gitaa, mpigaji Saxophone wao, Abdul Mwalugembe akastaafu.
“Tukio hilo lilimfanya Mayagilo kunibadilisha na nikaanza kusomea upulizaji Saxophone, ambapo nilisoma nadharia mwezi mmoja na nusu na vitendo pia muda kama huo, nikawa fiti kabisa,” anasema Pembe.
Anasema kuwa, alirekodi nyimbo nyingi Polisi Jazz, baada ya zile zilizoambatana na ‘Mwaka wa Watoto’, ambazo hata hivyo hazikuchukua chati.
Mwaka 1987 alistaafu ligwaride akiwa askari mwenye cheo cha Koplo, kwa kununua mkataba, baada ya kuvunjika ghafla kwa ahadi aliyopewa na Jeshi, ya kupelekwa nchini Korea kuendelezwa kimasomo, kwa sababu alihisi ndoto zake za kufika mbali kielimu zilishagonga ukuta wa zege.
Akiwa na Vijana Jazz aliyojiunga nayo wakati imetoka kuipua vibao kama ‘Mari Maria’, ‘Ambha’ na ‘Bujumbura’, Pembe anasema kuwa, kibao chake cha kwanza kurekodi kilikuwa ni kile kinachokwenda kwa jina la ‘Miaka 10 ya Umoja wa Vijana’.
“Hadi nafungasha virago Vijana Jazz, niliyoitumikia na kushika nyadhifa mbalimbali za Kiuongozi, nilikuwa nimetunga vibao vinne ambavyo ni ‘Siri ya Ndani’, ‘Baba Sammy’, ‘Mwanamke Salo’ na ‘Dar es Salaam’,” anasema Pembe.
Pembe asiyependa kuona bendi haina maendeleo na ambaye katika muziki anawakubali King Enock na Elias Nyoni, anasema hajapata mafanikio wakati wa Vijana Jazz, zaidi ya kusafiri nchini Zambia pekee.
Kwa mtazamo wake, Pembe anaona biashara huria na udhamini katika vipindi, kwenye vituo mbalimbali vya radio na runinga ndivyo vinavyochangia kwa kiasi kikubwa kuliua Dansi.
Anasema mfumuko wa vituo vingi vya radio na runinga umefanya kuwapo na upendeleo binafsi kwa badhi ya mitindo ya muziki, huku mingine ikididimizwa kwa makusudi kwa manufaa ya watu wachache kama si mtu mmoja.
“Watoto wangu wanaoonekana kufuata kwa karibu zaidi nyayo zangu baba yao, ni Omary (21) ambaye yuko Kisiwani Zanzibar hivi sasa akijishughulisha na muziki wa Hoteli na Mwajuma (15), ambaye bado ni mwanafunzi wa darasa la saba,” anasema Pembe.
Tayari Pembe aliye mbioni kufungua chuo cha Saxophone, ameshawaambukiza wengi kipaji cha upulizaji chombo hicho, badhi yao wakiwa ni wanamuziki wa Dansi, Injili pamoja na miondoko mingine.
Aidha, badhi ya wasanii wa miondoko ya muziki wa Bongofleva waliomshirikisha kupuliza Saxophone kwenye vibao vyao, ni pamoja na Q Chillah, Kikosi cha Mizinga na Cindi katika nyimbo ya pamoja na Ommy Dimpoz.
Huyo ndiye Rashid Pembe, baba wa familia mwenye mke na watoto sita ambao ni Rehema, Pembe, Amina, Omary, Khalid na Mwajuma.
Alizaliwa mwaka 1957, Kisarawe Pwani na kupata elimu ya msingi katika shule nne tofauti ambazo ni Kisarawe, Vikindu, Sotele na Kisiju zote za mkoani Pwani, kuanzia mwaka 1966 hadi mwaka 1972





Tuesday, August 19, 2014

ALIKOPITIA MWANAMUZIKI HUSSEIN JUMBE HAKUKUWA RAHISI


Nchini Tanzania, sanaa ya muziki wa dansi ni miongoni mwa kazi kadhaa za sanaa zinazoaminika kuwa ni za kujitolea zaidi.
 Inaaminika hivyo kutokana na ugumu wa kazi yenyewe ukilinganisha na mafanikio yake.
 Hapa nchini hadi kuyafika mafanikio, wanamuziki wengi kwanza hupitia taabu, mashaka na vikwazo kemkemu kiasi ambacho kama mtu si mstamilivu atakata tamaa 'mchana mchana!'
 Tunayo mifano mingi inayoweza kuyakinisha hayo, ila mfano mmoja  wapo ambao ndio wa karibu zaidi ni mwanamuziki Hussein Suleiman Jumbe 'Mzee wa Dodo' kama anavyojulikana kwa wengi.
 Jumbe ambaye alizaliwa miaka takriban 51 iliyopita, ni mwanamuziki nguli aliyejaaliwa kipaji adhimu cha sauti ya uimbaji. Ni mtunzi hodari pia mwenye tungo zilizojaa hisia na zinazosisimua zaidi, ambazo mara nyingi hugusa kila rika la watu.
 Kwa hivi sasa, nguli huyo aliyepata elimu yake ya msingi katika Shule za Uhuru Mchanganyiko Primary na Muslimu Secondary School zote za Dar es Salaam, anamiliki bendi yake mwenyewe inayojulikana kama Talent Band.Akizungumza leo asubuhi nyumbani kwake, Temeke Mwembeyanga, jijini Dar es Salaam, Jumbe anasema aliamua kujifunza muziki baada ya kuvutiwa na nyimbo za marehemu Marijani Rajab 'Jabali la muziki'.
 "Nilikuwa natembea na radio yangu kwa ajili ya kusikiliza nyimbo za Marijani, enzi hizo akiwa na bendi ya Safari Trippers," anakumbuka Jumbe na kuongeza kuwa vibao vilivyokuwa vikimpagawisha zaidi ni 'Roza Nenda Shule', 'Mwalimu Nyerere' na 'Nani Mchokozi'.
 Anasema, kabla nyimbo hizo hazijatoka kwenye radio, alizijua na kwamba alikuwa akiziimba kila alipokaa ambapo wakati huo ndio kwanza alikuwa bado yuko shule ya msingi.
 Anakumbuka zaidi kuwa kutokana na mapenzi yake kwa Marijani, mara kwa mara alikuwa anatembelea maonyesho yake na kila Jumapili alikuwa hakosi kwenda katika ukumbi uliokuwa ukijulikana kama ' Princess uliokuwa maeneo ya Mnazi Mmoja kwenye 'bugi dansi' dansi la mchana siku za Jumapili lililoisha saa kumi na mbili jioni, ambapo kiingilio chake kilikuwa shilingi tano tu.
Mnamo mwaka 1979, wakati akiwa darasa la nne alijiunga kwa siri na kundi la Orchestra Siza, ambalo maskani yake yalikuwa Mtaa Ruvuma, Temeke, jijini Dar es Salaam ambako pia ndiko alikokuwa akiishi yeye.
 Hapo katika kundi la Orchestra Siza, Jumbe anasema ndiko kwa mara ya kwanza alikokutana na mwanamuziki Roshi Mselela waliyepatana nae kupita kiasi, akawa bado anaendelea na muziki kwa siri.
 Lakini kwa vile dunia haina siri, mwaka mmoja tu baadaye wazazi wake wakagundua janja yake ya kujiingiza katika muziki na kuzembea masomo shuleni, wakamgombeza na kumpiga marufuku kufanya muziki.
 Hata hivyo, mwenyewe Jumbe anakiri kwamba kuishi bila kujihusisha na masuala ya muziki ilikuwa ngumu kwake, mwaka 1981 akajiunga tena kwa siri na kundi lingine la muziki wa dansi, Asilia Jazz ambalo lilikuwa likimilikiwa na Baraza la Muziki Tanzania (BAMUTA).
 "Safari hii, baba alipokuja kugundua kuwa naendelea kujishughulisha na muziki, alinichukua na kunipeleka kufanyakazi katika kiwanda cha plastiki," anasimulia Jumbe na kufafanua kuwa hapo aliajiliwa  kama Msimamizi wa Uzalishaji (Production Foremen).
 Huku akicheka, Jumbe anasema kuwa aliacha kazi kiwandani hapo mara moja baada ya kuona anakosa muda wa mazoezi ya muziki, ambapo kilichofuata ni familia yao yote kumtenga na kumsusa kabisa.
 "Nakumbuka katika kipindi hicho nilichosuswa na familia, nilitaabika kwa dhiki mpaka nilifikia hatua ya kuvaa viraka," anasema Jumbe.
 Anasema kuwa, katika jitihada zake za kuhakikisha hautupi mkono muziki, mwaka 1983 alilikimbia jiji la Dar es Salaam na kwenda Tabora kutafuta bendi atakayoitumikia kwa kujinafasi. Huko akapokewa na mkongwe Shem Kalenga ndani ya bendi ya Tabora Jazz ambako pia alikutana na mwimbaji Mohammed Gotagota ambaye kwa sasa ni marehemu.
 Tabora Jazz alikaa kwa miaka miwili, akachomoka akatokomea Musoma, Mara. Huko alikaa mwaka mmoja tu wa 1985 na ilipofika 1986 aliamua kurejea Dar es salaam kwani alikuwa amepokea taarifa ya msiba wa baba yake mzazi.
 "Nilipowasili, nilikuta tayari baba amekwishazikwa," anasikitika Jumbe na kusema kuwa baada ya hapo hakuona haja ya kuwa mbali na familia hivyo alimfuata Gotagota aliyekuwa bendi ya Urafiki wakati huo,nae akamuunganisha na kuwa muimbaji wa bendi hiyo.
Akiwa Urafiki Jazz 'Wana Chakachua' iliyokuwa ikiongozwa na Juma Mrisho 'Ngulimba wa Ngulimba', ndipo Jumbe alipoanza kudhihirisha makali yake katika utunzi kwani aliporomosha kibao kizito kilichokwenda kwa jina la 'Usia wa Mama'.
 Oktoba 17, 1987 aliitwa na mtu asiyemfahamu ambaye alimweleza kuwa amependezwa na uimbaji wake hivyo siku hiyohiyo aende makao makuu ya Mlimani Park yaliyoko karibu na Chuo Kikuu Dar es salaam. Yule mtu alikuja kumtambua baadaye kuwa kumbe alikuwa Hassan Rehani Bichuka 'Super Stereo'.
 “Wimbo wangu ya kwanza kabisa kutunga nikiwa na Wana Mlimani Park ni ule usemao 'Hisia za Mwanadamu' ambao mwaka 1990 ulishiriki mashindano ya nyimbo kumi bora na kushika nafasi ya tatu, ambapo nafasi ya kwanza ilinyakuliwa na bendi ya MK Group 'Ngoma za Magorofani’ na ya pili ikatwaliwa na Salna Brothers.
 Alidumu Mlimani Park kwa muda mrefu na kushiriki kuimba na kutunga vibao vingi vikali ambavyo baadhi yake ni ‘Epuka No2’, ‘Nuru ya Upendo’, ‘Shamba’, ‘Mtoto wa Mitaani’, ‘Chozi la Kejeli’, ‘Nachechemea’ na ‘Isaya Mrithi Wangu’ ambazo kila moja kwa wakati wake ilitikisa vilivyo.
 Mwaka 2002, aliondoka DDC na kujiunga na TOT Plus 'Achimenengule', ambapo kama kawaida yake, akiwa na kundi hilo lililokuwa chini ya Mbunge wa Mbinga Magharibi, Capt John Damian Komba, Jumbe aliporomosha vibao viwili moto wa kuoteambali.
 Vibao hivyo ni 'Gunia la Mazoezi' na 'Nani Kaiona Kesho' ambavyo vyote viko katika albamu moja ya ‘Sarafina’ iliyofyatuliwa mwaka huohuo 2002 na ambayo ilikuwa na jumla ya nyimbo sita.
 Jumbe alidumu TOT kwa miaka miwili, akatoka na kwenda kujalibu upepo Msondo Ngoma Music alikokutana na wakongwe we dansi kama vile Muhiddin Gurumo na Tx Moshi William ambao kwa sasa wote ni marehemu.
 Akiwa na Msondo, Jumbe alifanya vitu vizito kwenye albamu iitwayo ‘Ajali’ aliposhiriki kuimba katika nyimbo zote akitumia ufundi wa njia ndogo ya sauti ujulikanao kitaalamu kama 'Minor' na kutunga vibao 'Transfer' na 'Sumu ya Ufukara'.
 Tofauti na wanamuziki wengine wengi wanapohama bendi kuikashifu, Jumbe anaisifu Msondo kwa kusema kuwa ni bendi ambayo wanamuziki wake hawana majungu, fitina wala nyoyo za chikichiki.
 "Msondo wenzetu wanapendana halafu lao moja, hawana majungu hata kidogo," anasema Jumbe anapoulizwa kuhusu bendi hiyo inayotumia mtindo wa 'Mambo Hadharani'.
 Hivi sasa, Jumbe ambaye ni baba wa familia mwenye watoto wanane na mkewe Zakhia Jumbe, anayekiri kuwa maendeleo katika muziki ni 'matokeo', amepata mafanikio makubwa hasa baada ya kuanzisha bendi yake.
Tayari Talent Band ina albamu tatu ambazo ni ‘Kwangu ni Wapi’, ‘Subiri Kidogo’ na ‘Kiapo Mara Tatu’, huku hivi sasa akiwa anapika albamu nyingine itakayokusanya vibao vikali kama ‘Nyumba ya Urithi’, ‘Kaolewa Ramadhani Kaachika Ramadhani’ na ‘Ukienda Kuomba Mboga’.  Ndani ya vibao vyote kwenye albamu zilizotangulia za Talent Band, Jumbe ameonyesha ukomavu mkubwa kisanii kuanzia ujumbe hadi ala na kumfanya afanikiwe kupata maendeleo makubwa zaidi ya alipokuwa mwajiriwa.

 

Saturday, August 16, 2014

MFAHAMU SHEM IBRAHIM KARENGA MTUNZI WA MUIMBAJI NA MPIGA GITAA

Shem Karenga
Hakuna mpenzi ama shabiki wa miondoko ya muziki, hususan wa dansi hapa nchini, asiyelifahamu jina la mwanamuziki mkongwe, Shem Ibrahim Karenga. Shem Karenga ametokea kuwa maarufu mno hapa nchini pamoja na mataifa kadhaa jirani, kutokana na umahiri wake wa miaka mingi wa kuimba na kucharaza gitaa kiongozi la Solo.
Wengine wengi wanamfahamu kupitia tungo zake mbalimbali zilizochangia kumpa umarufu, alizozifyatua akiwa na bendi hizi na zile, kama vile ‘Tucheze Segere’, ‘Muna’, ‘Kila jambo’ na ‘Mbelaombe’. Kutokana na kutambua mchango wake katika tasnia ya muziki wa dansi, blog hii leo imefunga safari hadi nyumbani kwake Buguruni kwa Madenge, jijini Dar es Salam na kufanya naye mazungumzo juu ya maisha yake ya kimuziki.

Shem Ibrahim Karenga, mkongwe wa muziki wa dansi Alizaliwa mwaka 1950, Bangwe, Kigoma na kupata elimu ya msingi katika shule ya kimishionari ya Kihezya kuanzia mwaka 1957 hadi mwaka 1964.
“Kiukweli, nilianza kujifunza muziki tangu nikiwa shuleni kwa sababu mimi nimesoma shule ya Wamishionari, sasa kule tulikuwa tukifundishwa fani hiyo,” ndivyo anavyoanza kusema Karenga.
Karenga anasema kuwa, baada ya kumaliza shule huku shetani muziki akiwa kampanda kichwani, mwaka 1964 alijiunga na bendi ya Lake Tanganyika Jazz ambayo maskani yake yalikuwa mjini Kigoma. Anakumbuka kuwa, aliingia Lake Tanganyika akiwa mwimbaji na mcharazaji wa gitaa la besi, ambako pia alikuwa na ujuzi wa kutengeneza gitaa kwa kutumia vifaa vya kuokoteza. Akiwa na Lake Tanganyika Jazz, aliyodumu nayo kwa miaka minane, alianza pia kujifunza vyombo vingine vya muziki kama vile; Drums, Kinanda, gitaa la Rithym na  la Solo’. 
Kutoka kushoto waliosimama Capy John Simon, Shem Karenga, Muhidin Gurumo, Juma Kilaza, Ally Rashid, Kassim Mapili na Salum Zahoro. Waliochuchumaa Nguza Viking, Mjengo,...
“Mwaka 1972, niliitwa kwenye bendi ya Tabora Jazz kama mwanamuziki mwenye kipaji cha utunzi, mwimbaji na mpigaji  wa gitaa la Solo, nilijiunga na Tabora Jazz nikiwa na vibao vyangu Dada Asha na Lemmy nilivyovitungia Lake Tanganyika, ambavyo vilinipa umaarufu mkubwa nilipo vipakua hapo Tabora Jazz'.
Anasema, Tabora jazz walimchukua akiwa Mtaalam wa muziki, ambako hata hivyo alipokuwa na bendi hiyo alikuwa akijiendeleza zaidi kwa masomo ya jioni kwenye shule ya Sekondari ya Milambo, Tabora pamoja na kusoma vitabu mbalimbali vya muziki.
Shem Karenga enzi za ujana
Katika Tabora Jazz ambako alikuwa pia kama Kiongozi wa bendi, Karenga alikutana na wakali wengine wa muziki kama vile Kassim Kaluona na
Athuman Tembo ambao kwa sasa ni marehemu pamoja na Salum Muzila.

Kutokana na sababu binafsi ambazo hakutaka kuziweka wazi, mwaka 1983 alijiengua kutoka Tabora Jazz na kusimama kabisa kujihusisha na muziki, ambako kilichofuatia ilikuwa ni kifo cha bendi hiyo.

“Mwaka 1990 niliondoka Tabora na kutua jijini Dar es Salaam nilikokutana na Baraka Msirwa katika mwaka huohuo na kuniomba nijiunge na MK Beats ili kuiongezea nguvu,” anasema Kalenga.

Ndani ya MK Beats iliyokuwa ndugu na bendi nyingine iliyotamba vilivyo enzi hizo, MK Group, Karenga alikutana na wakali kama Malik Star,
Sisko Lulanga, Fungo Shomari na Bwami Fanfan.

Baada ya kujiunga na MK Beats iliyokuwa ikitumia mtindo wa ‘Tukunyema’, Karenga aliisuka vema na kuinyanyua vilivyo hasa kwa vibao moto wa kuotea mbali vilivyozitetemesha vikali bendi nyingine
zote za wakati huo.

Mwaka 1995, MK Beats ilisambaratika, ambako mwaka uliofuata, yaani 1996 alianzisha bendi ya Tabora Jazz Star kwa kushirikiana na mtu
aliyemtaja kwa jina la Ibrahim Didi.

“Bendi ya Tabora Jazz Star ndio niliyo nayo hadi sasa nikiwa Mkurugenzi Msaidizi, ambako nafasi ya Mkurugenzi Mkuu imeshikiliwa na Didi mwenyewe,” anasema Kalenga.

Akizungumzia anavyouona ushindani wa kimuziki akiwa na bendi yake hiyo ya Tabora Jazz Star, Karenga anasema kwa upande wake mambo si mazito sana kwa kuwa ana mashabiki wake wa tangu huko nyuma.

Kwa upande wa mafanikio, Karenga anasema ukiondoa nyumba nzuri aliyoiporomosha nyumbani kwao Kigoma, anashukuru kuona ana marafiki wengi na anaishi atakavyo akiwa anamudu vema kuitunza familia yake.

Ushauri anaoutoa kwa wanamuziki na mashabiki wa dansi ni kuwa, wasibabaike kwani muziki huo ni wa kudumu, ambako hata hivyo anasikitika kuona kuna uhaba mkubwa wa vijana warithi wa miondoko hiyo
kwa sasa.

“Unajua, sisi tulirithi dansi kutoka kwa baba, kaka na wakubwa zetu wengine, lakini ni masikitiko makubwa kuona vijana wetu wa sasa wanarithi muziki hewa wa Bongo Fleva,” anasema.

Anasema, sababu ya kuuita muziki wa Bongo Fleva kuwa hewa ni namna wasanii wake wanavyopora midundo na ala kutoka nje huku wakijidai kuwa ni mtindo mpya wa muziki hapa nchini.

Mkongwe huyo anayebainisha siri yake ya kukubalika katika muziki kuwa ni bidii na juhudi za dhati kwenye fani hiyo, anasema anavutiwa na wasanii wote wanaofanya vema katika sanaa.

Kama ilivyo kwa wakongwe wengine wengi wa muziki, Karenga amefaulu kuwarithisha muziki watoto wake wawili wa kiume ambao ni Ramadhan na Mussa waliowahi kuwika vilivyo katika bendi ya TOT Plus.

“Mussa ni mwimbaji na rapa mahiri, ambako kaka yake, Ramadhan ni mcharazaji wa gitaa kiongozi, Solo,” anasema Kalenga, baba wa watoto sita.


Watoto wengine wa Kalenga ambao hawakubahatika kurithi kazi yake ya muziki ni Tausi, Biata pamoja na Rehana.


Sunday, July 6, 2014

KAMA KAWA EFM 93.7FM INAKULETEA MUZIKI ULITINGISHA ZAMA ZILE, LEO HEWANI TENA USIKOSEE

JUMAPILI NYINGINE NDIO NIMEMALIZA KUKUKUSANYIA NYIMBO NTAKAZOKUPIGIA LEO...LA BAMBA UNAJUA ILITOKA WAPI? DOUBLE OO, NA NYIMBO SITA AMBAZO N SURPRISE, SIKIA SAUTI YA MOSHI WILLIAM TX ALIPOKUWA MDOGO, MSIKILIZE TENA SKEETER DAVIS EFM 93.7FM KUANZIA SAA 2-5 USIKU LEO KWA WENYE INTERNET ANUANI NI HII http://tunein.com/radio/E-FM-Radio-937-s224740/