Friday, October 7, 2016

BURIANI SALOME KIWAYA


Picha iliyopigwa Uingereza wakati Salome alipoenda huko na Shikamoo Jazz Band. Toka Kushoto Marehemu Salome Kiwaya, Marehemu Papa Wemba, na Marehemu Bi Kidude Mungu awalaze pema.
Kwa masikitiko makubwa nimepokea taarifa za msiba wa Mama Salome Kiwaya, mwanamuziki mkongwe. Taarifa zilinifikia kuwa Salome amefariki katika ajali ya gari iliyotokea Dodoma sehemu za Meriwa. Nilimfahamu Salome kwa mara ya kwanza mwaka 1987, wakati nikiwa bendi ya Tancut Almasi Orchestra, tulipopiga kambi Dodoma Hotel kwa muda wa miezi mitatu, tukitoa burudani kwanza kwa wajumbe wa mkutano wa Kizota, kisha wenyeji wa mji wa Dodoma. Katika kufahamiana  kipindi hicho, tuliweza hata  kupiga wimbo wake mmoja ulioitwa Tuhina, uliokuwa ukiimbwa na Kasaloo Kyanga na Kyanga Songa, ambao nao ni marehemu. Siku moja nilipita mtaani Dodoma na kununua kanda za muziki wa Salome, nilizipenda sana nyimbo zake na nikamuahidi kuwa ningejitahidi kuzipeleka kwa watu wenye uwezo wa kuendeleza kazi zile. Nilizipeleka kanda kwa Ronnie Graham, Mscotch mmoja mwenye upenzi na uelewa mkubwa wa muziki wa Kiafrika na hasa rumba, na huyu Mscotch ndie aliyewezesha kuanzishwa kwa bendi ya Shikamoo Jazz Band. Baada ya kuzisikia nyimbo zile akaamua kuwa Salome asindikizane na bendi ya Shikamoo kwenye ziara yao ya Uingereza kama muimbaji wa kike. Salome alienda Uingereza na aliporudi ndipo alipoanza kununa vyombo na kuunda kundi la Saki Stars, ikiwa ni kifupi cha Salome Kiwaya Stars. Mume wake Mzee Kiwaya nae ni msanii maarufu aliyekuwa kiongozi wa kikundi cha Utamaduni cha CDA miaka hiyo ya 80. Kuanzia hapo nimekuwa karibu sana na Salome, miaka ya 90 wakati nikiwa Mwenyekiti wa CHAMUDATA, Salome ndie alikuwa mwenyekiti wa chama hicho katika mkoa wa Dodoma baada ya mkutano mkubwa wa wanamuziki uliofanyika mwezi June 1998, kule Bagamoyo, ambapo wanamuziki 265 waliweza kukusanyika pamoja na kukaa siku nne katika mji wa Bagamoyo wakifanya warsha za fani mbalimbali za muziki. Katika miaka ya karibuni Salome alishughulika na sanaa ya urembo akiwa wakala wa Miss Tanzania kwa kanda ya Kati na kuweza kutoa MIss Tanzania mmoja, baadae aliingia katika siasa na kufikia kuwa Mwenyekiti wa UWT wa Mkoa wa Dodoma, lakini aliendelea na muziki katika maisha yake yote.

Mungu Amlaze Pema Salome Kwaya. Ucheshi wako hatutausahau. 
JOHN KITIME

Friday, September 23, 2016

TANGA MJI ULIKOANZA MUZIKI WA DANSI


Wiki hii nilipata bahati ya kutembelea mji wa Tanga, mji ambao  sifa zake zilianza kusikika kuanzia enzi za utawala wa Wajerumani, jiji ambalo shule ya kwanza ya serikali ilijengwa hapa enzi hizo hizo za utawala wa Wajerumani, jiji ambalo liliendelea kukua sana kutokana na kilimo cha katani na hivyo kukusanya vijana toka kila kona ya nchi kuja kutafuta kazi katika mashamba makubwa ya katani wakati huo. Tanga mji ambao kutokana na uwingi wa vijana wakati huo, shughuli za burudani ya muziki nazo zilifikia kiwango cha juu kuliko sehemu nyingi Tanzania.
Ukizungumzia historia ya muziki wa dansi, huwezi kukwepa kuzungumzia Tanga, kwani historia inatueleza kuwa kabla ya kuanza vikundi vya muziki wa dansi kulianzishwa klabu za kucheza dansi. Klabu hizo zikitumia muziki wa santuri, wanachama wake walicheza na hata kushindana kucheza muziki kwa mitindo mbali mbali ya kigeni ikiwemo waltz, tango, chacha, rumba na kadhalika. Klabu za kwanza nchini zilianzia Tanga. Kulikuwa na klabu kama Young Noverty miaka michache baada ya vita ya kwanza ya dunia, wakati huo nchi ya Tanganyika ikiwa bado changa kabisa. Mtindo huu wa vilabu vya dansi ulienea na baadae kuingia Dar es Salaam na miji mingine iliyokuwa imeshaanza wakati huo. Vilabu hivi ndivyo baadae vikaanzisha vikundi vya kwanza vya muziki wa dansi. Hata majina ya vikundi hivyo vya kwanza yalihusiana na klabu za burudani za wakati huo. Kulikuwa na vikundi kama Coast Social Orchestra, Dar es Salaam Social Orchestra na kadhalika.  Hivyo mji wa Tanga ulikuwa katika ndoto za vijana enzi hizo. Kwa vile vijana wengi walikusanyika katika jiji hili nchi, kulianzishwa pia klabu ambazo zilikuwa kwa ajili ya vijana waliokuwa wakitoka kabila moja. Klabu hizo zikiwa na nia ya wananchama wao kusaidiana katika shida na raha, na vilabu hivi pia vilikuwa ni sehemu muhimu katika kutoa burudani kwa vijana waliotoka sehemu moja. Kati ya klabu hizi kulikuweko na klabu iliyoitwa Young Nyamwezi, kama jina lake lilivyo ilikuwa ni klabu ya vijana kutoka Unyamwezini. Hatimae mwaka 1955 klabu hii ilianzisha bendi yake iliyoitwa Young Nyamwezi Band, bendi hii ilikuja kukua na baada ya Uhuru ilibadili jina na kuitwa Jamhuri Jazz Band. Hakika kwa vijana waliokuwa wapenzi wa muziki miaka ya 60 na 70 ilikuwa lazima uifahamu Jamhuri Jazz Band, muziki wake, au kwa lugha ya enzi zile, ‘vibao’ vyake vilijulikana Afrika ya Mashariki nzima. Bendi hii ilikuwa ikibadili mitindo ya upigaji wake na kupiga katika mitindo ya ‘Toyota’ na hatimae ‘Dondola’. Aliyekuja kumiliki bendi hii, ambayo wapenzi wake pia waliita JJB alikuwa Joseph Bagabuje,  kulikuwa hata maelezo wakati fulani kuwa JJB ilikuwa kifupi cha Joseph Jazz Band na si Jamhuri Jazz band. Kama ilivyokuwa kawaida ya bendi za wakati ule Jamhuri Jazz Band ilisafiri sana na kufanya maonyesho katika kila kona ya nchi yetu, jambo hilo pamoja na kuwa bendi hii ilirekodi na kutoa santuri kupitia kampuni za kurekodi za Kenya na pia kurekodi nyimbo zake katika radio ya Taifa uliifanya bendi hii kuwa maarufu sana. Upigaji wa aina ya pekee wa gitaa la rhythm wa bendi hii, ambao uligunduliwa na Harrison Siwale, maarufu kwa jina la Sachmo, uliigwa na wapiga magitaa ya rhythm wengi nchini. Uimbaji wa kutumia waimbaji wawili tu, uliopendelewa na bendi za Tanga wakati huo ikiwemo bendi nyingine maarufu wakati huo, Atomic jazz Band, ulikuwa ni wa aina yake pia. Jamhuri Jazz Band pia ndio kilikuwa chanzo cha bendi maarufu ya Simba wa Nyika na bendi zilizozaliwa baada ya hapo. Nilibahatika kukutana mtu aliyekuweko siku ya kwanza ya safari ya kuja kuzaliwa kwa Simba wa Nyika, hakika ni hadithi yake ilikuwa ya kusisimua. Inasemekana kuwa siku hiyo Jamhuri Jazz Band ilikuwa imekodishwa kwa ajili ya kupiga kwenye harusi kule Muheza. Wanamuziki walikuwa wakilazimika kukusanyika katika jengo la klabu lililokuwa Barabara ya 15 ili kupata usafiri wa kwenda  Muheza. Siku hiyo wanamuziki wengine walikusanyika lakini George na Wilson Peter, Luza Elian a wengine wachache hawakuonekana, baada ya upelelezi mfupi ikajulikana kuwa wamejificha au wameondoka mjini Tanga, hivyo ikalazimika kutafuta wanamuziki viraka wa haraka haraka kuweza kufanikisha onyesho la siku hiyo, msimuliaji alinambia kuwa japo yeye hakuwa mwanamuziki bali shabiki tu wa bendi aliweza kupanda jukwaani na kuimba katika harusi hiyo, hali haikuwa mbaya kwani alijitokeza mteja mwingine akitaka bendi ikapige kwenye harusi yake pia, lakini ombi lake lilikataliwa kwani wanamuziki walijua kuwa hawakuwa kwenye kiwango chao. Na baada ya hapo kikaanza kipindi kigumu kwa Jamhuri Jazz Band kujitahidi kurudisha hadhi na ubora wa bendi, na pia ikaanza safari iliyokuja kubadili historia ya muziki wa dansi Afrika mashariki kwa vijana hawa waliotoroka kuelekea Arusha ambako walianzisha Arusha Jazz Band na hatimae kuvuka mpaka na kuingia Kenya ambako walianzisha Simba wa Nyika ambayo  mafanikio yake yanatingisha hisia za wapenzi wa muziki wa dansi mpaka leo.


Wednesday, September 14, 2016

JAMHURI JAZZ BAND


Kwa mara ya kwanza niliwaona 'Live', Jamhuri Jazz Band wakipiga katika ukumbi wa Community Centre Iringa, ukumbi maarufu kwa wenyeji wakati huo kwa jina la Olofea senta (Welfare Centre). Ni vigumu kuelezea jinsi nilivyokuwa najisikia kwani nilikuwa sidhani kama kutakuja kuweko na wanamuziki wanapiga vizuri namna ile. Lakini katika wote mpiga rythm guitar Harison Siwale, aliyejulikana kwa jina la Satchmo, alikuwa na anabakia kuwa mpiga gitaa aliyenifurahisha kuliko wote. Kwanza alikuwa na staili ya peke yake, na mpaka leo nikisikiliza nyimbo zake kama vile Blandina, Mganga no 1, Maria bembeleza mwana au Ewe ndege, nabaki kusifia kuwa huyu bwana alikuwa na kipaji cha pekee. Kuna rafiki yangu aliwahi kumuuliza wakati ule huwa anapataje mawazo ya kupiga gitaa lake kwa staili ile? alijibu kuwa huwa anajaribu kupiga sauti za viumbe mbalimbali wa porini katika gitaa lake.
Wanamuziki waliokuwa katika bendi ya Mkwawa High School,  Manji, Sewando, Danford Mpumilwa, Askofu Kakobe watakumbuka jinsi walivyoweza kupata nafasi ya kupiga pamoja na bendi hii kila ilipokuja Iringa mjini, maana hizo ndiyo zilikuwa taratibu wakati huo lazima bendi kubwa ikija, wanamuziki wadogo huomba Kijiko, na kama unaweza kuimba au kupiga vizuri unaachiwa nafasi ili muhusika akatafute mpenzi. Bendi ikifika katika mji, kama mji ule una bendi basi nao watapata nafasi ya kushirikiana na wageni.  Bendi hii ilianza kwenye miaka ya 50 ikiwa ikijulikana kama Yanga Nyamwezi Band, Kiukweli ilikuwa ni Young Nyamwezi Band, bendi iliyokuwa imetengenezwa kwa ajili ya Vijana toka Tabora waliokuja kukata mkonge katika mashamba ya mkonge yaliyokuweko Tanga miaka hiyo. Na baada ya Uhuru ikajulikana kama Jamhuri Jazz Band, kifupi JJB japo kifupi hicho baadae kilidaiwa kuwa kilikuwa kifupi cha jina mwenye bendi Joseph Bagabuje. Wakati wa uhai wa Jamhuri Jazz bendi Tanga kulikuwa kuna waka moto kwa vikundi maarufu katika Afrika ya Mashariki kuwa vyote katika mji huo. Atomic Jazz, Amboni Jazz, Lucky Star, Black Star. Kwa vyovyote Tanga ulikuwa mji wa starehe wakati huo, hasa ukikumbuka kuwa kulikuweko na bendi nyingine ambazo hazikuwa maarufu labda kutokana na aina ya muziki zilizokuwa zinapiga. Kama vile ile bendi ya Magoa The Love Bugs ambayo ndiyo hatimae ilikuja kuwa The Revolutions na sasa Kilimanjaro Band
Mbaruku Hamisi,Abdallah Hatibu, Zuheni Mhando

Eliah John, Alloyce Kagila, Musa Mustafa

Yusuf Mhando, Joseph Bagabuje, Rajabu Khalfani


George Peter, Harrison Siwale, Wilson Peter

Thursday, September 8, 2016

WESTERN JAZZ BAND MOJA YA BENDI ILIYOKUWA MAARUFU TANZANIA

Mzee Iddi Nhende ndiye aliyepata wazo la kuanzisha bendi maarufu ya Western Jazz. Iddi Nhende alianza muziki akiwa bado mdogo katika bendi ya shule alipokuwa Primary huko Nzega, mwaka 1944 alijiunga na Tabora Boys Secondary na hapa akajiunga na Brass Band ya shule ambapo alikuwa mpigaji wa Cornet. Alimaliza shule na kuja Dar es Salaam kujiunga na Chuo cha Afya, Sewa Haji Medical Training Center. Baada ya kumaliza mafunzo akaajiriwa Bohari ya madawa na kisha mwaka 1957 alihamishiwa Muhimbili. Upenzi wake wa muziki ulimfanya mwaka huohuo ajiunge na Rufiji Jazz Band kama mpiga trumpet, bendi hii wakati huo ilikuwa ikifanya maonyesho yake Minazini Community Centre iliyokuwa eneo linaloitwa siku hizi Mchikichini na pia walikuwa wakipiga muziki katika ukumbi wa Arnatougro.
Kutokana na miji kuwa ndio ilikuwa inaanza, watu wengi kutoka maeneo mbalimbali walihamia mijini na kujaribu kutafuta wenzao waliotoka sehemu moja na kuwa na vikundi vya kusaidiana au kuwaunganisha, watu wa sehemu mbalimbali walianzisha bendi wakazipa majina ya wanakotoka, hivyo waanzilishi wa Rufiji Jazz walitoka Rufiji, na ndivyo ilivyokuwa kwa Kilwa Jazz, Ulanga jazz na kadhalika. Hivyo Iddi Nhende aliyekuwa ametoka Nzega akaamua kuanzisha bendi ya watu kutoka Magharibi, kwa kuwa nchi ilikuwa imegawanywa katika majimbo, yakiweko majimbo kama Northern Province, Southern Highlands Province, Western Province na kwa vile Nhende alitoka Western province akaanzisha Western Jazz Band 1959. Akanunua vyombo aina ya Grampian toka duka la Souza Junior duka la vyombo vya muziki lililokuwepo mtaa wa Mkwepu. Aliweza kupata fedha baada ya kuuza ng’ombe kadhaa wa mamake. Wakati huo katika bendi za aina yake ni Dar es Salaam Jazz Band peke yake waliokuwa na magitaa ya umeme, hivyo Nhende akawa na kazi ya kuwatafuta wapigaji ambapo alimfuata mpiga gitaa la umeme wa kwanza Haus Dibonde(Msukuma), aliyekuwa anapigia Dar es Salaam Jazz Band(hii ilikuwa chini ya Mzee Muba), baada ya hapo akawapata wanamuziki wengine kutoka Ulanga Jazz Band, wakati huo chombo cha banjo kilikuwa muhimu hivyo akamtafuta mpiga banjo toka Cuban Marimba tawi la Dar es Salaam. Cuban Marimba wakati huo ilikuwa na tawi Dar Es Salaam lililokuwa chini ya Mzee Mwaipungu. Mwaka mmoja baadae alipata transfer ya kwenda Morogoro, hivyo huku nyuma alilazimika kuongeza wasanii ili kuimarisha bendi wakati hayupo. Akampata David Makwaya mwimbaji, na Ally Rashid(huyu ameacha muziki karibuni akiwa Msondo), mpiga Saxaphone toka Zanzibar. Bahati mbaya yule mpiga gitaa Haus akapata kichaa katika mazingira yaliyohusishwa na ushirikina kutokana na ushindani wa bendi uliokuwepo. Hivyo basi walifuatwa wanamuziki watatu toka Tabora Jazz, wanamuziki hao walikuwa wametoka pamoja katika bendi iliyokuwa na makazi Mwanza ikiitwa Kimbo Twist Band na wakahamia Tabora Jazz, na kutoka hapo wakachukuliwa na Western Jazz. Wanamuziki hao walikuwa
Rashid Hanzuruni, Kassim Mponda na Omary Kayanda. Baada ya kazi nzuri sana, Hanzuruni Nae akarukwa na akili katika mazingira yale ya yule mpiga solo wa kwanza akalazimika kurudishwa Tabora ambako alikaa mpaka mauti yake. Wema Abdallah akachukua nafasi ya mpiga solo katika bendi ya Western. Tatizo la kinidhamu lilifanya Wema aondolewe Western, na mpigaji mwingine mzuri sana Shamba Abbdallah akachukua nafasi, solo la huyu bwana linasikika kwenye nyimbo ka Rosa na kadhalika.
Hall la nyumbani la Western Jazz lilikuwa Alexander Hall, ambalo lilikuja kuwa hall la DDC Kariakoo. Western walinunua drums baada ya Kilwa Jazz kununua drums na kuzipitisha kwao kuwaringia. Walinunua toka kwa bendi moja ya Wagoa iliyoitwa De Mello Brothers. Western walirekodi santuri kadhaa chini ya mkataba waliyousaini na lebo ya Phillips ya Kenya. Hatimae Western na mtindo wao wa Saboso walitoweka katika anga za muziki miaka ya mwisho ya sabini. Kati ya nyimbo zao nyingi ni hizi hapa; Rosa, Vigelegele, Jela ya Mapenzi, Helena no 1 na 2.

Saturday, August 20, 2016

MAZISHI YA BI SHAKILA , YATAFANYIKA LEO MBAGALA CHARAMBE

Mazishi ya Bi Shakila yatakuwa leo Jumamosi 20 AGOSTI 2016. Mbagala Charambe, saa kumi alasiri Uwanja wa Ninja.
 Namna ya kufika msibani nyumbani kwa marehemu kwa kutumia daladala. Unapanda magari ya Mbagala Rangi Tatu, ukifika mwisho unachukua basi la Nzasa na unashuka Mnara wa Voda hapo unauliza kwa Bi Shakila utaonyeshwa

Thursday, February 25, 2016

MZEE KASSIM MAPILI HATUNAE TENA


Mzee mapili
MZEE Kassim Mapili hatunae tena. Habari ilitufikia jioni hii kuwa Mzee aliingia chumbani kwake Jumanne usiku akitokea kuangalia mechi ya Arsenal na Barcelona, na toka alipoingia hakutoka tena, hivyo jioni ya leo majirani walilazimika kutoa taarifa ambapo polisi walivunja mlango wa chumba cha Mzee na kukuta amefariki. Kutokana na hali ya mwili inaonekana alifariki tangu juzi na hali ya mwili si nzuri. Mzee Mapili alilazwa miezi michache iliyopita Muhimbili kutokan na kuwa na tatizo la moyo, lakini alikusema mwenyewe hata wiki iliyopita kuwa kutokana na kusaidiwa na Salma Moshi, msanii mkongwe anaeishi Marekani kupata Bima ya Afya hali yake imeimarika kwani anapata dawa zote zinazohitajika bila ya matatizo. Siku ya Jumatatu Mzee mapili alishiriki kikamilifu katika kumzika mtangazaji Fred Mosha, na hata kumuimbia marehemu akisikitika kuondoka kwake mapema. MUNGU AMLAZE PEMA MZEE WETU MAPILI

Monday, February 22, 2016

LEO NDIO SIKU YA MAZISHI YA RAFIKI YETU NA NDUGU YETU FRED CAMILLIUS MOSHA


FRED
RIP FRED MOSHA
  LEO NDIO SIKU YA MAZISHI YA RAFIKI YETU NA NDUGU YETU FRED CAMILLIUS MOSHA. FRED ALIKUWA MTANGAZAJI ALIYEKUWA NA MAPENZI MAKUBWA NA MUZIKI WA DANSI. MAPENZI YAKE YALIANZA TOKA AKIWA MDOGO KWANI NAMKUMBUKA AKIJA NA MAMA YAKE KATIKA MADANSI YA MCHANA AMBAYO BENDI YETU YA TANCUT ALMASI ILIKUWA IKIPIGA KWENYE UKUMBI WA OMAX KEKO. UPENZI HUU ULIFIKIA MPAKA KIPINDI ALITAKA KUACHA SHULE NA KUJIUNGA NA BENDI YA DDC MLIMANI PARK, BAHATI NZURI MAMA YAKE ALIIKAMATA BARUA YA MAOMBI YAKE YA KAZI, NA KUZUIA MPANGO HUO WA KUACHA SHULE. FRED HAKIKA ALIKUWA MTANGAZAJI BORA WA HABARI ZA WANAMUZIKI WA MUZIKI WA ZAMANI WA DANSI.
RATIBA YA MAZISHI NI KAMA IFUATAYO;
  • SAA 4-5 MWILI UTAPELEKWA NYUMBANI KWAKE CHAMAZI UKITOKEA MUHIMBILI
  • SAA 7 MWILI KUPELEKWA KANISA LA RC CHANG'OMBE KWA MISA YA MAZISHI
  • BAADA YA HAPO SAFARI ITAANZA YA KUELEKEA MAKABURI YA KINONDONI KWENYE MAKAZI YAKE YA MILELE
  • MUNGU MALAZE PEMA PEPONI FRED MOSHA

Tuesday, February 9, 2016

WAKONGWE WA DANSI TANZANIA KATIKA WIMBO WA PAMOJA- MIAKA 50 YA UHURU

VIDEO HII YA WIMBO HUU MIAKA 50 YA UHURU INA KUMBUKUMBU NYINGI. HAPA WAPO PAMOJA JUKWAANI, KASONGO MPINDA NA KABEYA BADU

Thursday, December 3, 2015

ABOUBAKAR KASONGO MPINDA KUZIKWA LEO KISUTU


MUTOMBO & MPINDA
Marehemu Aboubakar Kasongo Mpinda


MWANAMUZIKI Aboubakar Kasongo Mpinda aliyefariki jana jioni anategemewa kuzikwa leo saa kumi katika makaburi ya Kisutu. Mpinda alifariki jana nyumbani kwake Mwananyamala na mwili wake kwenda kuhifadhiwa katika hospitali ya Mwananyamala.
Mungu amlaze Peponi Pema

Wednesday, December 2, 2015

KASONGO MPINDA CLAYTON HATUNAE TENA


MUTOMBO & MPINDA
Marehemu Mutombo Audax (kushoto), akiwa na marehemu Kasongo Mpinda
HAKIKA siku hii ni ya simanzi, nimetoka makaburi ya Kinondoni ambapo tumemzika mwanamuziki David Musa Gordon wa Safari Trippers, nafika nyumbani taarifa inakuja kuwa mwanamuziki mwingine mkongwe Kasongo Mpinda Clayton amefariki jioni hii nyumbani kwake Mwananyamala na mwili umepelekwa hospitali ya Mwananyamala.
Mungu Amlaze Pema

Saturday, November 28, 2015

DAVID MUSA AFARIKI DUNIA


MWANAMUZIKI mwanzilishi wa kundi la Safari Trippers na aliyekuwa mwalimu wa wanamuziki wengi sana David Musa amefariki usiku wa kuamkia leo. Msiba uko nyumbani kwake Chang'ombe. Habari zaidi tutazileta kadri tutakavyozipata. 
safari trippers
Kushoto mwenye miwani David Musa, wa tatu Marijani Rajabu na kulia mwisho Jumanne Uvuruge mtunzi wa wimbo wa Georgina.
 Mungu amlaze pema

Monday, November 23, 2015

MFAHAMU MBARAKA YUSUPH MWANAMUZIKI WA NATIONAL PANASONIC NA POWER IRANDA

“NIMEACHANA na muziki wa dansi hivi sasa na nimeamua kugeukia sanaa ya filamu, ambapo sababu kubwa ni kupungua kwa kasi yangu ya ucharazaji gitaa, kutokana na kupata mara mbili kwa nyakati tofauti, ugonjwa wa kupooza.”
Hayo ni maneno ya Mbaraka Yusuph, kati ya wacharazaji mahiri wa zamani wa magitaa yote pamoja na Saxophone, aliyewahi kuzitumikia bendi mbalimbali hapa nchini, zikiwamo, The Smashers, National Panasonic, OSS ‘Power Iranda’, Seven Blind Beats na the Big Africa ya Arusha..ENDELEA HUKU