Tuesday, August 30, 2022

WOMAN JAZZ BAND BENDI YA MWAKA 1966, ILIKUWA NA WANAMUZIKI WANAWAKE KATIKA IDARA ZOTE

 

>
Josephine James akitumia brush kwenye drums, na Lea Samwel kwenye Bongos

Historia ya bendi ya wanawake inaanzia pale Rais wa Guinea ya Conakry, marehemu Sekou Toure alipotembelea Tanzania mwaka 1965. Rais huyu alipenda sana utamaduni wa nchi yake na kama ilivyokuwa kwa Mobutu alisisitiza kurudia uasili katika shughuli za utamaduni na akaufadhili kwa hali na mali, hata kuanzisha label ya muziki ya serikali. Na ilikuwa wakati wa Rais huyu mpenda sanaa vilipoanzishwa vikundi vya sanaa vya mikoa nchini mwake na kutokana na vikundi hivyo alitengeneza vikundi vya Taifa vya sanaa mbalimbali.
Mfano mzuri sana ambao wapenzi wa muziki wa dansi wa zamani watakumbuka ni Bembeya Jazz, bendi iliyopiga wimbo maarufu wa Whisky Soda, hii ilikuwa ni bendi ya mkoani lakini ikashinda mashindano na kuhamishiwa mkao makuu ya nchi na kufanywa bendi ya Taifa. Bendi hii iliyoanzishwa mwaka 1959 bado iko hai mpaka leo na inafanya maonyesho Guinea na nje ya nchi hiyo, inawezekana ndio bendi kongwe Afrika ambayo iko hai. Mwaka 1961 ilianzishwa bendi ya muziki ya polisi wanawake hukohuko Guinea, bendi hiyo ikaitwa L’Orchestre Feminin De La Gendarmerie De Guinee,   wakati wa Sekou Toure ikabadilishwa jina na kuitwa Les Amazones De Guinee na kuwa na wadhifa wa bendi ya Taifa.
 Wakati wa misafara yake Rais Sekou Toure alisindikizana na vikundi vya sanaa, na alipokuja Tanzania ndege yake ilikuwa na wasanii wengi kuliko wanasiasa, katika msafara huo alikuja na bendi hiyo ya kina mama Les Amazones. 


                                     Les Amazones de GuinĂ©e wakiwa kazini




Hiyo bendi ilipotua nchini, baadhi ya mabinti wa TANU Youth League, ndio wakapewa kazi ya kuwa wenyeji wa wanamuziki hawa wa kike. Baada ya siku chache Rais Sekou Toure na wasanii wake wakaondoka lakini  wakawa wamepanda wazo la vikundi vya sanaa vya Taifa na pia wazo la bendi ya wanawake. Wale mabinti waliokuwa wakizunguka na wanamuziki, wengi wao walikuwa ni wafanyakazi Government Press wakaazimia nao kuanzisha bendi ya wanawake, japo walikuwa  hawana ujuzi wa chombo chochote cha muziki, lakini nia yao ilikuwa kuwa na bendi kama Les Amazones.
Chini ya ufadhili wa TANU Youth League mabinti hawa wakaanza kuhudhuria mafunzo ya muziki, pale Police Mgulani chini ya mwanamuziki mahiri wa Polisi Mzee Mayagilo, baadae wakawekwa chini ya kitengo cha Polisi Jazz Band, ambako huko wakamkuta marehemu Mzee Kassim Mapili ambae akawa ndiye mwalimu wao mkuu. Hayawi hayawi yakawa hatimae tarehe 31 Mei 1966, bendi ya kwanza ya wanawake Tanzania, ikaingia katika studio za Redio Tanzania Dar es Salaam na kurekodi nyimbo, wakiwa wanapiga na kuimba nyimbo walizotunga wao wenyewe. Nyimbo hizo zilikuwa; Tumsifu Mheshimiwa
, Leo Tunafuraha, Mwalimu Kasema, Women Jazz, Sifa nyingi tuwasifu viongozi na TANU yajenga nchi. 


Kundi zima lililoingia studio lilikuwa na wanamuziki wafuatao kumi na tano:

1. Mary Kilima- Mwimbaji

2. Juanita Mwegoha-Mwimbaji

3. Siwema Salum- Mwimbaji

4. Rukia Hassan- Mwimbaji

5. Kijakazi Mbegu- Solo Guitar

6. Mwanjaa Ramadhan-Bass Guitar

7. Chano Mohammed-Rhythm Guitar

8. Tatu Ally-Alto Sax

9. Mina Tumaini-Tenor Sax

10. Anna Stewart-Alto Sax

11. Rukia Mbaraka-Tenor Sax

12. Lea Samweli-Bongos

13. Josephine James-Drums

14. Zainab Mbwana-Maracass

15. Tale Mgongo-Timing.

Baada ya hapo bendi ilianza kupata umaarufu mkubwa watu wakishangaa kuona kundi la wanawake wakiporomosha dansi bila sura ya mwanaume, bendi ikaanza kufanya maonyesho kwenye hafla mbalimbali za serikali na chama, na pia kuanza kuzunguka mikoa mbalimbali wakifanya maonyesho yaliyokuwa yakijaza kumbi. Sifa zikavuka mipaka na wakajikuta wakipiga na kujaza watu kwenye kumbi  mbalimbali Nairobi na Mombasa. Kutokana na urafiki uliokuwepo wakati huo kati ya Tanzania na China, ikafikia  hatua ya bendi hii kuonekana ni muhimu kwenda kufanya ziara China, lakini wakati wa matayarisho ya safari hiyo, bendi ikasambaratika. Kilichofanya bendi isambaratike ilikuwa ni kudhurumiwa mapato. Akina mama hawa walikuwa wakifanya maonyesho na yalikuwa yakiingiza fedha, lakini walikuwa hawapati chochote kutokana na maonyesho yao zaidi ya umaarufu. Ni bahati mbaya majina ya waliokuwa wakitumbua fedha za bendi hii bila kuwagawiya wanamuziki hawa kipato chao halali, ni wanaume wenye majina maarufu katika historia ya siasa za nchi yetu.  Kufikia hatua hiyo wanamuziki hawa wakaona ni heri kurudia  kazi yao ya awali Government Press kuliko umaarufu uliokosa fedha, jambo ambalo lilianza kuwaletea matatizo katika familia zao bila kuwa na sababu za msingi bendi ikasambaratika. TANU youth League ikachukua vyombo vyake na kuvihifadhi, hatimae vyombo hivi vikawa ndivyo vyombo vilivyotumika kuanzisha Vijana Jazz band chini ya Mzee John Ondolo miaka kadhaa baadae. Karibu akina mama wote wa bendi hii kwa sasa ni marehemu Mungu awalaze pema, lakini hakika walio hai wanastahili kupewa tuzo katika maazimisho ya siku za akina mama.

Sikiliza wimbo wao wa Tumsifu Mheshimiwa hapa