Saturday, March 26, 2022

DR UFUTA MPIGA SOLO WACUBAN MARIMBA NA TK LUMPOPO AFARIKI DUNIA

 

Dr Ufuta uzeeni
J
OAKIM UFUTA, mpiga gitaa la solo aliyekuwa maarufu kwa wapenzi wa muziki enzi za Cuban Marimba ya Juma Kilaza, na bendi za Juma Kilaza zilizofuatia amefariki dunia. 
Dr Ufuta ambaye maisha yake ya uzeeni yalikuwa magumu kiasi cha kuwa mlinzi wa wa usiku wa sehemu mbalimbali pale Morogoro, na pia alikuwa fundi baiskeli,  amefariki Ifakara siku ya tarehe 18 March na kuzikwa kesho yake 19 March 2022 hukohuko Ifakara. 

Ufuta alizaliwa  Utuu Misheni Mahenge karibu miaka 70 iliyopita, alianzisha bendi yake ya kwanza mwaka 1966,  bendi yake aliyoiita Taifa Jazz, bendi hii iliyokuwa na waimbaji wanne, ilikuwa haina hata chombo kimoja kilichotumia umeme. Kati ya mwaka 1966 na 1968 hiyo ndiyo ikawa bendi moja maarufu  pale Mahenge. Mbunge wa jimbo la Mahenge wakati huo Mheshimiwa Ilanga, aliwanunulia vyombo vichache vijana hawa na hii ikawa bendi rasmi iliyokuwa ikisindikizana na Mbunge huyo katika kampeni zake mbalimbali.

 Mwaka 1968 kaka yake Lucas Simon alimshawishi aachane na bendi yake ya Taifa Jazz na kujiunga na Cuban Marimba wakati huo ikiwa chini ya Juma Kilaza. Na bendi ya Cuban aliweza kufika mpaka Nairobi ambako wakati wa kurekodi fundi mitambo mmoja pale studio alianza kumuita Dokta kutokana na upigaji wake mahiri na cheo hicho amebaki nacho mpaka umauti wake.

Picha hii ilikuwa ni ganda la moja ya santuri ya nyimbo za Cuban Marimba. Dr Ufuta ni aliyevaa miwani . Wa kwanza kulia waliosimama ni Juma Kilaza.

 Mwaka 1974 kuliktokea kutokuelewana kati ya wanamuziki wa Cubana Marimba na wamiliki wa bendi hiyo ambao walikuwa warithi wa marehemu  Salum Abdallah, mtiti huo ukasababisha Juma Kilaza, Joakim Ufuta, Juma Sangula, Ally Said na Hemedi Maneti kuihama bendi hiyo na kuunda TK Lumpopo, na hapo walitoa nyimbo nyingi za  kukumbukwa, wimbo wao wa kwanza ulikuwa Maisha ya Sasa. Katika bendi hii pia kukatokea kutokuelewana kwa ajili ya maslahi, Hemedi Maneti akatimka  na kujiunga na Vijana Jazz Band, Dr Ufuta akarudi tena Cuban Marimba. Baada ya muda kama ilivyokuwa kawaida miaka ile, bendi ilianza ziara ya  mikoa mbalimbali Kenya. Wakiwa Naivasha kukatokea kukorofishana tena,  wenzie wakarudi Tanzania yeye akabaki akitafuta maisha nchini Kenya.


Ufuta akitengeneza 


Mungu Amlaze pema peponi Joakim Ufuta

No comments:

Post a Comment