Friday, October 14, 2022

VERCKYS KIAMUANGANA MATETA AFARIKI DUNIA

 

Verckys

Mpiga saksafon maarufu Afrika, Verckys amefariki dunia jana Alhamis tarehe 13 Oktoba 2022, baada ya afya yake kuwa tete kutokana na kupata stroke ndogo miezi michache iliyopita. Verckys ameacha watoto 32.

Georges Kiamuangana Mateta maarufu kwa jina la Verckys alizaliwa Kisantu katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo  terehe 19 Mei,1944.
Alijipa jina la Verckys kimakosa kwani alitaka kujiita jina la mpiga saksafon maarufu wa Kimarekani wakati ule aliyeitwa King Curtis. Kwa bahati mbaya alisikia jina  "Curtis" kama  "Verckys."  Na wote mpaka leo tunamfahamu kama Verckys. 
Baba yake Verckys alikuwa mfanya biashara tajiri, hivyo Verckys aliweza kupata elimu nzuri kabisa. Mapema kabisa alionyesha umahiri kipaji chake cha muziki kwani alikuwa akifahamu kupiga vyombo kadhaa vya kupuliza kama vile filimbi na clarinet, hatimae alianza kujifunza saksafon alipokuwa kwenye kikundi cha madhehebu yaliyokuwa chini ya mchungaji maarufu wa Kikongo aliyeitwa Nabii Simon Kimbangu.

Mwaka 1962 alijiunga na bendi iliyoitwa Los Cantina, baadae akahamia Jamel Jazz na mwaka huohuo safari yake ikamfikisha kwenye kundi la Conga Jazz lililokuwa chini ya mkongwe mwingine maarufu katika muziki wa Kongo aliyeitwa Paul Ebengo, maarufu zaidi kwa jina la Dewayon. Mwaka 1963 akahamia O.K. Jazz in 1963, kundi lililokuja kumtambulisha rasmi katika ulimwengu wa muziki.  Alikuwa mpuliza saksafon mzuri sana kiasi cha  kupewa sifa ya kuwa ‘Mtu mwenye mapafu ya chuma’, akawa mtu wa karibu sana na Luambo Luanzo Franco Kiongozi wa OK Jazz.

Mwaka  1968, Franco akapata ziara ya kwenda Ulaya, akachukua baadhi ya wanamuziki na kwenda nao, huku nyuma  Verckys na muimbaji  Youlou Mabiala wakakusanya wenzao na kufanya mazoezi ya haraka na kuingia studio na kurekodi nyimbo nne. Kasheshe kubwa lilizuka baada ya Franco kurudi kutoka ziara yake na hatimae tarehe 5 April 1969, Verckys alilazimika kuacha  OK Jazz  na kuanzisha kundi lake mwenyewe aliloliita Orchestre Veve.
Kundi hili likuwa na waimbaji vijana machachari sana,  kati yao walikuweko  Matadidi Mabele maarufu kwa jina la Mario,  Marcel Loko maarufu kwa jina la Djeskain, and Bonghat "Sinatra" Tshekabu aliyekuwa maarufu kwa jina la Saak Saakul. Vijana hawa baadae walikuja kumkimbia Verckys na kuanzisha kundi lao lililokuja kutikisa mpaka bendi kongwe za wakati huo, kundi hili liliitwa Orchestra Sosoliso na umoja wao walijipa jina la Trio Madjesi .

 Turudi kwa Verckys, yeye na kundi lake la Orchestre Veve lilikuja kurekodi nyimbo nyingi sana maarufu, nyimbo zake pendwa za kwanza zilikuwa Mfumbwa, Bankonko Baboyi na wimbo ambao ulikuwa utunzi wa Saak Saakul ulioitwa Fifi Solange. Mafanikio makubwa aliyokuja kuyapata Verckys yalimuwezesha  kuingia rasmi katika biashara ya muziki kwa kuanzisha label yake na kuingia mikataba na bendi mbalimbali maarufu wakati ule. Baadhi ya bendi zilizotoa nyimbo ambazo kwa lebo hiyo ambazo  zilikuja kutikisa Afrika nzima zilikuwa, Les Grand maquisards, Orchestra Kiam ambayo jina lake Kiam lilikuwa ni ufupisho wa jina Verckys la Kiamuangana, Orchestra Bella Bella ya wale ndugu wawili waimbaji, Soki Vangu na Soki Dianzenza, Orchestra Lipua lipua, Les Kamale, na Empire Bakuba ya Pepe Kalle.
Mwaka 1972 Verckys alifungua studio yake  katika kituo alichokiita Veve Center. Alianza kufanya mambo mengi makubwa katika muziki, hili liliwezesha mwaka 1978 apate kuchaguliwa kuwa rais wa wanamuziki wa Zaire,  baada ya Franco Makiadi kumaliza muda wake.
Historia ya Verckys kwa kifupi imejaa mafanikio makubwa  kimuziki. Akiwa na miaka 18 alijiunga na kundi konwe la OK Jazz, alipofikia umri wa miaka 25 alifungua studio yake ya kurekodi muziki.  Mwaka 1972 alimshirikisha

Pepe Kalle kuimba kwenye nyimbo Sola, Mbuta  wakishirikiana na Bella Bella, na kumshirikisha na  Nyboma Mwandido kwenye wimbo Kamale uliopigwa na Orchestra Lipua Lipua .Verckys ndiye chanzo cha Orchestres Baya Baya, Lipua Lipua na  Kiam, matokeo yake ni nyimbo tamu maarufu kama Amba, Mombasa, Niki bue, Mbale, Kamiki, Bomoto na nyingine nyingi sana. Huwezi kumuweka pembeni Verckys utakapotaja mafanikio ya mtindo wa Cavasha, mtindo ulioishika Afrika nzima miaka ya sabini.

Mwaka  1976 Verckys alibadili jina la label  yake kutoka Editions Veve kuwa ZADIS, ambayo ilikuwa kifupi cha Zaire disc.  Kwa lebo hii mpya Orchestra Veve ikatoa nyimbo mbili ambazo zingali zinagusa nyoyo za wapenzi wa muziki wake mpaka leo,  nyimbo hizo ni Papy Baluti na Muana Mburu. Wakati huo Orchestra Veve ilikuwa na wanamuziki wafuatao Tino Muinkwa, Djo Roy, Nejos Tusevo, Pepitho Fukiau kwenye uimbaji, Lambion akiwa anapiga gitaa la solo, Aladji Baba kwenye gitaa la  rhythm, Ndolo na  Celi Bitsou wakiwa wapiga bezi. Kwenye drums alikuweko Bayard, Ponta Vickys kwenye congas, yeye mwenyewe Verckys, Dibuidi na Sax Matalanza wakipuliza Saksafon,  Makamba akiwa anapuliza trombone.  Ni kiasi cha kusikiliza nyimbo hizo mbili ili uweze kujua umahiri wa wanamuziki  waliotajwa.

Mwaka1978  alimrekodi kijana mdogo aliyeitwa Koffi Olomide, hadithi ya Koffi kwa sasa kila mtu anaijua.

MUNGU AMLAZE PEMA NGULI HUYU ALIYELETA FURAHA KWA MAMILIONI YA WATU KATIKA UHAI WAKE

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

1 comment: