Tuesday, November 8, 2011

Bavon Marie Marie


Ganda la Album iliyokuwa na wimbo Maseke ya Meme. Tshimanga Assossa  aliwa wa pili toka kulia


Wimbo Maseke ya Meme ulipigwa katika miaka ya 70 na bendi maarufu ya Negro Success. Kundi lililokuwa likiongozwa na mdogo wake Franco Luambo Luanzo Makiadi, nae si mwingine ila ni mpiga solo mkali Bavon Siongo au maarufu kama Bavon Marie Marie aliyezaliwa May 27, 1944 ambaye pia alitunga wimbo huu marufu. Wimbo huu Maseke ya Meme au kwa Kiswahili ‘Pembe za kondoo’ ulianza kusambazwa March 1970. Mashahiri ya wimbo huu yalileta utata sana baada ya kifo cha Bavon Marie Marie kilichotokea muda si mrefu baada ya wimbo huu kutoka hewani.  Sehemu ya mashahiri ya wimbo huu yalisema hivi;
Bavon Marie Marie
 Nalilia maisha yangu
Sijachoka kuishi
Lakini wanataka nitangulie
Naacha kuongea
Nasubiri kifo.
Bahati mbaya sana Agosti 5, 1970, siku ya Jumatano, Bavon Marie Marie akakumbwa na ajali ya gari iliyosababisha kifo chake katika mtaa wa Avenue Kasavubu, mjini Kinshasa. Wimbo ule ukaonekana kama ni utabiri wa kifo chake mwenyewe. Kwa vile Franco hakufurahia mdogo wake kuingia katika muziki,watu wakatafsiri kuwa alikuwa amemloga mdogo wake ambae alifariki akiwa na umri wa miaka 34 tu. Kuna hadithi nyingine inayosema kifo cha Bavon kilitokea muda mfupi baada ya ugomvi na kaka yake kwa kisa kuwa Franco alikuwa ametembea na Lucy aliyekuwa bibi wa Bavon. Inasemekana Bavon aliondoka spidi na gari akiwa na hasira na muda mchache baadae akaaingia chini ya lori.
Kuna nyimbo nyingi duniani ambazo watu hudhani ni kama utabiri wa wanamuziki kabla ya kufa. Wimbo Ee Mola wangu wa Salum Abdallah wa Cuban Marimba ni mfano mojawapo. Kuna wanamuziki wengi wanaogopa kuimba au kutunga nyimbo kuhusu kifo kwa imani kuwa ukitunga wimbo wa namna hiyo unaita kifo.

5 comments:

  1. asante kwa kutumbusha huyu legend wa muziki wa africa....

    ReplyDelete
  2. Dah! Kumbe Assosa katoka mbali sana.

    ReplyDelete
  3. Bavon aliaga dunia akiwa na umri wa miaka 26 an sio 34 vile umeandika ( yaani 1944 hadi 1970)

    ReplyDelete
  4. Naomba tafasili ya wimbo Philipo wa Madilu system.

    ReplyDelete