Sunday, April 14, 2013

FELIX MANUAKU WAKU..BABA YA WAPIGA SOLO WA KONGO WA KIZAZI KIPYA

FRANCO
FELLY
Namuheshimu sana marehemu Franco, lakini nadhani kama kuna mpiga gitaa aliyetoa mchango mkubwa sana katika muziki wa Congo katika miaka ya 70 na 80, nae ni mpiga solo Felix Manuaku.  Félix Manuaku Waku, ambaye hujulikana kama Pépé Fely au Felly ni mpiga gitaa kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Huyu bwana alipewa sifa ya kuwa mwanzilishi wa staili ya upigaji wa solo ambao ni maarufu katika upigaji wa muziki ulioko katika mahadhi ya Soukus. Felly alikuwa mmoja wa wanamuziki waanzilishi wa kundi lile maarufu la Zaiko Langa Langa, huku akaanzisha style ya upigaji wa solo wenye spidi kali vidoleni, staili ambao wapigaji kama Diblo Dibala(Machine gun), walikuja kujulikana sana kwa staili hiyo na kwa sasa ndio inatawala katika muziki wa staili ya Sebene. Kutokana na umahiri wake mkubwa wakupiga katika style iliyokuwa ngumu ya kutokuacha nafasi kati ya kipanda na kipande alipata sifa ya kuwa mwanamuziki mwenye ‘MKONO WA SHOTO MGUMU ZAIRE nzima. Mwaka 1979 Felly aliacha Zaiko na kuanzisha kundi jingine matata la Grand Zaiko Wawa. Hebu angalia na  kusikiliza kazi zake katika video hizi 

Baada ya kuweka picha ya Franco akiwa kijana,  mdau mmoja wa blog hii ametuletea taarifa hii..................



7 comments:

  1. Namkubali sana Pepe Fely. Hapo kwenye video ya juu kabisa naona anakung'uta solo bila plectrum. Fantastic stuff.

    ReplyDelete
  2. Mkuu Kitime hiyo video ya Manuaku Waku akiwa na Grand Zaiko ni lulu na hazina kubwa sana. Waimbaji kutoka kushoto ni Defao, Shimita, Djo Nickel na Djeffard. Hii ndio bendi iliyowatambulisha Defao na Shimita katika ulimwengu wa muziki.

    ReplyDelete
  3. Mkuu Balozi, huyu bwana Manuwaku Waku Le magicien ni kiboko ya yote kwa wapiga solo. Licha ya upigaji tu, huyu bwana ni mtunzi mkubwa sana. Huyu jamaa ndiye aliyekuwa kiongozi wa Zaiko toka 1972 - 1979, na aliachana na Zaiko kutokana na kuwa na mastaa wengi ambao kila mmoja alijitawala alivyotaka hatimaye Manuwaku akaona ujinga na kumwomba rafiki yake mkubwa Nyoka Longo kuwa anaondoka kutokana na hilo.

    ReplyDelete
  4. Bwana Kitime, ninapoangalia video kama hizi mimi hupatwa na uchungu sana kutokana na Tanzania kukosa kumbukumbu kama hii ya wanamuziki wake. Hizo video za Zaiko Langa Langa zilirekodiwa katika studio za televisheni ya Zaire mwaka 1976, hiyo ya Grand Zaiko Wawa ilirekodiwa mwaka 1984. Matokeo yake ni kwamba vizazi vya sasa na vijavyo vitaendelea kufaidi kazi za wanamuziki hawa kwa karne nyingi zijazo. Sisi Tanzania tuliambiwa na watawala wetu kuwa televisheni ni anasa na kwa ujinga wetu tulikubali. Kama tungekuwa na televisheni toka mwanzo, na sisi tungekuwa leo hii tunaangalia katika YouTube video za muziki live zilizorekodiwa miaka mingi iliyopita za wanamuziki wetu mahiri kama Marijani Rajab, Mbaraka Mwinshehe na wengine wengi.

    ReplyDelete
  5. Video ya katikati waimbaji kutoka kushoto ni Lengi Lenga 'Ya Lengos', Mbuta Mashakado, Nyoka Longo na Likinga Redo. Video ya chini waimbaji kutoka kushoto ni Lengi Lenga, Bimi Ombale, Nyoka Longo na Mbuta Mashakado. Mpiga drum katika video zote mbili ni Ilo Pablo Bakunde. Hii ni Zaiko Langa Langa iliyoundwa upya katikati ya miaka ya sabini baada ya kuondoka akina Papa Wemba, Bozi Boziana na Evoloko Jocker. Bimi Ombale, Mbuta Mashakado na Ilo Pablo walifariki mwaka 2011. Hiyo picha ya Manuaku Waku akiwa amevaa kofia nyeusi hapo juu ilipigwa Kinshasa wakati wa mazishi ya Mashakado.

    ReplyDelete
  6. Manuaku Waku ni sababu kuu ya Zaiko Langa Langa kuwa na mlolongo wa wapiga solo hodari na wenye vipaji vya hali ya huu kuliko pengine bendi yoyote DRC. Baada ya Manuaku kujitoa Zaiko Langa Langa viatu vyake vilivaliwa na Roxy Tshimpaka 'Le Grand Niaou' aliyetokea bendi ya Bana Ngenge. Roxy aliondoka Zaiko 1982 na kurithiwa na Beniko Zangilu 'Popolipo'. Beniko aliondoka 1988 na nafasi yake kuchukuliwa na vijana wawili matata sana Shiro Mvuemba na Baroza Bansimba. Bendi pia ilikuwa na wapiga solo wengine ambao hawakuvuma sana lakini walitoa mchango mkubwa. Hawa ni Matima Mpiosso na Petit Poisson.

    ReplyDelete
  7. Mkuu Kitime nimekubali Fely ni kiboko. Mimi najifunza gitaa na ninabaki kushangaa mambo anayoyafanya katika huo wimbo Salima akiwa na Grand Zaiko.

    ReplyDelete