Thursday, December 22, 2022

WASIFU WA MAREHEMU RAMADHANI KINGUTI - KINGUTI SYSTEM

 


Marehemu Ramadhan Maulid Kinguti maarufu kama Kinguti System ni mzaliwa Ujiji, Kigoma. Alikuwa mtu aliyependa sana utani na ucheshi.

Bendi yake ya kwanza aliyojiunga mwaka 1977, ilikuwa Super Kibisa iliyokuwa na makao yake makuu Kigoma. Super Kibisa  ni bendi iliyoanzishwa mwaka 1968 pale Kigoma. Mwaka 1977 kiongozi wa bendi alikuwa Mlolwa Mussa Mahango ambaye alikuwa ni binamu yake Ramadhani Kinguti, na  hivyo ikawa rahisi  kwake kujiunga na bendi ile. Super Kibisa ilikuwa mali ya watu watatu, Gollo Saidi, Haruna Mahepe, na Maulidi. Katika bendi ya Super Kibisa, kipaji cha utunzi cha Kinguti kilianza  kujitokeza mapema na aliweza kutunga nyimbo kadhaa kama vile Kazi ni uhai, Mapenzi tabu,na Zaina.

Miaka miwili baadae, 1979, Kinguti alichukuliwa na Ahmed Sululu ambae alikua Katibu wa bendi ya  Dodoma International na kuhamia Dodoma. Dodoma International ilimchukua Kinguti ili kujaza nafasi ya Shaaban Dede ambaye alikuwa kahama bendi hiyo na kuhamia JUWATA.

Alipofika Dodoma international , Kinguti  alikutana kwa mara ya kwanza na mpiga gitaa mahiri marehemu Kassim Rashid. Kinguti aliiacha Dodoma International Orchestra na kujiunga na  Orchestra Makassy ambapo wakati huo walikuweko wanamuziki akina Marehemu Masiya Radi, mwimbaji  Mkongo ambaye alifariki kwa kukanyagwa na daladala maeneo ya Kinondoni Mbuyuni. Baadhi ya wanamuziki wengine ambao Kinguti alikuwa nao alipokuwa Orchestra Makassy walikuwa marehemu  Remmy Ongala, marehemu Andy Swebe, Keppy Kiombile, John Kitime, marehemu Issa Nundu, marehemu Kyanga Songa, Choyo Godjero na wengineo, pia alikuweko marehemu Aimala Mbutu kwenye solo, na Kassim Mganga (babake wa mwanamuziki wa Bongo flava Kassim Mganga-Milionea wa Mahaba) kwenye rhythm, na wengine wengi.  Kwa kipindi fulani muda huu Kinguti akiwa na wenzake chini ya Mzee Makassy wakafanya ziara ndefu nchini Kenya, kati ya waliokuwepo katika safari hiyo ni Nico Makoli,  Keppy Kiombile, Andy Swebe, Mzee Aimala Mbutu, Mzee Liston na wengine wengi akiwemo Mzee makassy mwenyewe.

1986 alijiunga Afrisongoma chini ya Lovy Longomba, hapa alitunga nyimbo kadhaa kama Pesa ni maua, Amana mpenzi, Estah Usituchonganishe, waimbaji wakati huo walikuwa Kinguti, marehemu Lovy Longomba  na Anania Ngoliga, kwenye solo alikuweko marehemu Kassim Mponda, na rhythm Maneno Uvuruge. Kwa muda mfupi alikuwa DDC Mlimani Park, na hapa akatunga kile kibao maarufu Visa vya mwenye nyumba, ambapo aliimba na Hassan Bitchuka, Francis Lubua, Hussein Jumbe na Benno Villa. Mwaka 1989 alikuwa moja ya wanamuziki waanzilishi wa Bicco Stars Band akiwa na Mafumu Bilali, Asia Darwesh, Andy Swebe, Mzee Aimala Mbutu, walitikisa na vibao kama Muuza chips, Leyla, Magreth maggie, Kitambaa cha kichwa, Nyumba ya kifahari, na nyingine nyingi tu. 1999 alijiunga na kilimanjaro Connection, alikaa bendi hii iliyokuwa chini ya Kanku Kelly kwa miaka miwili kisha kuanzisha bendi akiwa na Hassan Shaw, bendi iliyoitwa The Jambo Survivors ambayo wengi hapa Tanzania wataikumbuka kwa kibao cha Maproso. Bendi ya Jambo Survivors ikiwa bado na Ramadhan Kinguti na Hassan Shaw, kwa miaka kadhaa ikahamia Thailand. Baada ya kurudi Thailand afya ya Kinguti ilikuwa na migogoro mingi hivyo hakurudi tena kwenye muziki na muda mwingi alikuwa Dar es Salaam kisha Kigoma.

Ramadhani Kinguti amefariki tarehe 21 Disemba 2022 katika hospitali ya Maweni Kigoma, na mazishi ni tarehe 22 Disemba 2022 hapohapo Kigoma

Mungu amlaze Pema.

3 comments:

  1. RIP Ramadhani Kinguti System Tulikupenda lakini Mwenyezi Mungu amekupenda zaidi

    ReplyDelete
  2. Kingugi system mkongwe wa muziki wa dansi hapa Tanzania tunamwombea mwanga wa milele Mungu amwangazie na akawasalimie Sana hakina shabani Dede, Eddy sheggy na wengi wengineo

    ReplyDelete
  3. 🙏🏾Pumzika kwa amani Ramadhan Kinguti.Amina.
    Safari yetu sote.😞

    ReplyDelete