Tuesday, July 10, 2012

Tanga Taarab, waanzilishi halisi wa modern Taarab


Waziri Ally akipiga kinanda Lucky Star
Katika miaka ya 50 wanawake tisa wa Tanga walijikusanya na kuanzisha  kikundi cha kuimba walichokiita Raha til Fuad maana yake Raha ya Moyo. Akina mama hawa chini ya bibie aliyeitwa Mama Akida au aka Mama Lodi, waliendesha kikundi chao wakiwa wanaimba nyimbo za Siti Binti Sadi na tungo zao ambazo waliimba katika melody ya nyimbo za kihindi zilizotamba wakati huo. Kundi hili liliendelea na kuanza kuruhusu wanaume kujiunga hasa wakiwa wapiga vyombo, akiwemo mtoto wa Mama Akida, Akida Jumbe hatimaye alijiunga na kundi hili kama mpiga accordion kwenye mwaka 1962. Kundi hili ambalo baadae lilikuja kuitwa Young Noverty, liliendelea mpaka kukaweko na mgawanyiko uliozaa kundi la Shaabab Al Waatan. Hapa ndipo kukaanza mtindo wa kuweko kundi pinzani jambo ambalo kwa njia ya ajabu sana likawa linadumu kiasi cha miaka kumi kumi. Miaka ya 1960s Young Noverty na Shabaab al Waatan, miaka ya 1970 Lucky Star Musical Club na Black Star Musical Club, miaka ya 1980 Golden Star Taarab na White Star Taarab, miaka ya 1990, Babloom Modern Taarab na Freedom Modern Taarab. Taarab ya Tanga ndo haswa inastahili kuitwa modern Taarab, kwani wao hawakufuata taarab ile iliyoletwa Zanzibar enzi ya Sultan Seyyid Barghash, makundi la taarab ya Tanga yalikuwa  madogo na vyombo vyake vilikuwa pamoja na Gitaa la besi, gitaa la solo, drums bongos ,akodion au kinanda, nyimbo zao zilikuwa fupi na si ndefu kama za Kizanzibari., nyimbo zilitegemea mipigo ya ngoma za asili za kumbwaya na chakacha na hata baadaye mitindo kama rumba,bossa nova ilitumika kama mapigo. Na Taarab ya Tanga ndio iliyoanzisha moto wa vikundi vya taarab Tanzania Bara. Moshi kulikuwa na New Alwatan, AzimioTaarab, na Blue Star Taarab , Arusha-Blue Star Taarab, Dodoma-Dodoma Stars, Kondoa –Blue Stars, Mbeya-Magereza Kiwira, Mwanza-Ujamaa Taarab, Bukoba wakiwa na Bukoba Stars, na muendelezo huu uliingia mpaka Burundi kutokana na mwana muziki mmoja alie julikana kama Athmani Mkongo, alitoka Burundi na bendi yake kufika Tanga akawa mwanamuziki mahiri wa Taarab na hata kuipeleka kwao Burundi na kukaanzshwa huko vikundi kadhaa vya Taarab.

4 comments:

  1. Kitine wewe nihazina, maana habari kama hizi tungezipata wapi, jamani blog zinasaidia na hasa za watu kama hawa ambao wanatupa vitu vyenye kujenga, kuelimisha na kutukumbusha, Tupo pamoja mkuu

    ReplyDelete
  2. Kitine kazi yako ni nzuri sana. Asante. Ombi langu ni kuwa; makala hizi ziambatane na nyimbo zao. Kwa makala hii weka za Black Stars na Lucky Stars; sauti za Bi Shakila na Bi Sharmila ziko so unique.

    ReplyDelete
  3. Duuh!

    Eee bwana Kitime huyo anaepiga KII BOD ni KIIZINJA?

    Duh! Watu wanatoka mbali!

    ReplyDelete