Monday, August 5, 2013

LEO TUNATIMIZA MIAKA 43 TOKA SIKU ALIPOFARIKI BAVON MARIEMARIE




Bavon Marie Marie, mdogo wake Franco Luambo,
alizaliwa May 27, 1944 katika jiji la Kinshasa na kupewa jina la Siango Bavon Marie Marie. Alipokuwa mdogo hakuwa mtukutu lakini alikuwa na akili sana, akajulikana sana kwenye eneo alilokulia   wilaya ya Bosobolo. Kadri alivyokuwa akaanza kuishi maisha ya  makeke zaidi kwa kuwa mlevi mzuri wa pombe na msafi aliyechichumbua kisawasawa kama ilivyokuwa desturi ya vijana wa Kinshasa wakati ule. Kama alivyokuwa kaka yake Franco Makiadi naye alikuwa mpiga gitaa mzuri sana. Alipigia bendi kama Cubana Jazz akiwa na mwanamuziki Bumba Massa, akapigia Orchestre Jamel kabla ya kuingia Negro Succes, bendi ambayo ilianzishwa 1960 za Vicky Longomba (Baba wa Awilo Longomba). Vicky aliwahi kuwa mmoja wa wanamuziki wa TP OK Jazz, sasa yeye  pamoja na wenzie Leon’ Bholen’ Bombolo, na mwimbaji mwenzie Hubert ‘Djeskin’Dihunga, mpiga sax Andre Menga, rhythm Jean Dinos, mpiga bezi Alphonse ‘Le Brun’ Epayo, mpiga drum Sammy Kiadaka na mwimbaji mwingine Gaspard ‘Gaspy; Luwowo wakaanzisha hiyo bendi kali kabisa  Negro Succes . Bavon akawa mpiga gitaa wa bendi hii baada ya mwaka 1965, yeye na mwenzie Bholen wakawa viongozi na masupastar wa wakati huo kwa vijana wa Kinshasa. Pamoja na kuwa kaka yake Franco  ndie aliyekuwa akijulikana kama Mwalimu Mkuu wa Rhumba la Kongo yeye pia alikuwa kipenzi  vijana kutokana na upigaji wa solo lake lililokuwa na uchangamfu zaidi .


Tarehe 5 Agost 1970 Bavon Marie alifariki katika ajali ya gari baada ya ugomvi uliotokana na mpenzi wa Bavon aliyeitwa Lucy, ambapo Bavon alimshutumu kaka yake kuwa kalala na mpenzi wake huyo. Ajali hiyo ilisababisha Lucy akatike miguu. Kuna watu wengine wanasema kisa kilikuwa ni ulevi tu wa Bavon ulisababisha bendi yake ishindwe kufanya show nae akawa kakasirika kwa hilo na kuendesha gari kwa fujo na kuishia chini ya uvungu wa roli kwenye njia panda. Pamoja na upigaji wa gitaa Bavon pia alikuwa mtunzi mzuri sana wa mashahiri ambayo yaliwagusa watu. Kwa mfano wimbo wake wa 'Mwana 15 Ans'…Mtoto wa miaka 15, Bavon aliongea kama binti wa miaka 15 ambae ana uchungu kwa kuwa familia yake inamtafutia mchumba japo yeye anataka kwenda shule. Hadithi ambayo wote tutakubali mpaka leo inamaana sana katika jamii za Kiafrika

No comments:

Post a Comment