Thursday, March 17, 2022

MANENO Uvuruge mwanamuziki toka familia ya wapiga magitaa

 

Maneno Uvuruge

Kuna familia nyingine hutokea kuwa na wanamuziki wengi tu, mfano ni familia ya maarufu ya mwanamuziki marehemu Michael Jackson. Watoto wote wa familia hiyo walikuja kuwa wanamuziki maarufu, wavulana wakaweza kuanzisha kundi la The Jackson 5, baadae hata dada zao Latoya na Janet Jackson nao wakaja kujitokeza kuwa wanamuziki waliokuja kujipatia mafanikio makubwa katika fani hii. Kuna familia kadhaa zenye sifa hizo hata hapa Tanzania, kuna familia ya Kanuti, Muumba na Uvuruge ni mifano ya jambo hili. Leo tumzungumzie Maneno Uvuruge kutoka familia ya akina Uvuruge.

Maneno Uvuruge ni moja ya wanamuziki waliotoka katika familia ya wanamuziki ya ukoo wa Uvuruge. Kaka zake Jumanne, Stamili, na Huluka ni kati ya wapiga magitaa walioheshimika sana katika jamii ya wanamuziki wa bendi Tanzania.

Jumanne Uvuruge ambae alikuwa mkubwa wa akina Uvuruge wote, ndie aliyetunga kibao maarufu cha Georgina, kilichopigwa na Safari Trippers na kuimbwa na Marijani Rajabu. Siku zake za mwisho za maisha Jumanne alikuwa anajishughulisha na kupata riziki yake kwa kuzunguka kutoka baamoja na kwenda nyingine na gitaa lake  na kupiga maombi mbalimbali ya wanywaji. Hayakuwa maisha rahisi

Jumanne Uvuruge mtunzi wa wimbo maarufu wa Georgina uliopigwa na Safari TRppers na kuimbwa na Marijani Rajabu

Maneno Uvuruge hana kumbukumbu ya jinsi gani Jumanne alijifunza gitaa, lakini anajuwa kuwa kaka yake Stamili alifundishwa na Jumanne. Anakumbuka zaidi jinsi Huluka alivyojifunza kwani ndie alikuwa kaka yake waliefuatana kuzaliwa..

Stamili Uvuruge hapa akiwa jukwaani wakati akiwa bendi ya Bima Lee

 
Huluka alijifunza gitaa kwa kuanza kuchonga gitaa lake mwenyewe, aliiba mishipi ya kuvulia ya baba  na ndio zikawa nyuzi za gitaa lake, kila baba yao alipogundua wizi huo alivunja vunja gitaa na kumkataza asiguse mishipi yake tena, lakini akamwelekeza inakonunuliwa, Huluka alitafuta pesa na kwenda kununua mishipi na kuendelea na gitaa lake la kopo. Wakati huo Huluka alikuwa anasoma, naye Maneno akaanza hamu ya kutaka kujua kupiga gitaa akawa anaiba gitaa la kaka yake kila alipoenda shule, ilikuwa ni ugomvi kila alipokata nyuzi kwani alikuwa bado anajifunza. Jumanne na Stamili wakaanza rasmi kumfundisha gitaa Huluka nae akalijua vizuri sana. Si muda mrefu baadae nae akaanza rasmi kumfundisha mdogo wake

Maneno Kushoto akiwa na kaka yake Huluka

 
Maneno anasema wimbo wa kwanza kakake kumfundisha ni ile rhythm ya wimbo Novelle Generation wa Orchestra Lipualipua, wimbo huu ulikuwa ni kipimo muhimu kwa wapiga rythm enzi hizo. Mwanamuziki muimbaji marehemu Freddy Benjamin ndie aliyemshauri Maneno kujiunga na bendi. Alimkaribisha UDA Jazz ambako alikuwa akiimbia, ambako Maneno alijaribiwa kama ilivyokuwa kawaida wakati ule kwa mwanamuziki mgeni, lakini pamoja na kuweza kupiga gitaa vizuri alifanyiwa mizengwe na mpiga rhythm aliyekuweko na ambae pia alikuwa katibu wa bendi hiyo wakati huo. Baada ya hapo Freddy alimuombea kazi katika bendi ya Super Rainbow, bendi ambayo iliyokuwa na makao yake makuu pale Sunlight Bar Mwananyamala B. Na katika bendi hiyo Maneno akakutana na wanamuziki wakubwa wakati huo kama Hatibu Iteytey, Nuzi Ndoli, Rocky na Mzee Bebe. Wakati huu Eddy Sheggy ambaye alikuja kuipaisha bendi hiyo kwa wimbo wa Milima ya Kwetu alikuwa hajajiunga  na bendi hii wakati huo. Katika kipindi ambapo Maneno Uvuruge alikuwa akipigia Super Rainbow ndipo Eddy Sheggy na Emma Mkello walipojiunga. Katika kipindi hichohicho bendi iliyokuwa ikiongozwa na Tchimanga Assossa, Orchestra Mambo Bado ilipata msukosuko na kuvunjika kwa mara ya kwanza na hivyo wanamuziki wake Juma Choka mpiga drums, Lodji Mselewa na Nana Njige nao pia wakaja kujiunga na kundi na Super Rainbow, lakini hawakukaa sana Assossa aliweza kuifufua tena Mambo Bado na wote wakarudi wakifuatana na Maneno Uvuruge. Lakini tayari bendi ilikuwa iko katika hali mbaya kwani Assossa aliacha tena akiwa katika harakati ya kuunda bendi mpya na Mambo Bado ikafa rasmi..

Huluka Uvuruge akiwa jukwaani Msondo Music Group


Juma Choka akamtaarifu Maneno kuwa Urafiki Jazz kuna nafasi ya kazi na hapo akenda na kusailiwa na Marehemu Mzee Juma Mrisho maarufu pia kama Ngulimba wa Ngulimba, wakati huo Urafiki Jazz Band  nayo ilikuwa katika siku zake za mwisho lakini bado yule mpiga solo mahiri marehemu Michael Vicent alikuweko. Kipindi hiki pia waimbaji Mohamed Gota gota na Hussein Jumbe nao pia wakajiunga na bendi hiyo. Maneno Uvuruge sasa alianza kufahamika kwa wanamuziki wengine kuwa ana uwezo mkubwa wa kupiga gitaa na bendi zikaanza kumsaka, na kuanzia hapo amekuwa hatafuti kazi bali anatafutwa. Bendi ya kwanza kumchukua ilikuwa ni Maquis Original, alichukuliwa na bendi hii ili awe mpiga gitaa la rhythm, alijiunga na wapiga rhythm wawili mahiri Mbwana Cox na Omari Makuka. Akawa mwanamuziki wa Maquis wakati huo wapiga solo wa bendi hiyo walikuwa ni Nguza Viking, na Mzee Lubaba. Siku moja mwanamuziki Belly Kankonde akakutana na Marehemu Mzee Mwendapole aliyekuwa mmiliki wa bendi ya Afriso na wakamua kuipa uhai bendi ya Afrisongoma. Kankonde akawashawishi wanamuziki wenzie wanne wa Maquis, Maneno Uvuruge, Kiniki Kieto (mwimbaji), Comson Mkomwa (saxophone) na Keppy Kiombile(bass) wakahamia Afrisongoma.  Maneno hakukaa muda mrefu kwani Nguza alimfuata yeye na Comson na kuwarudisha Maquis , na kwa kuwa walikuwa wamekwisha pokea fedha za Mzee Mwendapole kesi ilifika polisi na ikalazimu Maquis warudishe fedha hiyo. Lovy Longomba kwanza alijiunga na Maquis nae hakukaa muda mrefu bendi hiyo, kwani Mzee Mwendapole akamshawishi akaunde upya kundi la Afrisongoma ambalo katika awamu ya kwanza liliishia kurekodi mara moja na kutokuwa na maendeleo. Lovy pia tena akamuondoaManeno Maquis kwa mara ya pili na kuhamia nae Afrisongoma. Wakati huo Mosesengo Fan Fan yule mpiga gitaa mahiri aliyetoka kwa Franco na kupigia Matimila na Makassy alikuwa amehamia Uingereza na akawa amemtaka Kiniki Kieto awashawishi Maneno Uvuruge, Keppy Kiombile, na Vivi Kapaya wamfuate huko Uingereza waweze kutengeneza kundi la muziki huko, lakini mpango huo uliishia kwa Kiniki na Vivi kuendelea na Fanfan wakati Maneno na Keppy wakahamia Afrisongoma wakiwa na Lovy. Wanamuziki kadhaa walihamia Afriso wakati huo wakiwemo Kalamazoo, na Mzee Mponda ambae baada ya kutoka Msondo alikuwa kapita Sikinde na akatua Afrisongoma. Na hapo ndipo msondo wakamchukua Maneno kwa mara ya kwanza. Alikaa kwa muda lakini rafiki zake akiwemo Benno Vila Anthony wakaweza kumshawishi ahamie Sikinde. Baada ya muda si mrefu Nguza akamfuata ili kumshawishi ajiunge na Orchestra Sambulumaa. Ilikuwa ni ushawishi wa Skassy Kasambula na Emmanuel Mpangala aliyekuwa mkurugenzi wa bendi ndio ulioweza kumfanya Maneno ahamie Sambulumaa......itaendelea


No comments:

Post a Comment