Friday, July 8, 2022

TUZIKUMBUKE BENDI ZETU 1


 Kuanzia miaka ya 1920 kuna taarifa za maandishi za kuwepo kwa vikundi vya muziki Tanzania. Tanzania Bara ikiwa na bendi nyingi za muziki wa dansi, wakati Tanzania visiwani Taarab ikitawala. Leo nataka niwazungushe mikoa mbalimbali ambako kulikuwa na bendi. Bendi nyingine zilikuwa maarufu mpaka kujulikana nje ya nchi yetu na nyingine hazikuwa maarufu au hazikudumu sana, lakini kuna wasanii wengi walitoka huko na kuja kuwa maarufu nchini na hata duniani.
Nianze na Kigoma, huu si mji ambao siku hizi unatajwa wakati ukiongelea muziki wa dansi lakini kulikuwa na bendi kadhaa kutoka mji huo zilizokuja kujitokeza, tuanze na Lake Tanganyika Jazz Band, hii ndiyo bendi alikotokea mpiga solo, mtunzi na muimbaji Shem Karenga, ambaye alianza huko akiwa mpiga gitaa la bezi na hatimae kuhamia Tabora jazz band ambako nyota yake ilianzia kung’ara hapo. Kigoma kulikuweko na bendi iliyoitwa Super Kibisa Jazz  Band, bendi hii ilikuwa na waimbaji wazuri na wapigaji wazuri sana, mmoja wa wapiga magitaa wa bendi hiyo Mzee Simba, hatimae alikuja kujiunga na JKT Kimbunga, bendi aliyokaa nayo mpaka alipostaafu. Pia kulikuweko na bendi iliyochukua jina la mji huo na kuitwa Kigoma jazz band, bendi nyingine iliyokuweko Kigoma iliitwa Kasababo Jazz Band, hii ndiyo ilikuwa bendi ya awali kabisa ya marehemu Shaaban Dede.
Mkoa jirani wa Mara ulikuwa na bendi nyingi pia, bila shaka ni vizuri kuanza na bendi ya Mara Jazz Band, hii ilipata umaarufu mkubwa ikiwa na mtindo wake wa Sensera. Lakini pia kulikuwa na bendi iliyochukua jina la mji wa Musoma, bendi iliyoitwa Musoma Jazz Band hii ilijitambulisha kwa mtindo wake wa Segese. Bendi nyingine kutoka mkoa huu ilikuwa Special Baruti Band, hii ndiyo bendi ya awali ya muimbaji maarufu Jerry Nashon kabla hajaingia jiji la Dar es Salaam. Musoma kulikuwa na bendi iliyokuwa mali ya Kanisa Katoliki iliyoitwa Juja Jazz band, hata kule Iringa kulikuwa na bendi nyingine mali ya Kanisa katoliki iliyoitwa VICO Stars ikiwa ni kifupi cha Vijana Consolata Stars. Bendi nyingine kutoka mkoa wa Mara ilikuwa ni Eleven Stars Band, japo ilijiita jina hilo, bendi ilikuwa na wanamuziki sita tu.

Tukiingia jiji la Mwanza, jiji lililokuwa likijisifu kwa starehe miaka ya sitini na sabini, kutokana na almasi, pamba na biashara ya mifugo, kulikuweko na bendi kadhaa ikiwemo Kimbo Twist Band ambako waliwahi kupita kati ya wapiga solo mahiri waliowahi kutokea Tanzania, marehemu  Rashid Hanzuruni na marehemu Kassim Mponda. Mwanza pia kulikuwa na bendi ambayo asilimia kubwa walikuwa ni wanamuziki kutoka Kongo, bendi hiyo iliitwa Orchestra Super Veya, bendi hii ilikuwa na umaarufu mkubwa kanda ya ziwa na ndiko alikopitia mwanamuziki maarufu Mzee Zahir Ally Zollo.
Mji wa Shinyanga kulikuwa na bendi maarufu iliyoitwa Shinyanga Jazz Band, bendi hii ilirekodi nyimbo kadhaa lakini wimbo wao mmoja unakumbukwa na wapenzi wa muziki wa dansi mpaka leo unaitwa Tenda Wema nenda zako. Wimbo huu ulitungwa na marehemu Mzee Zacharia Daniel Mabula, na kwa sababu ya wimbo huo mpaka kifo chake aliitwa Zacharia Tendawema au Mzee Tendawema, licha ya  historia yake ya kupitia bendi nyingi zikiwemo Western Jazz band, JKT Kimulimuli na TANCUT Almasi Orchestra ambako pia huko alitunga nyimbo nyingi, lakini  wimbo huo ulikuwa ndio nembo yake.
Tabora ulikuwa mji uliochangamka sana, kwanza ni moja kati ya miji ya zamani nchini, pili Tabora ulikuwa mji wenye vijana wengi kutokana na kuwa na shule  na vyuo vilivyokuweko katika mji ule. Kulikuwa na shule kongwe kama  Sekondari ya Tabora Boys na Sekondari ya Tabora Girls, pia vyuo kama Tabora Secretarial, chuo cha Ualimu cha Tabora, na chuo kikongwe cha reli,  Railway Training School. Hivyo basi Tabora nayo ilichangamka sana kimuziki, kulikuwa na bendi maarufu ya Tabora Jazz Band, na bendi yake dada, Nyanyembe Jazz band na pia ilikuweko bendi kongwe ya Kiko Kids. Wanamuziki wengi sana maarufu walitoka bendi hizi wakiwemo Shem Karenga , Wema Abdallah, Kassim Kaluona na Salum Zahoro, majina yaliyokuja kuvuma Afrika ya Mashariki na kati.

Mwaka 1972 Mzee Moses Nnauye aliteuliwa kuwa mkuu wa mkoa wa Singida, kutokana na kupenda kwake muziki haikuchukua muda mrefu akahakikisha Singida ikapata bendi nzuri iliyoitwa Ujamaa Jazz Band, bendi iliyokuwa ikipiga kwa mtindo iliyouita King’ita Ngoma. Wanamuziki kadhaa kama Waziri Ally, Selemani Mwanyiro walipitia bendi hii. Nikumbushe jambo jingine kuwa Mzee Nnauye alipokuwa mkuu wa wilaya ya Bagamoyo pia alianzisha bendi iliyoitwa Sabasaba Jazz band, mtindo wa bendi hiyo uliitwa Kizibo. Hamza Kalala alikuwa mpiga solo wa kwanza wa bendi hii, baada ya Mzee Nyange aliyekuwa mpiga solo wa Cuban Marimba kukataa wito wa kujiunga na bendi hiyo.


No comments:

Post a Comment