Wednesday, December 21, 2011

Koka koka Sex Battalion- Vijana Jazz

Siku ya Alhamisi tarehe 2 Januari mwaka 1975 kundi zima la Vijana Jazz Band waliingia katika studio za Hi-Fi, jengo la Pioneer House katika jiji la Nairobi, waliingia studio na kurekodi nyimbo 6. Lakini katika mpango huu ambao ni wazi haukuwa na baraka za muajiri wao (Tanu Youth League),  kundi hili lilijiita Koka koka Sex Battalion. Nyimbo hizo karibuni zimetolewa katika CD na kampuni Uingereza  ya Sterns. Mchezo kama huo ulikuja rudiwa tena mwaka 1981, wakati baadhi ya wanamuziki kutoka Mlimani Park walipokwenda Nairobi na kurekodi nyimbo kadhaa zikiwemo, Nawashukuru wazazi wangu, Nalala kwa tabu, Bubu ataka kusema, wakitumia jina la Black Warriors. Baadhi ya nyimbo za Koka koka Sex battalion ni Niliruka ukuta, Magdalena na Kokakoka. Ni wazi kuwa Vijana jazz walitumia  jina la Kokakoka Sex Battalion kwa kuwaiga Orchestra Sosoliso, ambao waliwahi kutoa kibao kilichoitwa Sex Madjesi, na wao wenyewe kuanza kutambulika hivyo. Wakati huu wana Koka koka walikuwa wanaiga vitu vingi toka kwa Orchestra Sosoliso, hata gitaa la solo katika wimbo wa Niliruka ukuta liliigwa kutoka nyimbo moja ya Sex Madjesi. Ukitaka kupata vionjo vya CD hiyo bofya hapa

3 comments:

  1. Mkuu,

    Hii Cd n'shaitia mkononi. Naisikiliza huku nalambalamba mdomo kwa raha zangu!

    Mkuu, hili dokezo kwamba Vijana walikuwa wanachukua vionjo vingi toka kwa Sosoliso leo nitalifanyia kazi. Sijui kwa nini hata Sikinde nikiwasikiliza naona kuna vionjo kibao vya Orchestra Veve!?

    Kwa bahati nzuri nina CD ya Sosoliso. Mwaka 2007 nilikwenda kuzurura Paris, Ufaransa nikapita Fnac recordshop. Basi ile nimeingia section ya Afrika CD ya kwanza kukumbana nayo ilikuwa Trio Madjesi ya Sosoliso. Aaghhhh! kitendo bila kuchelewa nikaitia mkononi (Siyo siri Mama watoto ilibidi aniburuze nje ya duka huku kakunja ndita kwa sababu Fnac Recordshop walichukua mpaka senti kumi yangu ya mwisho maanake niliondoka na CD zaidi ya ishirini). Kwenye hiyo CD ya Trio Madjesi kuna hit zote za Sosoliso; Photo ya Madjesi 1&2, Mama tika ngai nalembi,Cinema, Sex Madjesi 1&2, Moussa Photo na yo, Il est Mechant, Carte Blanche 1&2, Lomeka na Moseka. Hii CD inanikumbusha sana miaka ya kati 1970 enzi za mabitozi, laizoni, mapekosi, slim fit na kofia za Jackson 5!

    Mdau, Sokomoko Damu, Helsinki, Finland.

    PS/ Mkuu rejea tuliyozungumza kwenye simu Jumatatu ile link ya ile issue ya RTD hii hapa:
    http://www.youtube.com/watch?feature=player_embedded&v=7SOQNtIslg4

    Au ingia youtube halafu andika:
    Link Tanzania Heritage Project

    Warning:
    Ukishaangalia usije ukapata BP, au Depression, au Ukapandwa na Hasira, au Ukasikitika, au Ukaogopa, au Ukapata Wazimu kabisa.

    ReplyDelete
  2. “Nenda upesi, nenda ukamwabiee,
    Tokea leo, asinifwatefwate,
    Kitendo kile, alichonitendea,
    Kingeniponza, nipoteze maisha.
    Kunidanganya kwamba hajaolewa, na chumba kile amekipanga yeye,
    Kumbe uwongo, Alenidanyaa.
    Ilipofika saa nane za usiku, nikasikia hodihodi fungua,
    Bahati nzuri, nikaruka ukutaa…

    …kama ukifika mwambie ajirekebishe, mambo kama yale mabaya na yana hatari…”


    We acha tu.

    ReplyDelete
  3. Ukweli ni kwamba ni lazima ujufunze kwa mwalimu na ndiyo maana miziki ya Tanzania na congo ya miaka ya zamani ilikuwa ni mitamu na mpaka sasa ukisikia oss ,ddc,makassy vijana jazz jazz au uda utapenda kusiki mpaka asubuhi ni sababu msingi wa mziki wa dansi uko kwenye rumba na hiyo rumba ndugu zetu wakongo na ndugu zetu watanzania walikuwa wanatafuta kila njia ya kuweza kutoka kivyao na kutambulika kipekehe kwa mfano ddc ni kweli stahili yao ilikuwa sawa sawa na veve hasa kwenye midomo ya bata ukija msondo tpk ok jazz ukija maquiz ilikuwa sawa sawa na afriza ilikuwa ni mojawapo ya mashindano yaliyoweza kuinua wanamuziki wengi wa kitanzania nawatanzania wenye asili ya kicongo ni tofauti na leo weli cd nimeinunua hapa uk hmv na inautamu wa ali ya juu ambo mimi mchunguzaji wa miziki imenipa furaha moja ya ajabu ,ninachosema hapa muziki wa tanzania pamoja na kukosa studio wakati huu bado uko juu hawa vijana wa leo itawachulia muda kufiki uwezo wa bendi za zamani,
    bwana kitime tunashukuru sana.

    ReplyDelete