Saturday, January 6, 2018

TASNIA YA MUZIKI 2017 KWA UFUPI

Kuanzia mwaka 2012 nimekuwa nikimaliza mwaka kwa kuandika makala ya mtizamo wangu kuhusu hali ya muziki katika mwaka uliokwisha. Na mwaka 2017 ndio huoo umetokomea, ni vizuri kuangalia yaliyopita ili kujitayarisha na yajayo. Kama ilivyokuwa kwa miaka mingi sasa, anga za muziki wa nchi yetu zilitawaliwa na muziki wa Bongoflava. Muziki ambao kwa asilimia kubwa hutengenezwa studio, hakuna shaka watu wengi  nchini na nchi jirani wametokea kuupenda sana muziki huu. Katika mkutano ulifanyika wiki chache zilizopita, kiongozi mmoja wa mambo ya Hakimiliki kutoka  Kenya alisema asilimia kubwa ya muziki unaopigwa kwenye vyombo vyao vya utangazaji ni wa kutoka Tanzania. Imefika mahali mpaka wasanii wa huko wameanza kudai muziki wa Tanzania upunguzwe ili wao waweze kupata nafasi zaidi katika redio na luninga zao. Inachekesha kuwa kilio kama hichohicho kinasikika kwa wanamuziki wa aina tofauti nchini kuhusiana na ‘kufunikwa’ na Bongofleva. Wasanii wa Bongofleva wameendelea kupata tuzo kutoka kwa taasisi mbalimbali za Kimataifa, na hata wengine kuingia mikataba na kampuni kubwa za kimataifa za usambazaji, na kwa picha hii Bongoflava itaendelea kutawala anga za muziki hata mwaka ujao. Muziki ambao tunaweza kusema chanzo chake ni muziki wa mchiriku wenye asili ya ngoma za Kizaramo, maarufu kama muziki wa singeli nao ulikuja juu sana kwa miezi michache ya mwaka huu, japokuwa ule moto wake unapungua, inawezekana muziki huo unajimaliza wenyewe kutokana na mashahiri yanayotumika katika nyimbo hizo, na hata video zinazo ambatana nazo, lakini hakika muziki huu ni ubunifu unaoweza kuitwa muziki wa asili ya Kitanzania bila shaka yoyote. Hakukuwa na mambo ya kushtua sana katika muziki wa Taarab hali hiyohiyo pia ilionekana katika muziki wa dansi. Bendi kadhaa na vikundi vya taarab vilitangaza kuanzishwa lakini havikuja na kitu kipya cha kuweza kuleta mshtuko katika tasnia, kifupi hakukuwa na jambo lolote chanya la kukumbukwa kutoka upande huo kwa mwaka 2017. Pamoja na kuwa haukuonekana kuwa umeshuka lakini pia hakukuwa na dalili za kupanda kwa muziki wa Enjili, kwenye sanaa usipopanda ujue umeshuka. Muziki wa kwaya ulianza kujitokeza zaidi hasa kwenye kutoa elimu ya mambo mbalimbali ya kijamii na pia kurudia nafasi yake ya zamani ya kusifia viongozi mbalimbali, kazi ambayo kwaya ilikuwa ikifanya toka miaka ya mwanzoni baada ya Uhuru. Kwaya kadhaa ziliweza kutengeneza video ambazo zimekuwa zikionekana kwenye luninga, japo ni wazi hazikutengenezwa kwa ajili ya biashara. Kuna kundi la wanamuziki ambao wao husema huwa hawana nia kabisa ya kusikika kwenye vyombo vya utangazaji vya hapa nchini, wao hutengeneza muziki kwa ajili ya maonyesho ya nje ya nchi. Wanamuziki hawa wameendelea kuwa na safari za kwenda nje kupiga muziki wao katika matamasha ya kimataifa bila kuhangaika kutambulisha kazi zao hapa nchini, sababu kubwa ambayo wamekuwa wakitoa ni urasimu wa taratibu za muziki kusikika katika vyombo vyetu vya utangazaji.  Hivyo badala ya kupoteza muda kupingana na mfumo, wao wameendelea na shughuli za kujitambulisha nje, ni nadra habari zao kuonekana kwenye vyombo vya habari vya nchini japo wanazunguka nchi mbalimbali duniani wakipiga muziki unaotambulika huko kuwa ni wa Kitanzania.  Muziki wa asili  ni kazi ambayo inaonekana ni kwa ajili ya watalii na shughuli maalumu za kiserikali au sherehe za kifamilia. Picha hii inadanganya kwani muziki asili unaendelea nchini mijini na vijijini japo hauonekani kwenye vyombo vya utangazaji, labda pale ambapo ni kiburudisho cha viongozi. Muziki wa asili uko katika makundi mawili, uko muziki ambao unafanywa na wasanii ukiwa ni mchanganyiko wa ngoma mbalimbali ili kuweza kuvutia biashara, na uko muziki asili ambao huchezwa na kuimbwa na wenye kabila lao kwa upenzi wa utamaduni wao. Kwa kuwa hauonekani wala kuzungumziwa sana kwenye vyombo vya utangazaji, unaweza ukadhani haupo au haupendwi lakini hilo si sahihi. Maelfu ya vijana nchi nzima wanacheza na kupiga ngoma za kiasili kwa ufasaha mkubwa.
 Kumekuweko na matamasha kadhaa ya muziki nchini, kama tamasha la Fiesta, Marahaba, Tulia Traditional Dance Festival, Sauti za Busara, Karibu Music Festival na kadhalika, lakini matamasha haya ilikuwa ni nafasi ndogo sana ukilinganisha na idadi ya wanamuziki walioko nchini. Wilaya, mikoa nayo ingeweza kutayarisha matamasha yake ya utamaduni ingekuwa sehemu nzuri sana ya kuendeleza utamaduni, wasanii kubadilishana ujuzi, kuibua vipaji na kuleta burudani kwa wananchi  kwa ujumla. Ufadhili katika shughuli za muziki umekua ukiangalia sana faida za kibiashara, kumekuwa na kampuni chache ikiwa zipo ambazo zimefadhili matamasha kwa nia tu ya kuendeleza muziki. Matamasha mengine yamekuwa yakitegemea ufadhili wa balozi mbalimbali za nje kuwezesha kufanya maonyesho ya muziki wetu. Ni kichekesho kwa kweli. Hata zile kampuni ambazo ni maarufu nje ya Tanzania kwa kuunga mkono shughuli za sanaa, kwa namna ya ajabu zikiwa Tanzania ghafla zinakuwa na msimamo tofauti.
Maeneo ya kufanya shughuli za muziki yamezidi kupungua, mengine yamevunjwa na maeneo kuachwa wazi kama vile eneo lilokuwa DDC Magomeni na Mango Kinondoni, mengine yamekuwa makanisa na kadhalika. Pamoja na kuwa kulikuwa na wimbi la kujenga kumbi ambazo hutangazwa kuwa ni ‘multi purpose’, kumbi hizi haswa zilijengwa kwa ajili ya kufanyia shughuli za harusi, kuna mambo kadhaa ambayo si rafiki kwa muziki katika kumbi hizi, na hata wenye kumbi hukataa kumbi zao kutumika kwa shughuli za muziki hasa wa dansi.
 Katika mwaka 2017  Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dr Harrison Mwakyembe amekuwa na mikutano mingi na wanamuziki, jambo jema kinachosubiriwa 2018 ni matokeo ya mikutano hii. Ushauri kwa wanamuziki ambao muziki wao unajikongoja, kuna umuhimu wa kutafuta majibu ya kisayansi kwanini hali iko hivyo. Majibu mepesi ya kulaumu vyombo vya habari, serikali na wadau wengine, kamwe hayata saidia katika kuleta mabadiliko.


No comments:

Post a Comment