Saturday, September 7, 2013

UNAJUA KUWA MWANZONI MWA MIAKA YA 70 TAYARI BONGO KULIKUWA NA MWANAMUZIKI MNAIJERIA




Asubuhi ya leo nimepigiwa simu ambayo imenipa taarifa iliyobadili sana mtazamo wangu kuhusu historia ya wanamuziki wa Tanzania.
Nimepigiwa simu na aliyenipigia akajitambulisha kuwa anapiga simu kutoka Shirati Na kuwa aliwahi kuwa mwanamuziki zamani sana. Mheshimiwa huyu ambaye ananambia enzi hizo alikuwa akiitwa Papaa Kabaka alikuwa mpiga tumba wa bendi iliyokuwa inaitwa Geita Success, imekuwa ni mara yangu ya kwanza kujua kuhusu bendi hii. Kwa kadri ya Papaa Kabaka, bendi hii ilitokana na wanamuziki wa Kikongo waliotoka Orchestra Super Veya, bendi iliyokuwa na makao yake makuu jijini Mwanza na ilitamba sana katika Kanda ya Ziwa mwanzoni mwa miaka ya sabini. Ikumbukwe pia kuwa kuwa Super Veya ilitokana na kumeguka kwa Orchestra Fauvette, ambapo kundi jingine lilimeguka na kwenda kuweka makao yake Moshi na kujiita Zaire Success, na hatimae kupata tawi jingine lililojulikana kama Bana Afrika Kituli palepale Moshi.
Jambo lililonipamtazamo mpya wa historia ya wanamuziki wa Tanzania ni kuwa mpiga solo mmojwapo wa Geita Success alikuwa Mnaijeria ambae aliyenisimulia alikumbuka jina lake moja tu la Pius, ni mara ya kwanza kusikia kuwa kulikuwa na mwanamuziki kutoka Afrika Magharibi kuwepo nchini wakati huo, wengi wa wanamuziki wageni walitoka Kongo, na wengi kutoka kusini mwa nchi hii, Zambia, Zimbabwe, Malawi, na Afrika ya Kusini. Ni wazi kuna mengi yamejificha katika historia ya muziki wa nchi hii kutokana na kutokuwa katika kumbukumbu za maandishi.
Bendi hii ya Geita Success ilikuwa ikifanya maonyesho yake kwenye ukumbi wa Hostel za Council wakati huo, sijui kumekuweko na maendeleo gani ya ukumbi huo kwa sasa, hasa ukichukulia kuwa kumbi karibu zote za serikali nchini zimeguezwa matumizi, lakini hiyo ni makala nyingine kabisa.
Papaa Kabaka hakukaa muda mrefu Geita Success, japo kuwa anakumbuka kupokea bendi kamaJamhuri Jazz na hata Mbaraka na bendi yake na kama ilivyokuwa kawaida zamani bendi mwenyeji ilipiga nyimbo mbili au tatu na bendi wageni wakaendelea na show.
 Papaa Kabaka alihamia Mara Jazz ambako kadri ya aliyenieleza Ahmad Kipande pia alipitia bendi hii akawa akipiga solo na Abdallah Ndege Mkenya aliyetokea Kindu Jazz ya Kenya (hapa nina wasiwasi na kumbukumbu hii kuhusu Ahmadd Kipande kuna hitajika ushahidi zaidi, na pia kuna mkanganyiko je alikuwa kiongelea Mara Jazz au Musoma Jazz?) Baadhi ya wanamuziki wengine ambao walikuwa wakipiga kipindi hicho ni Sosi Nyabi akipiga rhythm gitaa na kuimba, Kimaya Obange akipiga Bass Gitaa. Aliyenipa taarifa hii kwa sasa anaitwa Simon Otieno ambaye kwa sasa ni Mchungaji pale Shirati

No comments:

Post a Comment