Saturday, October 2, 2010

Atomic Jazz Band




Atomic ilikuwa moja kati ya bendi zilizowika sana nchi hii. Bendi iliyokuwa na makazi yake Tanga, Tanga wakati huo ikiwa na vikundi vingi maarufu vya muziki, kama vile Jamhuri, White Star, Amboni, Lucky Star, Black Star. Bass katika bendi hii kwa kweli lilikuwa likiingiza upigaji wa bezi katika kiwango kipya,wapigaji wake walileta changamoto hata walipokuja hamia katika bendi mpya. Pichani toka kushoto John Mbula -Saxophone,Rodgers- mwimbaji, John Kilua-Thumba(huyu alikuwa ni ndugu ya Julius Kiluwa ambaye ndiye alikuwa mwenye bendi),John Kijiko-Solo gitaa, Hemed Mganga-rythm gitaa (niliwahi kupiga bedni moja na mzee Mganga kwa wakati fulani. Tulikuwa wote Orchestra Makassy na ndie baba mzazi wa mwimbaji wa kizazi kipya Kassim Mganga),Mohamed Mzee-Bass.
Picha hii ilikuwa ni jarada la santuri iliyokuwa na wimbo maarufu Mado Mpenzi Wangu. Wimbo ulikuwa ni ujumbe wa kweli kutoka kwa mwanamuziki mmoja kwenda kwa mpenzi wake ambae jina kidogo linafanana na Mado ili kuficha ukweli. Mtunzi wa wimbo huu alikuwa mpenzi sana wa bendi hii na bado kwa rafiki zake anajulikana kwa jina la Mado. Siku hizi amekuwa mpenzi tu wa kawaida wa muziki.

No comments:

Post a Comment