Friday, December 13, 2013

GURUMO 53-TAMASHA LA KUSTAAFU MUHIDIN MAALI GURUMO

Wanamuziki kadhaa wenye heshima katika muziki wa dansi watakuweko katika Tamasha la Gurumo 53, ambalo ni tamasha la kustaafu muziki  mwanamuziki mkongwe Muhidin Maalim Gurumo. Kati ya wanamuziki watakao panda jukwaani ni  Komandoo Hamza Kalala, Mzee Makassy, wanamuziki nyota waliowahi kutamba na bendi ya DDC Mlimani Park , Cosmas Chidumule, Abdallah Gama, Hussein Jumbe, Mashaka Shaaban, Kalamazoo, Henry Mkanyia na Karama Legesu. Wengine ni Ali Yahaya na Boniface Kachala, Tshimanga Kalala Assossa, Shaaban Lendi na Ibrahim Mwinchande. Pia wapulizaji wakongwe Majengo na King Maluu watakuweko na wote kwa pamoja wataporomosha show kubwa Jumamosi hii ndani ya TCC Club Chang’ombe. Wakali hao  jana Alhamisi walihitimisha mazoezi ya nyimbo tano watakazopiga katika tamasha hilo. Mazoezi hayo makali yalifanyika Amana Club ambako kwa wiki nzima wanamuziki watakaoshiriki tamasha hilo wamekuwa wakikutana hapo na kupiga mazoezi ya kufa mtu. Baadhi ya nyimbo zilizofanyiwa mazoezi ni  pamoja na “Selina” utunzi wake Gurumo kwa kushirikiana na marehemu Joseph Mulenga, “Barua kutoka kwa Mama” uliotungwa na Cosmas Chidumule na “Gama” (Tshimanga Kalala Assossa). Tamasha la Gurumo 53 ni maalum kwa ajili ya kuhitimisha miaka 53 ya utumishi uliotukuka katika muziki wa dansi kwa Muhidin Maalim Gurumo ambaye ametangaza rasmi kustaafu muziki. Wasanii wengine wanaoshiriki mazoezi hayo ni Miraji Shakashia, Hafsa Kazinja, Juma Katundu, Edo Sanga. Burudani zingine zitakazokuwepo siku hiyo ni pamoja na bendi za Msondo Ngoma Music Band, Talent Band, na Twanga Pepeta.

No comments:

Post a Comment