Friday, April 28, 2017

SI KWELI KUWA HARRISON SATCHMO SIWALE ALIFIA GEREZANI,


Mar. Harrison Siwale-Satchmo

......................  SIKILIZA HAPA GUITAR LA MZEE SIWALE...................
 
Tarehe 8 September 2013, niliandika katika blog hii habari niliyoipa kichwa cha habari, Harrison Siwale aliishia wapi? Ni habari ya kusikitisha.

Niliandika hivi-----Nimetoka kuongea na Mzee mmoja ambaye nilimuomba anitafutie habari za Harrison Siwale  aka ‘Satchmo’, ambaye alikuwa mpiga rhythm mahiri na maarufu sana katika miaka ya sabini, Harrison alikuwa na staili ya pekee ya upigaji wa gitaa wa kudokoa nyuzi na kupata aina ya pekee ya mlio wa gitaa. Kati ya nyimbo ambazo upigaji huu unasikika ni katika nyimbo za Jamhuri Jazz Band kama vile Mganga 1  na 2, Blandina na kadhalika. Pamoja na bendi nyingine Harisson aliwahi kupigia Atomic na Jamhuri Jazz Band zote za Tanga, na kisha kuvuka mpaka na kuwa na makazi Mombasa kwa muda mrefu ambako aliendelea na muziki. Kwa kadri ya maelezo niliyopewa leo na huyu Mzee niliyemuomba anitafutie habari ili nijue yu wapi huyu mwanamuziki siku hizi? Haya ndio aliyonambia.



'Baada ya kufa kwa yale makundi ya Simba wa Nyika na Les Wanyika, Harrison Siwale alianza kupiga muziki wa Injili katika eneo la Kilifi. Akawemo katika kundi lililokuwa likifanya maonyesho yake katika miji mingi ikiwemo Mombasa na Nairobi. Umahiri wake wa kazi ukamfanya mwenye vyombo vya hilo kundi alilokuwemo Harrison kumuamini sana na kumuachia awe kiongozi wa kundi hilo na kuwa huru kuzunguka sehemu mbalimbali. Inasemekana Harrison akapata tamaa ya kuingia mitini na vyombo vile, hivyo ghafla akapotea. Taarifa zikamfikia mwenye vyombo kuwa vyombo vyake viko njiani kuvushwa kungia Tanzania kupitia mji wa Lungalunga. Mwenye vyombo akaweka mtego hapo na Harrison akakamatwa hapo akiwa na vyombo hivyo, kesi ilifika mahakamani na akahukumiwa kifungo cha miaka mitatu'. Baada ya hapa kuna hadithi mbili, moja ikisema alifia gerezani Shimo la Tewa, na nyingine ikisema alifariki baada ya kumaliza kifungo chake.

Je, nini hasa kilitokea? Najaribu kuwasiliana na watu mbalimbali kupata hadithi zaidi kuhusu mwanamuziki huyu.

HATIMAE (2017 APRIL).... Kwa bahati sana nimeweza kuanza kuwasiliana na mtoto wa Harrison Satchmo Siwale, ambae tuliweza kukutana kupitia facebook. Kijana huyu ambaye jina lake ni Salehe Siwale aliweza kunambia kuwa baba yake alimuoa mama yao na walizaliwa vijana wawili yeye na kaka yake.

Na niliweza kupata taarifa za ziada baada ya kuniunganisha na mama yake ambaye ndie alikuwa mke wa Mzee Siwale nikaweza kuongea nae mubashara kupitia video call ya whatsapp. Kwanza kabisa mama huyo ansema kuwa katika kipindi alichoishi na Mzee Siwale hakuwahi kufungwa wala kuzungumzia kuwa aliwahi kufungwa. Na Mzee Siwale alifariki katika Kitongoji cha Rongai  huko Nakuru na kuzikwa tarehe 31/3/2013. Ukiangalia kuwa taarifa ya awali niliyopewa ilikuwa katika miezi michache baada ya kifo chake, niwazi si kweli kuwa alifia Gerezani na kama angekuwa aliwahi kufungwa hakika mkewe angekuwa anajua.

Mungu Amlaze Pema Mchungaji Harrison ‘Satchmo’ Siwale








Saturday, April 22, 2017

KIFO CHA SOKOINE KILIIKUTA ORCHESTRA MAMBO BADO IKO SHINYANGA


Mwaka 1984 nilikuwa mwanamuziki wa bendi ya Orchestra Mambo Bado, bendi iliyokuwa inaongozwa na Tchimanga Kalala Assossa. Bendi ilikuwa ni moja ya bendi zilizokuwa pendwa wakati huo, mtindo wa bendi ulikuwa unajulikana kama Bomoa. Neno hili lilitokana na wimbo wa Bomoa Tutajenga Kesho, wimbo ambao  baadae kwa sababu ambazo mpaka leo sizijui, ulikuja kupigwa marufuku na Umoja wa Vijana wa Mkoa wa Dar es Salaam wakati ule, usisike kwenye radio ya Taifa, redio ambao ilikuwa pekee wakati huo. Orchestra Mambo Bado ilikuwa na watu ishirini hivi, Tchimanga Assossa kiongozi na mwimbaji. George Mzee muimbaji, Lucas Faustin muimbaji, Jenipher Ndesile muimbaji, Banza Tax muimbaji, Athumani Cholilo muimbaji, John Kitime muimbaji, Likisi Matola mpiga gitaa la bezi, Andre Milongo akipiga gitaa la second solo, Huluka Uvuruge na Kazembe wa Kazembe wapiga gitaa la solo, William Maselenge akiwa kwenye gitaa la rhythm. Kulikuweko na wacheza show wanne, mafundi mitambo watatu na mweka hazina mmoja na meneja wa bendi. Masikani ya bendi yalikuwa katika ukumbi wa Lango la Chuma, Mabibo Dar es Salaam
Tarehe 12 April 1984, kundi zima lilitua katika mji wa Shinyanga baada ya kuwasili hapo kwa treni kutokea Dar es Salaam. Kwa taratibu za miaka hiyo, pamoja na ratiba ya ziara ya bendi kutangazwa kwenye gazeti la Uhuru, meneja wa bendi alikuwa akilazimika kutangulia mji ambao dansi litapigwa kuwahi kufanya mikataba na kumbi  ambazo dansi lingepigwa na pia kufuatilia vibali mbalimbali vya kuruhusu onyesho kufanyika. Mawasiliano yalikuwa magumu na urasimu ulikuwa mkubwa. Haikuwa kazi rahisi maana miaka hiyo ili bendi isafiri ililazimika kupata  kibali cha Afisa Utamaduni wa Mkoa ambao ni masikani ya bendi kuruhusu bendi kutoka nje ya Mkoa na kisha kibali hicho kupelekwa kwa Ofisa Utamaduni wa Mkoa ambao bendi inakwenda, nae baada ya kuruhusu bendi kuingia mkoani kwake, unaomba kibali cha Afisa Utamaduni wa Wilaya unakotaka kupiga muziki ili nae akuruhusu kufanya onyesho kwenye wilaya yake. Baada ya hapo meneja hutafuta na mtu ambaye ana spika ya mkononi, megaphone kuikodisha na kisha kutafuta mtu wa kutangaza onyesho. Ili kubana matumizi kuna mara nyingine wanamuziki wenyewe ililazimika wapite mtaani na spika hiyo kujitangaza. Kulikuwa na mji kama Mpanda wakati huo, ambapo mtangazaji hakuwa na megaphone, mtu maalumu alipita mtaa kwa mtaa akiwa na ngoma ambao aliipiga watu wakikusanyika basi anatangaza ujio wa bendi katika mji wao.
Tarehe 12 April 1984, Orchestra Mambo Bado iliwasili Shinyanga kwa treni ikitokea Dar es Salaam, kuanza ziara ya Kanda ya Ziwa. Wanamuziki tulionyeshwa vyumba vya kulala, mambo yalionekana kuwa yatakuwa mazuri kwa siku ile, matangazo yalikuwa yamebandikwa kwenye nguzo za umeme sehemu mbalimbali za mji, na hali ya kuonyesha kuwa watu walikuwa na taarifa ya ujio wetu ilikuwa dhahiri. Ilikuwa ni muda wa saa kumi hivi ilipotangazwa kuwa nchi imepata msiba mkubwa sana. Waziri Mkuu Edward Moringe Sokoine amefariki katika ajali ya gari jirani na Morogoro. Kwanza ilikuwa ni mshtuko, halafu akili ilipotulia tulijua kuwa na sisi kama bendi tunaingia kwenye tatizo kubwa sana, tulikuwa na nauli ya kuja tu mpaka Shinyanga, na fedha ya kula ya siku moja tulikuwa tunategemea kupiga dansi ili kuweza kulipa malazi ya siku hiyo na kupata fedha ya kula na kuendelea na safari kesho yake, tukitegemea mapato mengine makubwa katika maonyesho ya Mwanza wikiendi iliyokuwa inafuata. Hayo yote tulijua sasa yameharibika, tulirudisha vyumba vyote mara moja na kubaki na viwili tu kimoja kikiwa cha wasichana waliokuwa kwenye bendi, wengine wote ikalazimu tuhamishie mizigo yetu chumba kingine. Baadae tulikaa na Afisa Utamaduni kutafakari kama dansi lingeweza kulia siku ile, na kama halitalia nini hatima ya watu hawa 20 wageni kutoka Dar es Salaam? Kama kiasi cha saa moja jioni, Afisa Utamaduni akaruhusu tupige dansi ili tuweze kupata nauli ya kurudi Dar es Salaam, kwani ilijulikana wazi kitaanza kipindi cha maombolezo ambacho hakuna mtu alijua kitaisha lini,  hivyo hakukuwa na sababu ya kuendelea na safari kutoka hapo. Vipindi vya maombolezo huwa ni vipindi ambavyo pamoja na mambo mengine shughuli za muziki husimamishwa. Kwa wanamuziki na wale wanaotegemea shughuli za muziki na familia zao, kipindi hiki huwa kigumu sana. Lakini kinaleta ukakasi akilini kwani shughuli za kupiga muziki kwenye kumbi husimamishwa, madisco hufungwa na vikundi vya muziki haviruhusiwi kufanya  kazi lakini radio huendelea kupiga muziki uleule ambao umezuiwa kwenye kumbi, sehemu za starehe kama baa huendelea kupiga muziki na kufanya biashara zao bila tatizo ila wanamuziki ndio huzuiwa kufanya shughuli zao kwa maelezo kuwa ni kipindi cha maombolezo. Nakumbuka sana misiba  mikubwa ya viongozi wetu ukiwemo wa Baba wa Taifa kwa sababu kubwa mbili, kwanza uchungu wa kupoteza kiongozi wetu na njaa iliyofuatia baada ya hapo.

Saturday, March 18, 2017

AMRI BILA TAFITI ZINAATHIRI SANA SEKTA YA MUZIKI


KATIKA shughuli ambazo watu wengi huona ni rahisi kuendesha na kutoa maamuzi bila utafiti ni soka na muziki. Ukisikiliza mazungumzo baada ya mechi za soka ndipo utakaposikia watu wanavyotoa ushauri au kukosoa wachezaji, kocha refa, chama cha mpira wa miguu, hakika ingewezekana watu hawa wakapata mamlaka, maamuzi yangekuwa ya ajabu sana.
Hali kadhalika kwenye muziki. Kwa mfano ukiuliza,   kwanini muziki wa bendi hauna umaarufu kama zamani? Hakika ukipita kila mtaa utapata majibu, wengine watakwambia kosa la vyombo vya utangazaji , wengine watakwambia wanamuziki wenyewe , wengine watakwambia serikali, na pia utapewa maelekezo mbalimbali ya nini kifanyike. Bahati nzuri majibu haya ya mtaani hayana madhara kwani huishia hapo hapo. Lakini bahati mbaya huja pale ambapo viongozi wenye mamlaka nao hugeuka wataalamu wa muziki na wao kutoa maamuzi kadri ya mtizamo wao, lakini maamuzi yao huwa amri, na amri inapotolewa bila utafiti wa kutosha madhara yake yanaweza kuendelea miaka mingi baadae. Ninaloweza kusema kwa uhakika, ni kuwa muziki wa Tanzania leo ungekuwa katika nafasi ya juu zaidi duniani kama isingekuwa maamuzi ambayo yalitolewa bila utafiti miaka ya nyuma. Labda nitoe mifano kadhaa. Mpaka miaka ya 70, wanamuziki wa Tanzania walikuwa wakienda sambamba na wanamuziki wa nchi nyingine nyingi Afrika, licha ya kutokuwa na miundo mbinu muhimu katika maendeleo ya muziki kama vile kutokuwa na kampuni za kurekodi na kutengeneza santuri. Lakini kimuziki, wanamuziki wa kipindi hiki walikuwa bega kwa bega na wenzao ambao walikuwa na miundo mbinu stahiki. Tanzania tulikuwa na bendi ambazo zilikuwa  zinapiga muziki wa rumba, nyimbo nyingi za wakati huo mpaka leo bado zinasifika na kupendwa katika anga za muziki. Pia tulikuwa  na wanamuziki vijana ambao wengi wao walikuwa mashuleni, hawa wakiwa na mtizamo mpana zaidi wa kutambulika duniani, wanamuziki hawa kama ilivyokuwa sehemu nyingi Afrika walianza kupiga muziki uliojulikana kama Afro Rock, muziki ambao ulichanganya mahadhi ya muziki asili wa Kitanzania na mapigo ya kizungu, wakifuatia nyayo za kundi la Osibisa, na wanamuziki kama Ransome Fela Kuti. Kukawa na makundi kama Afro 70, Trippers, Sun Burst, The Jets na kadhalika kwa kuyataja machache, makundi ambayo yalianza kuingiza muziki wa Tanzania kwenye soko kubwa zaidi la Kimataifa, kwa mfano wimbo wa Weekend wa Afro70 uliingia kwenye Top Ten Nigeria miaka hiyo, wakati huo muziki wa Nigeria haukuwa na umaarufu wowote nchini kwetu.  Kwa kuwa vijana hawa wengi walikuwa bado shuleni, na kufuatana na maadili ya wakati ule, wanafunzi hawakuruhusiwa  kushiriki madansa ya usiku, hivyo basi kulikuweko na utamaduni wa madansa ya mchana yaliyoitwa Bugi. Hapo vijana walikusanyika kupiga muziki wao kila mwisho wa wiki, shughuli zikianza saa nane mchana na kuisha saa kumi na mbili jioni. Lakini siku moja kiongozi mmoja akatokea na kupiga marufuku Bugi, hivyo kuwaondoa wanamuziki vijana wengi kwenye muziki kwani wasingeruhusiwa kushiriki madansi ya usiku.  Wakati vijana hao wanaacha muziki, vijana wengine Afrika waliendelea mbele. Hata majirani zetu Kenya na Zambia wakawa na wanamuziki wengi walioweza kuingia katika soko la Kimataifa, wanamuziki wetu walikosa fursa hiyo. Pengo hili linaendelea kuwepo mpaka leo. Kuziba pengo hilo kunahitaji kutafiti tulipojikwaa na kuangalia tunafanya nini kurekebisha hali iliyopo. Swala la kupiga marufuku kazi za muziki si jambo geni katika historia ya muziki, kulikuwa na maamuzi kadhaa ya kisiasa pia ambayo pia hayakuwa na utafiti hivyo kudhoofisha maendeleo ya muziki Tanzania. Kwa mfano kulishawahi kutolewa amri ya kupiga marufuku wacheza show, wakati huo karibu bendi zote kubwa za muziki wa rumba kote Afrika Mashariki na Kati zilihakikisha kuwa zinakuwa na kundi la wacheza show, na waimbaji maarufu kama Mbilia Bel na Tshala Mwana wote awali walikuwa ni wacheza show. Kwa kipindi kirefu kulikuweko na sinto fahamu ya wacheza show na ikalazimika taaluma hiyo irudi kinyemela kwani makundi yote ya muziki kutoka nje yalipokuja nchini yalisindikizana na wacheza show. Nyimbo kadhaa ziliwahi kupigwa marufuku na hatimae kuja kuonekana ni za muhimu katika jamii, ukiwemo wimbo maarufu wa Super Matimila, Mambo kwa Soksi, ambao ulipigwa marufuku na baade kuonekana ni wimbo muhimu kuhamasisha watu kutumia kinga katika zama hizi za balaa la Ukimwi. Upigaji marufuku wa tungo unakwaza watunzi na kuishia kutunga nyimbo nyepesi ambazo zina uhakika wa kutokupigwa marufuku. Katika miaka ya karibuni kumewahi kufanyika maamuzi kadhaa yasiyokuwa na utafiti kwa mfano,  serikali iliwahi kununua mashine iliyoitwa Mastering Mixer kwa gharama ya shilingi milioni 50, kwa maelezo kuwa ndio itakayowezesha kumaliza wizi wa kazi za muziki. Sio siri wizi uko palepale. Hayo yalikuwa maamuzi bila utafiti, ni vizuri kujua hiyo ‘mixer’  iko wapi ili kutathmini ni matokeo ya uamuzi huu uliogharimiwa na serikali. Uamuzi mwingine ulikuwa ni ule wa kutunga sheria ya kuweka stempu za TRA kwenye kazi za sanaa, kwa maelezo kuwa utamaliza wizi wa kazi za muziki na filamu. Si mara moja taarifa imatolewa kuwa serikali ilitoa milioni 20 kwa mtafiti toka ‘Chuo Kikuu’ kuhakiki kuwa njia hiyo ndio itamaliza wizi wa kazi za sanaa, hakuna ‘mtafiti’ anayejitokeza kuwa alipokea fedha na kufanya utafiti huo, wala hakuna nakala ya utafiti huo, ni aina nyingine ya maamuzi bila utafiti na matokeo yake wizi wa kazi za sanaa umeenea kila kona nchini na mauzo halali ya kazi za muziki yamepotea. Ushauri tu kwa viongozi kuwa muziki si shughuli ya kubahatisha ina misingi yake, ni muhimu kwa manufaa ya Taifa, umefika wakati wa kufanya utafiti kwanza kabla ya kutoa maamuzi.

Tuesday, January 31, 2017

URAFIKI JAZZ BAND

Mzee Juma Mrisho aka Ngulimba wa Ngulimba liyekuwa Kiongozi wa Urafiki Jazz Band

Pichani toka kushoto waliosimama-Hamis Nguru-mwimbaji, Marifa Ramadhani-Tumba, Juma Saidi- Maracas, Abas Lulela-Bass, Abasi Said -Saxophone, Fida Said-Saxophone, Mohamed Bakari (Churchill)-rythm, Juma Mrisho(Ngulimba wa Ngulimba)-Mwimbaji na Kiongozi wa Bendi.Waliokaa Michael Vicent-Solo gitaa, Ezekiel Mazando-Rythm, Juma Ramadhani Lidenge-second solo na Ayub Iddi- Bass
Bendi ya Urafiki (Urafiki Jazz Band), ilianzishwa mwaka 1970 na kiwanda cha nguo cha Urafiki kilichopo Ubungo. Jina rasmi la kiwanda lilikuwa ni FRIENDSHIP TEXTILE MILL. Kiwanda kilijengwa kwa msaada wa watu wa Jamhuri ya China na kwa urafiki huo kilipewa jina la Friendship Textile. Bendi ilianzishwa ili kutangaza bidhaa hasa Khanga na Vitenge za kiwanda hiki kwani wakati huo kulikuwa na viwanda vingine kadhaa vya nguo nchini kama vile Mwatex, Mutex, Kilitex, na kadhalika


Meneja Mkuu wa kiwanda cha Urafiki Bw. Joseph Rwegasira aliubariki mpango huo wa kuanzishwa bendi ya dansi ya kiwanda na hivyo aliidhinisha malipo ya hundi ya Shs. 50,000/= kununulia seti ya vyombo vya muziki kutoka katika duka la Dar Es Salaam Music House ambalo mpaka leo lipo katika mtaa wa Samora Avenue – Dar Es Salaam.

Ili kupata kundi lililo bora, Menejimenti ya kiwanda cha Nguo cha Urafiki ilimuajiri Juma Mrisho Feruzi maarufu kwa jina la Ngulimba wa Ngulimba na kumuagiza atafute wapigaji kutoka popote ili kuunda kundi imara.. Katika kuhakikisha bendi hiyo mpya inasimama, Ngulimba alichukua wapigaji watano kutoka Orchestre African Qwillado, bendi ambayo aliipigia kabla ya kuanza Urafiki. Na hii ndio maana nyimbo za mwanzoni za Urafiki Jazz Band zilionekana kama zina mahadhi ya Orch. Qwillado.

Wanamuziki aliowachukua Ngulimba kutoka Orch. Qwillado walikuwa ni Michael Vincent Semgumi, mpiga gitaa la Solo, Ayoub Iddi Dhahabu – Besi, Abassi Saidi Nyanga – Tenor Saxophone na Fida Saidi, Alto Saxophone. Ngulimba yeye akawa Muimbaji na pia Kiongozi wa Bendi.

Wanamuziki wengine wa mwanzo ambao waliungana na hao watano waliotoka Orch. Qwillado ambao tayari walikwisha ajiriwa kiwandani Urafiki, walikuwa – Juma Ramadhani Lidenge – Second Solo, Mohamed Bakari Churchil – gitaa la kati (rhythm), Ezekiel Mazanda – rhythm, Abassi Lulela – Besi, Hamisi Nguru – Muimbaji, Mussa Kitumbo – Muimbaji, Cleaver Ulanda – Muimbaji, Maarifa Ramadhani – Tumba, Juma Saidi – Manyanga (maraccass) na Hamisi Mashala – mpiga drums.

Mtindo walioanza nao Urafiki ulijulikana ‘Mchaka Mchaka’ na baadae ukabadilika na kuwa ‘Chaka Chua’ na hatimae mwisho mwisho bendi inaelekea ukingoni walipiga mtindo wa ‘Pasua’ na ‘Patashika’

Mwaka 1971 Gidion Banda, mwanamuziki kutoka bendi ya Morogoro Jazz alijiunga na kundi akiwa mpigaji wa Saxophone.

Aidha, Bendi ya Urafiki ilipitiwa na wanamuziki wengi baadhi wakiwemo Gideon Banda mpuliza saxophone kutoka Morogoro Jazz wengine wakiwemo Thobias Cosmas Chidumule na Frank Mahulu – Waimbaji waliotokea Western Jazz (Saboso) mwaka 1973 na kuongeza nguvu katika safu ya uimbaji. Waimbaji hao walishiriki nyimbo nyingi baadhi zikiwa Tausi Karuka, Jembe na Panga (Geza Ulole), Kosa la Nani, Mauaji ya Soweto, Rukia Hukusikia, Maonyesho ya Mtu Mweusi n.k.

Pia waliongezeka Mkali na Hidaya kutoka Morogoro wakipuliza matarumbeta, hao walikuja 1973 na Ali Saidi alietokea Cuban Marimba akipiga gitaa la kati (rhythm) na baadae mwaka 1975, Mganga Hemedi kutoka Tanga, akitokea Atomic Jazz, nae alijiunga na kuwa upande wa solo na rhythm.

Urafiki Jazz imetunga nyimbo nyingi, zaidi ya mia tatu zinazoelekeza kwenye siasa, mapenzi, nasaha na mafundisho na pia kukosoa. Baadhi ya nyimbo zake za siasa zilizopata umaarufu ni kama zile Mwenyekiti Nyerere, Mauaji ya Soweto, Jembe na Panga n.k..

Mwaka 1975 Bendi ilishiriki katika mashindano ya bendi za muziki wa dansi yaliyofanyika Mnazi Mmoja – D’Salaam na kushika nafasi ya tatu na Mzee Ngulimba, kama Kiongozi wa Urafiki aliiwakilisha Tanzania pamoja na bendi ya Afro 70 iliyopata nafasi ya kwanza na baadhi ya vikundi vya utamaduni kutoka Tanzania Bara na Zanzibar nchini Nigeria katika maonyesho ya mtu mweusi yaliyofanyika huko.

Saturday, November 12, 2016

RAJABU OMARY KUNGUBAYA APATA MGUU WA BANDIA KUTOKA KWA WAPENZI WA MUZIKI WA ZAMANI


Marehemu Omary Kungubaya
Rajabu Kungubaya
Rajabu Omary Kungubaya, mtoto wa marehemu Omary Kungubaya, mwanamuziki ambaye alipata umaarufu kutokana na wimbo wake wa ‘ Salamu za wagonjwa’ uliokuwa wimbo wa kufungua na kufunga kipindi cha salamu za wagonjwa kilichokuwa kikirushwa na Radio Tanzania, leo amepokea mguu wa bandia ili kumsaidia kutokana na mguu wake wa kulia kuwa umekatwa kutokana na ajali ya bodaboda. Wanamuziki John Kitime na Mjusi Shemboza walimuona Rajabu kwa mara ya kwanza siku walipoenda kumzika Mzee Kungubaya na kuona umuhimu wa kumsaidia Rajabu kutokana na  hali yake ya kutegemea magongo wakati wa kutembea. Kwa kutumia kundi a Whatsapp la ZAMA ZILE, (kundi la wapenzi wa muziki wa zamani wanaosikiliza kipindi cha ZAMA ZILE kinachoendeshwa na John Kitime kupitia EFM 93.7fm kila Jumapili kuanzia saa 2-5 usiku), wanakikundi waliweza kuchanga fedha zilizowezesha kijana huyu kupata mguu wa bandia.
 Rajabu ni mchangamfu anaeonekana kupendwa na kila mtu, kutokana na majirani zake wote kumuunga mkono ikiwemo serikali ya mtaa wake. Mwenyekiti wa serikali ya mtaa akiwa na wajumbe wengine wa serikali ya mtaa wake wote walimsifu kwa tabia yake ambayo walisema ilikuwa ni mfano hasa kwa jitihada zake za kutunza familia yake. Mke wa marehemu Mzee Kungubaya, ambaye ni mama mzazi wa Rajabu alisema yeye alikuwa anategemea kuishi kwa kufanya kazi za kibarua katika sehemu ambazo kuna ujenzi unaendelea, hufanya kazi kama kubeba maji na zege kuwasaidia wajenzi. Marehemu Kungubaya ameacha watoto wakiwemo wadogo ambao mmoja yuko shule ya chekechekea na mwingine darasa la 6, wote hawa wanamtegemea sasa kaka yao ambae ana mguu mmoja. Rajabu alikatika mguu kutokana na gari kuovertake na kumfuata upande wake na kumgonga wakati akiwa kwenye bodaboda, aliyemgonga, jina na namba ya simu ipo aliahidi kumsaidia lakini hajatimiza ahadi zake kwa kijaa huyu aliyempa ulemavu wa maisha.


Saturday, October 29, 2016

EXCLUSIVE- ANGALIA PAMBAMOTO LILIVYOKUWA LIKICHEZWA MIAKA YA 90 -VIDEO

VIJANA DAY kila Jumapili mchana Vijana Jazz Band walikuwa wakipiga katika ukumbi wa Vijana Social Hall Kinondoni na hii ilikuwa mojawapo ya raha ukumbini. Aina ya uchezaji hakika ni tofauti na leo.
 Jukwaani wapiga magitaa
Miraji Shakashia- solo
John Kitime- Rythm
Manitu Musa - Bass
Drums- Juma Choka
Sax Rashid Pembe na Said Mohamed Ndula
Trumpet- Mawazo Hunja na Tuba
Uimbaji
Jerry Nashon, Mohamed Gotagota, na Abdallah Mgonahazelu 

TOA MAONI

Friday, October 21, 2016

MAZISHI YA MZEE KUNGUBAYA

MWANAMUZIKI mkongwe ambaye alipata umaarufu kutokana na wimbo wake Salam za Wagonjwa amezikwa leo katika makaburi ya kifamilia Njeteni Kwembe. Msiba huo ulihudhuria na watu wengi wakiwemo majirani, ndugu, wanamuziki na wapenzi wa muziki wa Mzee Kungubaya.Tatu itakuwa siku ya Jumamosi 22/10/2016.
Jeneza likiwa nje ya nyumba ya marehemu

Mwanamuziki Mjusi Shemboza akiongea na mmoja wa watoto wa marehemu Mzee Kungubaya




Mjusi Shemboza akiwa na Mtendaji Mkuu wa COSOTA wa zamani Mzee Mtetewaunga

Msafara wa kuelekea makaburini



Mazishi ya Mzee Kungubaya

Thursday, October 20, 2016

BURIANI OMARY KUNGUBAYA

kungubaya
Mzee Omari Kungubaya akipiga gitaa siku ya mkesha wa msiba wa Dr. Remmy Ongala
MZEE Omari Kungubaya ambaye atakumbukwa kwa wimbo wake Salam za wagonjwa, wimbo uliokuwa ukiashiria kuanza na kuisha kwa kipindi cha salamu za wagonjwa kupitia Radio Tanzania kwa miaka mingi amefariki leo mchana baada ya afya yake kuwa si nzuri kwa muda mrefu. Msiba wake uko nyumbani kwake Njeteni, Mbezi ya Kimara Habari zaidi tutawaleteeni Mungu amlaze pema peponi

Friday, October 7, 2016

BURIANI SALOME KIWAYA


Picha iliyopigwa Uingereza wakati Salome alipoenda huko na Shikamoo Jazz Band. Toka Kushoto Marehemu Salome Kiwaya, Marehemu Papa Wemba, na Marehemu Bi Kidude Mungu awalaze pema.
Kwa masikitiko makubwa nimepokea taarifa za msiba wa Mama Salome Kiwaya, mwanamuziki mkongwe. Taarifa zilinifikia kuwa Salome amefariki katika ajali ya gari iliyotokea Dodoma sehemu za Meriwa. Nilimfahamu Salome kwa mara ya kwanza mwaka 1987, wakati nikiwa bendi ya Tancut Almasi Orchestra, tulipopiga kambi Dodoma Hotel kwa muda wa miezi mitatu, tukitoa burudani kwanza kwa wajumbe wa mkutano wa Kizota, kisha wenyeji wa mji wa Dodoma. Katika kufahamiana  kipindi hicho, tuliweza hata  kupiga wimbo wake mmoja ulioitwa Tuhina, uliokuwa ukiimbwa na Kasaloo Kyanga na Kyanga Songa, ambao nao ni marehemu. Siku moja nilipita mtaani Dodoma na kununua kanda za muziki wa Salome, nilizipenda sana nyimbo zake na nikamuahidi kuwa ningejitahidi kuzipeleka kwa watu wenye uwezo wa kuendeleza kazi zile. Nilizipeleka kanda kwa Ronnie Graham, Mscotch mmoja mwenye upenzi na uelewa mkubwa wa muziki wa Kiafrika na hasa rumba, na huyu Mscotch ndie aliyewezesha kuanzishwa kwa bendi ya Shikamoo Jazz Band. Baada ya kuzisikia nyimbo zile akaamua kuwa Salome asindikizane na bendi ya Shikamoo kwenye ziara yao ya Uingereza kama muimbaji wa kike. Salome alienda Uingereza na aliporudi ndipo alipoanza kununa vyombo na kuunda kundi la Saki Stars, ikiwa ni kifupi cha Salome Kiwaya Stars. Mume wake Mzee Kiwaya nae ni msanii maarufu aliyekuwa kiongozi wa kikundi cha Utamaduni cha CDA miaka hiyo ya 80. Kuanzia hapo nimekuwa karibu sana na Salome, miaka ya 90 wakati nikiwa Mwenyekiti wa CHAMUDATA, Salome ndie alikuwa mwenyekiti wa chama hicho katika mkoa wa Dodoma baada ya mkutano mkubwa wa wanamuziki uliofanyika mwezi June 1998, kule Bagamoyo, ambapo wanamuziki 265 waliweza kukusanyika pamoja na kukaa siku nne katika mji wa Bagamoyo wakifanya warsha za fani mbalimbali za muziki. Katika miaka ya karibuni Salome alishughulika na sanaa ya urembo akiwa wakala wa Miss Tanzania kwa kanda ya Kati na kuweza kutoa MIss Tanzania mmoja, baadae aliingia katika siasa na kufikia kuwa Mwenyekiti wa UWT wa Mkoa wa Dodoma, lakini aliendelea na muziki katika maisha yake yote.

Mungu Amlaze Pema Salome Kwaya. Ucheshi wako hatutausahau. 
JOHN KITIME

Friday, September 23, 2016

TANGA MJI ULIKOANZA MUZIKI WA DANSI


Wiki hii nilipata bahati ya kutembelea mji wa Tanga, mji ambao  sifa zake zilianza kusikika kuanzia enzi za utawala wa Wajerumani, jiji ambalo shule ya kwanza ya serikali ilijengwa hapa enzi hizo hizo za utawala wa Wajerumani, jiji ambalo liliendelea kukua sana kutokana na kilimo cha katani na hivyo kukusanya vijana toka kila kona ya nchi kuja kutafuta kazi katika mashamba makubwa ya katani wakati huo. Tanga mji ambao kutokana na uwingi wa vijana wakati huo, shughuli za burudani ya muziki nazo zilifikia kiwango cha juu kuliko sehemu nyingi Tanzania.
Ukizungumzia historia ya muziki wa dansi, huwezi kukwepa kuzungumzia Tanga, kwani historia inatueleza kuwa kabla ya kuanza vikundi vya muziki wa dansi kulianzishwa klabu za kucheza dansi. Klabu hizo zikitumia muziki wa santuri, wanachama wake walicheza na hata kushindana kucheza muziki kwa mitindo mbali mbali ya kigeni ikiwemo waltz, tango, chacha, rumba na kadhalika. Klabu za kwanza nchini zilianzia Tanga. Kulikuwa na klabu kama Young Noverty miaka michache baada ya vita ya kwanza ya dunia, wakati huo nchi ya Tanganyika ikiwa bado changa kabisa. Mtindo huu wa vilabu vya dansi ulienea na baadae kuingia Dar es Salaam na miji mingine iliyokuwa imeshaanza wakati huo. Vilabu hivi ndivyo baadae vikaanzisha vikundi vya kwanza vya muziki wa dansi. Hata majina ya vikundi hivyo vya kwanza yalihusiana na klabu za burudani za wakati huo. Kulikuwa na vikundi kama Coast Social Orchestra, Dar es Salaam Social Orchestra na kadhalika.  Hivyo mji wa Tanga ulikuwa katika ndoto za vijana enzi hizo. Kwa vile vijana wengi walikusanyika katika jiji hili nchi, kulianzishwa pia klabu ambazo zilikuwa kwa ajili ya vijana waliokuwa wakitoka kabila moja. Klabu hizo zikiwa na nia ya wananchama wao kusaidiana katika shida na raha, na vilabu hivi pia vilikuwa ni sehemu muhimu katika kutoa burudani kwa vijana waliotoka sehemu moja. Kati ya klabu hizi kulikuweko na klabu iliyoitwa Young Nyamwezi, kama jina lake lilivyo ilikuwa ni klabu ya vijana kutoka Unyamwezini. Hatimae mwaka 1955 klabu hii ilianzisha bendi yake iliyoitwa Young Nyamwezi Band, bendi hii ilikuja kukua na baada ya Uhuru ilibadili jina na kuitwa Jamhuri Jazz Band. Hakika kwa vijana waliokuwa wapenzi wa muziki miaka ya 60 na 70 ilikuwa lazima uifahamu Jamhuri Jazz Band, muziki wake, au kwa lugha ya enzi zile, ‘vibao’ vyake vilijulikana Afrika ya Mashariki nzima. Bendi hii ilikuwa ikibadili mitindo ya upigaji wake na kupiga katika mitindo ya ‘Toyota’ na hatimae ‘Dondola’. Aliyekuja kumiliki bendi hii, ambayo wapenzi wake pia waliita JJB alikuwa Joseph Bagabuje,  kulikuwa hata maelezo wakati fulani kuwa JJB ilikuwa kifupi cha Joseph Jazz Band na si Jamhuri Jazz band. Kama ilivyokuwa kawaida ya bendi za wakati ule Jamhuri Jazz Band ilisafiri sana na kufanya maonyesho katika kila kona ya nchi yetu, jambo hilo pamoja na kuwa bendi hii ilirekodi na kutoa santuri kupitia kampuni za kurekodi za Kenya na pia kurekodi nyimbo zake katika radio ya Taifa uliifanya bendi hii kuwa maarufu sana. Upigaji wa aina ya pekee wa gitaa la rhythm wa bendi hii, ambao uligunduliwa na Harrison Siwale, maarufu kwa jina la Sachmo, uliigwa na wapiga magitaa ya rhythm wengi nchini. Uimbaji wa kutumia waimbaji wawili tu, uliopendelewa na bendi za Tanga wakati huo ikiwemo bendi nyingine maarufu wakati huo, Atomic jazz Band, ulikuwa ni wa aina yake pia. Jamhuri Jazz Band pia ndio kilikuwa chanzo cha bendi maarufu ya Simba wa Nyika na bendi zilizozaliwa baada ya hapo. Nilibahatika kukutana mtu aliyekuweko siku ya kwanza ya safari ya kuja kuzaliwa kwa Simba wa Nyika, hakika ni hadithi yake ilikuwa ya kusisimua. Inasemekana kuwa siku hiyo Jamhuri Jazz Band ilikuwa imekodishwa kwa ajili ya kupiga kwenye harusi kule Muheza. Wanamuziki walikuwa wakilazimika kukusanyika katika jengo la klabu lililokuwa Barabara ya 15 ili kupata usafiri wa kwenda  Muheza. Siku hiyo wanamuziki wengine walikusanyika lakini George na Wilson Peter, Luza Elian a wengine wachache hawakuonekana, baada ya upelelezi mfupi ikajulikana kuwa wamejificha au wameondoka mjini Tanga, hivyo ikalazimika kutafuta wanamuziki viraka wa haraka haraka kuweza kufanikisha onyesho la siku hiyo, msimuliaji alinambia kuwa japo yeye hakuwa mwanamuziki bali shabiki tu wa bendi aliweza kupanda jukwaani na kuimba katika harusi hiyo, hali haikuwa mbaya kwani alijitokeza mteja mwingine akitaka bendi ikapige kwenye harusi yake pia, lakini ombi lake lilikataliwa kwani wanamuziki walijua kuwa hawakuwa kwenye kiwango chao. Na baada ya hapo kikaanza kipindi kigumu kwa Jamhuri Jazz Band kujitahidi kurudisha hadhi na ubora wa bendi, na pia ikaanza safari iliyokuja kubadili historia ya muziki wa dansi Afrika mashariki kwa vijana hawa waliotoroka kuelekea Arusha ambako walianzisha Arusha Jazz Band na hatimae kuvuka mpaka na kuingia Kenya ambako walianzisha Simba wa Nyika ambayo  mafanikio yake yanatingisha hisia za wapenzi wa muziki wa dansi mpaka leo.


Wednesday, September 14, 2016

JAMHURI JAZZ BAND


Kwa mara ya kwanza niliwaona 'Live', Jamhuri Jazz Band wakipiga katika ukumbi wa Community Centre Iringa, ukumbi maarufu kwa wenyeji wakati huo kwa jina la Olofea senta (Welfare Centre). Ni vigumu kuelezea jinsi nilivyokuwa najisikia kwani nilikuwa sidhani kama kutakuja kuweko na wanamuziki wanapiga vizuri namna ile. Lakini katika wote mpiga rythm guitar Harison Siwale, aliyejulikana kwa jina la Satchmo, alikuwa na anabakia kuwa mpiga gitaa aliyenifurahisha kuliko wote. Kwanza alikuwa na staili ya peke yake, na mpaka leo nikisikiliza nyimbo zake kama vile Blandina, Mganga no 1, Maria bembeleza mwana au Ewe ndege, nabaki kusifia kuwa huyu bwana alikuwa na kipaji cha pekee. Kuna rafiki yangu aliwahi kumuuliza wakati ule huwa anapataje mawazo ya kupiga gitaa lake kwa staili ile? alijibu kuwa huwa anajaribu kupiga sauti za viumbe mbalimbali wa porini katika gitaa lake.
Wanamuziki waliokuwa katika bendi ya Mkwawa High School,  Manji, Sewando, Danford Mpumilwa, Askofu Kakobe watakumbuka jinsi walivyoweza kupata nafasi ya kupiga pamoja na bendi hii kila ilipokuja Iringa mjini, maana hizo ndiyo zilikuwa taratibu wakati huo lazima bendi kubwa ikija, wanamuziki wadogo huomba Kijiko, na kama unaweza kuimba au kupiga vizuri unaachiwa nafasi ili muhusika akatafute mpenzi. Bendi ikifika katika mji, kama mji ule una bendi basi nao watapata nafasi ya kushirikiana na wageni.  Bendi hii ilianza kwenye miaka ya 50 ikiwa ikijulikana kama Yanga Nyamwezi Band, Kiukweli ilikuwa ni Young Nyamwezi Band, bendi iliyokuwa imetengenezwa kwa ajili ya Vijana toka Tabora waliokuja kukata mkonge katika mashamba ya mkonge yaliyokuweko Tanga miaka hiyo. Na baada ya Uhuru ikajulikana kama Jamhuri Jazz Band, kifupi JJB japo kifupi hicho baadae kilidaiwa kuwa kilikuwa kifupi cha jina mwenye bendi Joseph Bagabuje. Wakati wa uhai wa Jamhuri Jazz bendi Tanga kulikuwa kuna waka moto kwa vikundi maarufu katika Afrika ya Mashariki kuwa vyote katika mji huo. Atomic Jazz, Amboni Jazz, Lucky Star, Black Star. Kwa vyovyote Tanga ulikuwa mji wa starehe wakati huo, hasa ukikumbuka kuwa kulikuweko na bendi nyingine ambazo hazikuwa maarufu labda kutokana na aina ya muziki zilizokuwa zinapiga. Kama vile ile bendi ya Magoa The Love Bugs ambayo ndiyo hatimae ilikuja kuwa The Revolutions na sasa Kilimanjaro Band
Mbaruku Hamisi,Abdallah Hatibu, Zuheni Mhando

Eliah John, Alloyce Kagila, Musa Mustafa

Yusuf Mhando, Joseph Bagabuje, Rajabu Khalfani


George Peter, Harrison Siwale, Wilson Peter

Thursday, September 8, 2016

WESTERN JAZZ BAND MOJA YA BENDI ILIYOKUWA MAARUFU TANZANIA

Mzee Iddi Nhende ndiye aliyepata wazo la kuanzisha bendi maarufu ya Western Jazz. Iddi Nhende alianza muziki akiwa bado mdogo katika bendi ya shule alipokuwa Primary huko Nzega, mwaka 1944 alijiunga na Tabora Boys Secondary na hapa akajiunga na Brass Band ya shule ambapo alikuwa mpigaji wa Cornet. Alimaliza shule na kuja Dar es Salaam kujiunga na Chuo cha Afya, Sewa Haji Medical Training Center. Baada ya kumaliza mafunzo akaajiriwa Bohari ya madawa na kisha mwaka 1957 alihamishiwa Muhimbili. Upenzi wake wa muziki ulimfanya mwaka huohuo ajiunge na Rufiji Jazz Band kama mpiga trumpet, bendi hii wakati huo ilikuwa ikifanya maonyesho yake Minazini Community Centre iliyokuwa eneo linaloitwa siku hizi Mchikichini na pia walikuwa wakipiga muziki katika ukumbi wa Arnatougro.
Kutokana na miji kuwa ndio ilikuwa inaanza, watu wengi kutoka maeneo mbalimbali walihamia mijini na kujaribu kutafuta wenzao waliotoka sehemu moja na kuwa na vikundi vya kusaidiana au kuwaunganisha, watu wa sehemu mbalimbali walianzisha bendi wakazipa majina ya wanakotoka, hivyo waanzilishi wa Rufiji Jazz walitoka Rufiji, na ndivyo ilivyokuwa kwa Kilwa Jazz, Ulanga jazz na kadhalika. Hivyo Iddi Nhende aliyekuwa ametoka Nzega akaamua kuanzisha bendi ya watu kutoka Magharibi, kwa kuwa nchi ilikuwa imegawanywa katika majimbo, yakiweko majimbo kama Northern Province, Southern Highlands Province, Western Province na kwa vile Nhende alitoka Western province akaanzisha Western Jazz Band 1959. Akanunua vyombo aina ya Grampian toka duka la Souza Junior duka la vyombo vya muziki lililokuwepo mtaa wa Mkwepu. Aliweza kupata fedha baada ya kuuza ng’ombe kadhaa wa mamake. Wakati huo katika bendi za aina yake ni Dar es Salaam Jazz Band peke yake waliokuwa na magitaa ya umeme, hivyo Nhende akawa na kazi ya kuwatafuta wapigaji ambapo alimfuata mpiga gitaa la umeme wa kwanza Haus Dibonde(Msukuma), aliyekuwa anapigia Dar es Salaam Jazz Band(hii ilikuwa chini ya Mzee Muba), baada ya hapo akawapata wanamuziki wengine kutoka Ulanga Jazz Band, wakati huo chombo cha banjo kilikuwa muhimu hivyo akamtafuta mpiga banjo toka Cuban Marimba tawi la Dar es Salaam. Cuban Marimba wakati huo ilikuwa na tawi Dar Es Salaam lililokuwa chini ya Mzee Mwaipungu. Mwaka mmoja baadae alipata transfer ya kwenda Morogoro, hivyo huku nyuma alilazimika kuongeza wasanii ili kuimarisha bendi wakati hayupo. Akampata David Makwaya mwimbaji, na Ally Rashid(huyu ameacha muziki karibuni akiwa Msondo), mpiga Saxaphone toka Zanzibar. Bahati mbaya yule mpiga gitaa Haus akapata kichaa katika mazingira yaliyohusishwa na ushirikina kutokana na ushindani wa bendi uliokuwepo. Hivyo basi walifuatwa wanamuziki watatu toka Tabora Jazz, wanamuziki hao walikuwa wametoka pamoja katika bendi iliyokuwa na makazi Mwanza ikiitwa Kimbo Twist Band na wakahamia Tabora Jazz, na kutoka hapo wakachukuliwa na Western Jazz. Wanamuziki hao walikuwa
Rashid Hanzuruni, Kassim Mponda na Omary Kayanda. Baada ya kazi nzuri sana, Hanzuruni Nae akarukwa na akili katika mazingira yale ya yule mpiga solo wa kwanza akalazimika kurudishwa Tabora ambako alikaa mpaka mauti yake. Wema Abdallah akachukua nafasi ya mpiga solo katika bendi ya Western. Tatizo la kinidhamu lilifanya Wema aondolewe Western, na mpigaji mwingine mzuri sana Shamba Abbdallah akachukua nafasi, solo la huyu bwana linasikika kwenye nyimbo ka Rosa na kadhalika.
Hall la nyumbani la Western Jazz lilikuwa Alexander Hall, ambalo lilikuja kuwa hall la DDC Kariakoo. Western walinunua drums baada ya Kilwa Jazz kununua drums na kuzipitisha kwao kuwaringia. Walinunua toka kwa bendi moja ya Wagoa iliyoitwa De Mello Brothers. Western walirekodi santuri kadhaa chini ya mkataba waliyousaini na lebo ya Phillips ya Kenya. Hatimae Western na mtindo wao wa Saboso walitoweka katika anga za muziki miaka ya mwisho ya sabini. Kati ya nyimbo zao nyingi ni hizi hapa; Rosa, Vigelegele, Jela ya Mapenzi, Helena no 1 na 2.

Saturday, August 20, 2016

MAZISHI YA BI SHAKILA , YATAFANYIKA LEO MBAGALA CHARAMBE

Mazishi ya Bi Shakila yatakuwa leo Jumamosi 20 AGOSTI 2016. Mbagala Charambe, saa kumi alasiri Uwanja wa Ninja.
 Namna ya kufika msibani nyumbani kwa marehemu kwa kutumia daladala. Unapanda magari ya Mbagala Rangi Tatu, ukifika mwisho unachukua basi la Nzasa na unashuka Mnara wa Voda hapo unauliza kwa Bi Shakila utaonyeshwa